Habari za Punde

Eden Hazard achanganyikiwa kati ya Chelsea na kuhamia Real Madrid

Nyota wa Chelsea Eden Hazard amesema kwa sasa hajui kama aamue kusalia Stamford Bridge au ahamie klabu ya Real Madrid ya Uhispania.
Mshambuliaji huyo wa Ubelgiji amesalia na miaka miwili kwenye mkataba wake Chelsea, lakini amekuwa kwa muda sasa anahusishwa na kuhamia kwa mabingwa hao wa Ulaya.
Hazard amefunga mabao saba katika Ligi ya Premia kufikia sasa."Sitaki kusema, 'ndio, natia saini mkataba mpya', na kisha mwishowe nisitie wino kwenye mkataba," mchezaji huyo wa miaka 27 aliambia wanahabari.
"Ninataka kufanya lililo jema kwangu, lakini nataka pia kufanya lililo bora kwa klabu hii kwa sababu imenipa karibu kila kitu.
"Kwa hivyo, tusubiri tuone mambo yatakuwaje. Wakati mwingine kichwani, huwa naamka asubuhi na kufikiria ninataka kuondoka. Wakati mwingine nafikiria kwamba ninataka kusalia hapa."Ni uamuzi mgumu kuufanya. Unahusu maisha yangu ya baadaye."
Hazard aliwafungia Chelsea bao la kwanza walipowalaza Southampton 3-0 Jumapili na kuendeleza mwanzo wao mwema wa msimu, ambapo kufikia sasa bado hawajashindwa na klabu yoyote.
Fowadi huyo wa Chelsea anaamini kwamba anahitaji kuhamia klabu nyingine na kulipiwa pesa nyingi kabla yake kustaafu.Ameieleza klabu ya Real Madrid kama klabu bora zaidi duniani.
"Hiyo ndiyo maana nilizungumza baada ya Kombe la Dunia na kusema kwamba nafikiri kwamba wakati umefika kwangu kufanya mabadiliko kwa sababu nilicheza vyema kwenye Kombe la Dunia," aliongeza Hazard, ambaye Julai alikuwa amesema kwamba huenda muda umefika kwake kujaribu mambo mapya baada ya kukaa miaka sita Stamford Bridge.
"Ninacheza vyema sana kwa sasa."Real Madrid ndiyo klabu bora zaidi duniani. Sitaki kusema uongo leo. Ilikuwa ni ndoto yangu (kujiunga nao) tangu nikiwa mtoto. Nilikuwa naota kuhusu klabu hii.
"Tutaona mambo yatakwendaje. Sitaki kuzungumza kuhusu hili kila siku, sina muda. Lakini tutazungumzia mustakabali wangu hivi karibuni."

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.