Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein(kushoto) alipokuwa akitoa hutuba yake katika sherehe za uzinduzi wa maonesho ya Siku ya Chakula Duniani yaliyofanyika leo katika kijiji cha Chamanangwe Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba,[Picha na Ikulu .]11 Oct 2018.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa upo umuhimu mkubwa kwa jamii kuwa
na uhakika wa chakula na lishe bora kwa sababu hio ndio nguzo imara ya kuulinda
uhuru na kuondoa utegemezi.
Dk. Shein aliyasema hayo
leo katika sherehe za ufunguzi wa maonesho ya Siku ya Chakula Duniani, ambapo
kwa Zanzibar zimefanyika Chamanangwe, Wilaya ya Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba hafla
iliyohudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa
Zanzibar Balozi Seif Ali Idd pamoja na wananchi.
Katika maelezo yake Rais
Dk. Shein alisema kuwa uhakika wa chakula na lishe bora ni muhimu katika
kuimarisha afya za wananchi na kuchangia katika kuondoa umasikini.
Aliongeza kuwa sababu hiyo
ndiyo iliyopelekea maonesho hayo yakapewa uzito mkubwa katika mipango muhimu ya
Serikali ukiwemo MKUZA Awamu ya 3, Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020,
Sera na mikakati ya kiserikali ikiwemo mkakati wa Mapinduzi ya Kilimo.
Alisema kuwa mikakati ya
jumla inayotolewa na mipango iliyopo inalenga katika kuongeza uzalishaji,
ujenzi na upatikanaji wa miundombinu, utiaji wa thamani na uhifadhi wa chakula
kwa lengo la kuongeza tija, kipato na kuondoa umasikini hapa Zanzibar.
Rais Dk. Shein alisema
kuwa katika awamu mbali mbali za uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
Serikali imebuni na kuitekeleza mikakati na program mbali mbali ili uzalishaji
wa mazao mbali mbali yakiwemo ya chakula na biashara unaongezeka na kupata tija
zaidi.
Alieleza kuwa katika
Awamu ya Saba ya Uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar jitihada maalum
zimefanywa kwa lengo la kuongeza mavuno ya mpunga kwa upande wa mazao ya
chakula na zao la karafuu kwa mazao ya biashara.
Alisisitiza kuwa lengo
la Serikali ni kupunguza kiwango cha uagiziaji mchele nje ya nchi na
kujitosheleza kwa mchele angalu kutoka asilimia 39.9 ya sasa hadi asilimia 60
ifikapo mwaka 2020 jambo ambalo linawezekana ambapo tayari jitihada za wakulima
na serikali zimeanza kuonekana.
Dk. Shein alisema kuwa
katika kufikia dhamira ya kuwa na uhakika wa chakula na lishe bora Serikali
inatambua na kuendelea kuzifanyia kazi changamoto zinazowakabili wakulima na
sekta yote ya kilimo.
Alitumia fursa hiyo
kutoa wito na indhari wka wale wote wanaojenga majengo ya makaazi katika
mabonde ya mpunga kuonoka wenyewe huku akiwataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya kuanza kulichukulia hatua suala hilo.
Aliongeza kuwa katika
kuzitatua changamoto hizo Serikali imetenga jumla ya TZS bilioni 63 kwa ajili
ya maendeleo ya sekta ya kilimo nchini ikiwemo uzalishaji wa mazao, mifugo,
mazao ya biashara, uimarishaji wa huduma
na miundombinu, usarifu pamoja na utekelezaji wa miradi mengine ya maendeleo.
Rais Dk. Shein
aliwahakikishia wakulima na wananchi kuwa Serikali itaendelea kuitekeleza
dhamira yake ya kutoa ruzuku kwa wakulima wa mpunga ili kuhakikisha kuwa
malengo ya kuongeza mavuno yanazidi kupata mafanikio.
Kwa maelezo ya Rais Dk.
Shein Serikali inaendelea na jitihada za kupunguza utegemezi wa mvua katika
kilimo cha mpunga kwa kuimarisha miundombinu ya umwagiliaji maji ambapo katika
mradi wa kuongeza uzalishaji wa mpunga (ERPP), Serikali itajenga miundombinu hekta
193 Unguja na Pemba kwa ajili ya uzalishaji wa mbegu za mpunga.
Alieleza kuwa hivi sasa
tayari hatua za ujenzi na upelekaji wa umeme zinaendelea katika mabonde ya
Dodeani, Machigini, Dobi, Kwalempona kwa upande wa Pemba na katika mabonde ya
Mtwango, Koani, Bandamaji, Mchangani na Kibondemzungu kwa upande wa Unguja.
Kadhalika alisema kuwa
Serikali imechukua mkopo wa Dola za Kimarekani milioni 50 kutoka Banki ya Exim
ya Korea kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji maji wa hekta 1,524
sawa na ekari 3,810 katika mabonde ya mpunga ya Cheju, Kilombero na Bumbwisudi
kwa Unguja na Makwararani na Mlemele kwa upande wa Pemba.
