Habari za Punde

Ukosefu wa Uadilifu Uliitia Dosari Sekta Binafsi - Majaliwa.

Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa akifungua Mkutano Mkuu wa 18 wa Mwaka Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania TPSF, akimuwakilisha Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. John Magufuli, uliofanyika katika Ukumbi wa Hoteli ya Serena Jijini Dar es Salaam


Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa. akiwa katika Picha ya pamoja na Washriki wa Mkutano Mkuu wa 18 wa Wanachama wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF). leo Agosti 28/2018 Jijini Dar es salaam.
(Picha na Ofisi ya Wazri Mkuu )

Na.Khadija Mussa.OWM. 
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema ukosefu wa uadilifu ni moja ya eneo ambalo lilitia doa utendaji wa sekta binafsi hususan pale ambapo ilishirikiana na Serikali.

Ameyasema hayo leo (Jumanne, Agosti 28 ,2018) wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 18 wa mwaka wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) kwa niaba ya Rais Dkt. John Magufuli.

Katika mkutano huo uliofanyika kwenye Hoteli ya Serena, jijini Dar Es Salaam, Waziri Mkuu amesema uadilifu ni changamoto kubwa inayopaswa kufanyiwa kazi na Serikali na TPSF.

“Katika kusisitiza suala la uadilifu, nitoe rai kwamba muwe na mfumo wa kujitathmini,kupeana alama chanya na kuhimizanakuenenda katika misingi bora ya uendeshaji wa shughuli zenu.”

Kadhalika, Waziri Mkuu ameitaka TPSF ijifunze kwa wenzao walioendelea kwa kutokuwa na vitendo vya rushwa, kutoa adhabu kwa wanaoenda kinyume na misingi ya uadilifu walijiwekea.

Amesema kwa kufanya hivyo watakuwa wamejiongezea nguvu yao kama taasisi lakini pia kupeleka ujumbe kwa wanachama wao kuwa wanathamini haki na kuchukia rushwa.

Waziri Mkuu ameongeza kuwa shughuli za sekta binafsi zimeendelea kuongoza katika kuchangia pato la Taifa na ukuaji wa uchumi kwa ujumla. 

Amesema kwa mujibu wa takwimu sekta ya utalii inachangia asilimia tisa, huduma asilimia 35, kilimo asilimia 26.6, madini asilimia 3.3 na sekta ya viwanda inachangia takribani asilimia 10.

“Jukumu letu sote ni kuchochea uzalishaji na kufanya wepesi  kwa wajasiriamali wetu watoke nje ya mipaka yetu na kwenda kuuza bidhaa zetu nchi jirani. TPSF mtusaidie katika hili.”

Waziri Mkuu amesema Serikali kwa upande wake itaendelea kuweka mazingira wezeshi kwa kuboresha miundombinu, kutoa vivutio kwenye kodi, kanuni na sheria ili kukuza sekta binafsi.

Hivyo, Waziri Mkuu amesema sekta binafsi nchini nayo haina budi kutumia vema fursa hiyo ya uwepo wa mazingira wezeshi na rafiki kwa kuwekeza kwenye uchumi wa nchi.

Amesema ni vema wakatambua kwamba wana jukumu kuliletea Taifa maendeleo, hivyo wafanye kazi kwa ukaribu na ubia baina yao ili kuhakikisha nchi inanufaika na fursa zilizopo.

Pia amewasihi waendelee kuwekeza zaidi kwenye uzalishaji wa bidhaa za viwandani na wahakikishe kuwa wanajali maisha ya Watanzania ambao ndio soko na wateja wa bidhaa zao.

(mwisho)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMANNE, AGOSTI 28, 2018.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.