Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk.Ali Mohamed Shein, akitembelea Uwanja wa Mao Zedong's Zanzibar, wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Uwanja wa Mao Zedong's uliofanyika leo, akipata maelezo kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Vijana, Michezo Utamaduni na Sanaa Zanzibar.Ndg. Omar Hasan King, wakati akitembelea Uwanja huo kulia Waziri wa Vijana Michezo,Utamaduni na Sanaa.Mhe.Balozi Ali Abeid Karume, Balozi Mdogo wa China, Xie Xiaowu, na kushoto Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, wakati wakitembelea Uwanja huo baada ya Ufunguzi wake uliofanyika leo.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amekemea tabia iliojengeka nchini ya wanamichezo ku[peleka kesi
za michezo mahakamani, na kusema hatua hiyo imekuwa ikidumaza maendeleo ya
michezo nchini.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo katika hafla ya uzinduzi wa Uwanja wa Mao Tse Tung uliopo Kikwajuni
Mkoa wa Mjini Magharibi ambao umejengwa kwa msaada wa Serikali ya Jamhuri ya
Watu wa China kwa mashirikiano ya pamoja na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Amesema michezo ni jambo la ridhaa na maelewano, hivyo
matatizo yote yanayojitokeza, ni lazima yashughulikiwe na kumalizwa kwa busara.
Alitoa indhari kwa
kubainisha kuwa kuanzia sasa hatokuwa tayari kusadia shughuli za kimichezo,
ikiwemo soka endapo tabia ya kupeleka
kesi hizo mahakamani itaendelea.
“Acheni tabia hiyo
mnaitia aibu nchi yetu, nataka nikwambieni kuwa FIFA inatuonea imani tu juu ya
jambo hilo, ni matumaini yangu kuwa kesi za michezo hazitafikishwa tena
mahakamani” alisema.
Aidha, Dk. Shein
alisema Serikali inakusudia kuongeza bajeti ya Wizara ya Vijana,Utamaduni,
Sanaa na Michezo kuanzia mwaka ujao wa
fedha, ili kuimarisha na kuendeleeza michezo mbali mbali nchini.
Alisema hatua hiyo
itakwenda sambamba na uimarishaji wa timu ya Taifa ya mpira wa miguu, ili
kuleta ushindani na kuwa miongoni mwa timu bora katika ukanda wa Afrika
Mashariki.
Dk. Shein alieleza
kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha inafanikisha azma yake ya kujenga
Uwanja mkubwa wa kisasa utakaochukua watu 45,000 kutoka maeneo yaliyotengwa huko
Fumba pamoja na Tunguu.
Katika hatua nyengine Dk. Shein aliigiza Wizara ya
Vijana,Utamaduni,Sanaa na michezo kuandaa programu nzuri itakayowezesha
matumizi bora ya kiwanja hicho, ili uweze kudumu.
Alisema ni vyema
kukawepo utaratibu wa kuweka viingilio
katika baadhi ya mashindano ili kuweza kupata fedha zitakazowezesha kukifanyia
matengenzo madogo madogo kiwanja hicho pale panapohitajika.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein alieleza kuwa ujenzi wa uwanja huo ni utekelezaji wa Ilani ya
Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020.
Nae Waziri wa Wizara
ya Vijana, Sanaa, Utamaduni na Michezo Balozi Ali Abeid Karume alitoa shukurani
na pongezi kubwa kwa Rais Dk. Shein kwa jitihada zake za kuhakikisha uwanja huo
unajengwa upya na una kuwa wa kisasa.
Balozi Karume alimponmgeza Dk. Shein kwa kuweka
kipaumbele suala la kuimarisha michezo, hivyo, akaahidi Wizara yake
kuwaendeleza vijana pamoja na kukitunza ipasavyo kiwanja hicho.
Aidha, Balozi Karume
alitumia fursa hiyo kueleza mafanikio na matunda ya Mapinduzi matukufu ya
Januari 12, 1964.
