Habari za Punde

UBUNGO NA KIGAMBONI KUNUFAIKA NA MRADI MKUBWA WA KUTEKETEZA TAKA


Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Balozi Joseph Sokoine akizungumza wakati wa uzinduzi wa mradi wa uteketezaji wa taka kwa njia salama bila kuathiri mazingira. Warsha hiyo ya siku moja imefanyika katika ukumbi wa NIMR jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mwakilishi wa Shirikika la Umoja wa Mataifa linalohusika na uendelezaji wa Viwanda (UNIDO) Dkt. Stephen Kagbo.


Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mazingira Bi. Magdalena Mtenga akifafanua jambo mbele ya waandishi wa habari mara baada ya uzinduzi wa warsha ya mradi wa uteketezaji wa taka kwa njia salama bila kuathiri mazingira. Mradi huo kwa nchi ya Tanzania utatekelezwa katika Wilaya za Kigamboni na Ubungo.


Wataalamu kutoka Taasisi za Serikali, Sekta binafsi na Asasi zinazojishughulisha na masuala ya Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira wakiwa katika picha ya pamoja na mgeni rasmi Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Balozi Joseph Sokoine (wa nne kutoka kulia) mara baada ya uzinduzi wa warsha ya uteketezaji wa taka kwa njia salama bila kuathiri mazingira, jijini Dar es Salaam.


Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana na UNIDO hii leo wamezindua warsha ya Mradi wa kudhibiti kemikali zitokanazo na uchomaji wa taka katika maeneo ya wazi. Akizindua warsha hiyo iliyofanyika katika Ukumbi wa NIMR jijini Dar es Salaam, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Balozi Joseph Sokoine amesema kuwa mradi huo unatarajia kuja na mapendekezo ya namna ya kupunguza athari za uchomaji taka katika mazingira.

Balozi Sokoine amesema kuwa lengo kubwa la warsha hiyo ya wataalamu ni kujadili mbinu bora za uchomaji taka bila kuathiri mazingira.

“Tunategemea mradi huu utatusaidia sana sisi watu wa mazingira katika kudhibiti uchomaji hovyo wa taka, uchomaji unaofanyika maeneo ya wazi unazalisha kemikali ambazo zinadumu kwa muda mrefu katika mazingira.” Alisisitiza Balozi Sokoine.

Naye Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mazingira Bi. Magdalena Mtenga amesema kuwa jamii inapaswa kufahamu kuwa taka ni mali na ni vema zikabadilishwa kuwa fursa, ikiwa ni njia bora ya kusukuma mbele agenda ya uchumi wa viwanda.

“Uchomaji wa taka unasababisha uzalishaji wa kemikali hatarishi kwa mazingira ambazo hudumu kwa muda mrefu na sisi lengo letu ni kudhibiti hii hali ndio maana tumekuja na huu mradi ili  taka zirejerezwe na kutumika kwa matumizi mengine” Mtenga alisisitiza.

Kwa upande mwingine Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na uendelezaji wa viwanda (UNIDO)  Dkt. Stephen Kagbo amesema uchafuzi wa mazingira ni suala linalozikabili nchini nyingi barani Afrika hivyo ujio wa mradi huu utatoa fursa ya kuja na teknolojia ya kisasa ya kuteketeza taka kwa namna bora bila kuathiri mazingira.

Utekelezaji wa Mradi huo utaanza katika Wilaya za Ubungo na Kigamboni na nchini nyingine zinazonufaika na mradi kama huu ni pamoja na Botswana, Lesotho, Madagascar, Mozambique, Swaziland na Zambia.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.