Katika kuhakikisha
Zanzibar inahifadhi ya mazao na kujikinga na balaa la njaa, Dk. Shein alisema
kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeandaa mpango madhubuti wa kuanzisha
ghala la chakula cha akiba ambapo tayari ghala moja limeshatayarishwa.
Alisema kuwa ghala hilo
limefanyiwa matengenezo makubwa yaliyogharimu TZS 254,767,000 ghala ambalo lipo
Malindi mjini Unguja na lenye uwezo wa kuhifadhi tani 6000 za mchele kwa wakati
mmoja na linatarajiwa kufunguliwa hivi karibuni na katika mwaka wa fedha 2019/2020
Serikali imedhamiria kulifanyia matengenezo makubwa ghala la Tibirinzi huko
Pemba.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein alieleza kuwa Serikali inaendelea na jitihada za kuimarisha sekta ya
ufugaji na uvuvi ili nazo ziwe kuchangia katika kuyafikia malengo ya kuwa na
uhakika wa chakula na lishe bora.
Alisema kuwa kwa lengo
la kuzidi kuimarisha sekta ya uvuvi, Serikali imeanzisha Kampuni ya uvuvi na
hivi sasa inatengeneza meli mbili za uvuvi nchini Maldives na Sri Lanka zenye
uwezo wa kuvua tani 90 za samaki kwa wiki kwenye bahari kuu.
Aliwanasihi vijana
wazitumie fursa za ajira zilizopo katika sekta ya kilimo,ufugaji na uvuvi katika
kukabiliana na changamoto za uhaba wa ajira Serikalini na Serikali iko tayari
kuwawezesha. Alisema kuwa tayari kuna mwekezaji kutoka nchini China ambaye
analengo la kuja kisiwani Pemba kuekeza kiwanda cha samaki.
Dk. Shein alieleza kuwa
Serikali imeanzisha Taasisi ya Utafiti
wa Kilimo, Wakala wa matrekta na zana za kilimo na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo
kwa lengo la kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazoikabili sekta za kilimo kwa
ujumla wake na kubuni njia bora za kuongeza uzalishaji kulingana na mazingira
yaliopo.
Alisisitiza kuwa Wizara
ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi lazima ihakikishe inaziwezesha Taasisi za
utafiti kwa kila hali na kuzisimamia vizuri ili zitoe matunda ya kazi zao kwa
lengo la kuongeza tija katika sekta ya kilimo na ufugaji.
Alisema kuwa Serikali
itaendelea kupambana na misumeno ya moto na inayopatiakana hivi sasa itaendelea
kuchomwa moto huku kukiandaliwa taratiu za kuwepo sheria za kuwashtaki
wanaokutwa na misumenohiyo, ambapo pia aligusia umuhimu wa uhifadhi wa mazingira.
Dk. Shein alitembelea mabanda mbali mbali ya maonesho.
Nae Waziri wa Kilimo,
Maliasili na Uvuvi Rashid Ali Juma alieleza kuwa uongozi wa Wizara unatoa
pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa uwamuzi wake wa kuagiza sherehe hizo kwa mwaka
huu zifanyika kisiwani Pemba na kueleza maamuzi hayo ni ya busara katika
kuimarisha kilimo.
Alieleza kuwa kauli mbiu ya mwaka huu ni “Juhudi zetu ndio
hatma yetu” Dunia bila ya njaa inawezekana ifikapo 2030” na kusisitiza kuwa kwa
juhudi za makusudi hilo linawezekana huku akisema kuwa misumeno ya moto 295
imekamatwa na inaendelea kuteketezwa.
Mapema Katibu Mkuu wa
Wizara ya Kilimo, Maliasili na Uvuvi Maryam Juma Saadallah alieleza kuwa eneo
hilo lililofanyiwa maonesho lina ukubwa wa ekari 85 ambapo Wizara imetenga
ekari 17 kwa ajili hiyo ambapo katika kufanikisha shughuli hiyo jumla ya
milioni 116 zimetumika.
Alisema kuwa siku ya
chakula duniani kwa mwaka 2018 yatafikia kilele chake tarehe 16 Oktoba 2018
ambapo lengo ni kuwaweka pamoja wadau wa sekta za kilimo wakiwemo wataalamu,
wakulima, wafugaji, wavuvi, wajasiriamali na wafanyabiashara.
Nae Mwakilishi kutoka
Shirika la Umoja wa Mataifa la FAO na IFAD Tanzania Dk. Mwatima Abdalla Juma
alisema kuwa Mashirika ya Umoja wa Mataifa yanayojishughulisha na kilimo na
ufugaji yataendelea kuiunga mkono Zanzibar.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment