Habari za Punde

TANZANIA YAONGOZA DUNIANI KWA KUWA NA UTAJILI WA URITHI WA ASILI BAADA YA BRAZIL

 Wasanii wa kundi la Wanne Star wakicheza ngoma za utamaduni jukwaani wakati wa ufunguzi wa tamasha hilo leo Oktoba mosi, Jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha la Urithi Kitaifa, Profesa Audax Mabula akizungumza katika ufunguzi huo ambapo amesema Tanzania inajivunia kuwa na Lugha kuu nne zilizopo Barani Afrika. Wakati wa ufunguzi huo leo Oktoba Mosi katika Kijiji cha Makumbusho Jijini Dar es Salaam. 

Tanzania ni ya pili kwa Urithi wa Maliasili baada ya Taifa la Brazil la Bara la Amerika ya Kusini kwa kuwa na vivutio vingi vya Asili.
Hayo yameelezwa leo wakati wa ufunguzi rasmi wa Tamasha la Urithi Wetu (Urithi Festival)  linalofanyika katika viunga vya Kijiji cha Makumbusho Jijini  Dar-es –Salaam na Mgeni rasmi Mwenyekiti wa Shirikisho la vyama vya Wadau wa Utalii Tanzania,  Bwana  Abdukadir Luta Mohamed.
Amesema kuna vivutio vingi vya  urithi wa utamaduni, ukiweka pamoja vivutio vya utalii wa asili na utamaduni, Tanzania inaweza kuongoza kwa kuwa na vivutio vingi vya utalii  duniani.
Bwana Mohamed  amevitaja baadhi ya vivutio hivyo  kuwa pamoja na tamaduni, makabila, mila, desturi, vyakula na Malikale.
Awali akizungumza wakati wa kumkaribisha mgeni rasmi, Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha la Urithi Kitaifa, Profesa Audax Mabula ameeleza kuwa Tanzania inajivunia kuwa na lugha kuu nne zilizopo Barani Afrika.
Amezitaja lugha hizo kuwa ni Wabantu ambao inawajumuisha makabila kama vile Wasukuma, Wajita na Wanyamwezi, Wanailotiki inawajumuisha Wamaasai, Wakushitiki-inayojumuisha  Wairaq,Wambulu, Wakhoisan –inayowajumuisha Wahadzabe na Wasandawe.
Profesa Mabula ameeleza kuwa, Kabila la Wasandawe limeanza kupotea lakini ni imani kuwa kabila hilo litaendelezwa kupitia tamasha la Urithi Wetu.
Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha la Urithi Kitaifa amesema "Utalii wa Utamaduni utainuliwa kupitia Urithi festival.
Amewaomba Watanzania kushiriki vema kwenye Tamasha hili na kuvaa mavazi ya Kitanzania kama vitenge, ngozi, batiki, shuka na mavazi mengine ya asili katika maadhimisho haya na ya kila  Mwezi wa tamasha la Urithi.
"Urithi festival inatoa fursa kwa watu wote. Tunapenda waje hapa waone ubunifu, vitu muhimu na mambo ya ubunifu wa kila aina” Amesema Profesa Mabula.
Ameongeza kuwa, Watu tuheshimu Urithi wetu wa Utamaduni ili kuchochea Utalii wa ndani na nje ya Nchi.
Tamasha hilo limepambwa na  vikundi mbalimbali vya ngoma za kiasili, sarakasi, nyimbo, Wajasiriamali, vyakula vya kiasili ikiwemo nyama choma za porini  kama swala na nyati zilnazouzwa kwa shilingi elfu Nane kwa kilo.
Naye Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Bw. Richard Mayongela  katika kuunga mkono Tamasha la Urithi Wetu, imekabidhi fulana 100 katika hafla hiyo.
Tamasha hilo ambalo litakuwa likifanyika kila mwaka, linaandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii, na lilizinduliwa rasmi Septemba 15 mwaka huu jijini Dodoma na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan likiwa na lengo la kuongeza idadi ya watalii nchini.
Imeelezwa kuwa, baada ya Tamasha hilo kufungwa rasmi jijini Dar-es-Salaam litaendelea kufanyika Jijini Arusha kwenye Uwanja wa Sheikh  Amri  Abeida Karatu, ambako ni njia kuu ya kuingilia katika Hifadhi ya Bonde la Ngorongoro na Serengeti kuanzia Oktoba 8  hadi  13.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.