Habari za Punde

Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Atembelea Kiwanda cha TANICA na BUKOP Mjini Bukoba.

Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Kassim Majaliwa akisalimiana na wafanyakazi wa kiwanda cha  kahawa cha TANICA mjini Bukoba baada ya kutembelea kiwanda hicho, 
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akipata maelezo kutoka kwa Mhandisi Mkuu wa kiwanda cha kukoboa kahawa cha BUKOP, Theobad Mushashu  kuhusu ukoboaji kahawa wakati alipotembelea kiwanda hicho, Oktoba 6, 2018. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu Mhe.Kassim Majaliwa amesema changamoto ya upatikanaji wa ajira hususani kwa vijana imeanza kupungua nchini baada ya viwanda vingi kuanza kufanya kazi.

Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli imedhamiria kukuza uchumi kutoka wa chini hadi wa kati kupitia sekta ya viwanda ifikapo mwaka 2025.

Aliyasema hayo jana jioni (Jumamosi, Oktoba 6, 2018) alipotembelea kiwanda cha kukoboa kahawa cha BUKOP na cha kusindika kahawa cha Tanica, mjini Bukoba.

Alisema kwa sasa tabia ya vijana wengi kukaa vijiweni imepungua kwenye maeneo mengi nchini baada ya wengi kuajiriwa katika viwanda mbalimbali vilivyoanzishwa na kufufuliwa.

Waziri Mkuu alisema viwanda vimekuwa vikitoa ajira nyingi kwa wananchi, ambapo alitolea mfano kiwanda kimoja cha Tanika kilichoajiri watumishi 800. 

“Nyie mlioajiriwa kiwandani hapa hakikishe mnafanya kazi kwa bidii, weledi, uaminifu na uadilifu wa hali ya juu ili kukiwezesha kiwanda kuendelea na uzalishaji,” alisisitiza.

Waziri Mkuu ambaye yuko mkoani Kagera kwa ziara ya siku nne, inayolenga kufuatilia maendeleo ya viwanda na zao la kahawa, ambalo ni kati ya mazao makuu sita ya biashara.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alimuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba  Bw. Bernad Limbe kuhakikisha anatafuta eneo kwa ajili ya wafanyabiashara ndogondogo.

Aliyasema hayo baada ya kupata malalamiko kutoka kwa wananchi waliokuwa wakifanya biashara katika eneo bandari na kuondolewa bila ya kupewa eneo lingine.

Waziri Mkuu alisema ni marufuku kuwaondoa wananchi katika maeneo yao ya kufanyia biashara bila ya kuwaonesha eneo lingine  ambalo watalitumia kwa aliji ya kufanyia biashara zao. 

Awali, Meneja Mkuu wa kiwanda hicho, Bw. Linus Leopord alisema kwa mwaka wanazalisha tani 600 za kahawa iliyokaangwa na kusagwa, ambayo inatosheleza kwa mahitaji ya soko.

Pia kiwanda cha kahawa cha Tanica kinauwezo wa kuzalisha kahawa ya unga tani 500 kwa mwaka ila kutokana na uchakavu wa miungombinu kinazalisha tani 300 kwa mwaka.

Kuhusu masoko Bw. Leopord alisema kwa sasa mauzo yameongezeka, wanauza tani 50 ya kahawa iliyokaangwa na kusagwa kwa mwezi, ambapo awali walikuwa wanauza tani 32.

Kadhalika, Meneja huyo alisema wameimarisha na kuongeza soko la nje ambapo kwa sasa wanauza tani 35 za kahawa ya unga kwa mwezi, awali walikuwa wanauza tani 20.

Alisema kiwanda cha Tanika kinamilikiwa na chama cha ushirika cha KCU (53.37 %), KDCU (31.8%), Hazina (7.67), TFC (6.22%) na wafanyakazi wa Tanica (0.92%).

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAPILI, OKTOBA 7, 2018.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.