Nae Balozi Mdogo wa China anaefanya kazi zake hapa
Zanzibar Xie Xiuowu alisema ujio wa mradi huo utaendeleza uhusiano na
ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya China na Zanzibar.
Aidha, alisema kukamilika kwa kiwanja hicho pamoja
na ujenzi wa viwanja mbali mbali vya michezo ya ndani (indoor games)
kutaimarisha viwango vya wanamichezo wa Zanzibar na hivyo kufanya vyema katika
mashindano mbali mbali ya .
Mapema Katibu Mkuu
Wizara ya Vijana, Sanaa, Utamaduni na Michezo Omar Hassan (King) alieleza kuwa
jumla ya gharama zote za mradi zilikuwa ni TZS Bilioni 15 ambapo Serikali ya
Jamhuri ya Watu wa China walitoa msaada wa TZS Bilioni 11.
Alisema kuwa mradi huo
ulikuwa na maeneo ambayo yaligharamiwa na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China
na maeneo mengine yaligharamiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambapo
mpaka sasa fedha zote zimelipwa na hakuna deni lolote linalodaiwa.
Aliongeza kuwa mradi huo
ulianza rasmi tarehe 3 Machi 2017 na ulitakiwa ukamilike mwishoni wa mwezi wa
Mei, 2018 kwa kazi zile zilizomo kwenye makubaliano na Serikali ya Jamhuri ya
Watu wa China.
Alieleza kuwa hata
hivyo, baada ya kuangalia kwa makini ikaonekana kwamba kuna haja kubwa ya
kumalizia maeneo yote ya uwanja ili uwanja upendeze zaidi hasa maeneo ya ukuta
pembezoni mwa uwanja kwa kujaza zege nyengine.
Katibu Mkuu huyo
alieleza kuwa kupitia mahitaji hayo, ndipo kukapelekea kuchelewa kwa ujenzi huo
kwa muda wa miezi mitatu na hadi ilipofika mwezi Agosti, 2018 ambapo kwa msaada
wa Serikali ya China zilikuwa zimekamilika na kufikia Novemba 2018 kazi zote za
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar nazo zilikamilika.
Alieleza kuwa kwa
mujibu wa makubaliano yaliyomo katika mkataba huo wa ujenzi wa “Zehngtai Group
Company” baadhi yao watabaki hapa Zanzibar kwa muda wa miaka miwili ili
kuangalia kama kutakuwa na matatizo yoyote makubwa ili yafanyiwe marekebisho.
Katibu Mkuu huyo aliyataja
maeneo ambayo yametekelezwa kupitia fedha za msaaada kutoka Serikali ya Jamhuri
ya Watu wa China ambayo ni uwanja wenyewe ambao una viwanja viwili vya mchezo
wa mpira wa miguu ambayo vina vipimo vya Kimataifa na vimewekewa nyasi bandia.
Mengine ni majukwaa
mawili makubwa na mawili madogo yenye uwezo wa kuchukua watazamaji 2,100,
uwanja wa kucheza aina nne za michezo ikiwemo “Bastektball” na “Volleyball”
ambapo pia, kuna sehemu ya michezo ya ndani (Indoor) ikiwemo kucheza “Table
Tennis” ambayo ina jumla ya meza sita.
Mambo mengine
yaliyotekelezwa ni kuwepo kwa sehemu ya mazoezi ya viungo ya kuinua vitu vizito
(Gym nastic), jengo la vyoo 48 kwa ajili ya huduma za jamii, majengo mawili kwa
ajili ya Ofisi na ujenzi wa ukuta kwenye eneo la Mashariki.
Akiyataja mambo ambayo
yametekelezwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Katibu Mkuu huyo aliyataja
kuwa ni pamoja na kusafisha eneo lote la uwanja wa Mao kwa kubomoa majengo ya
zamani, kuwapatia eneo wakandarasi kwa ajili ya kuweka makaazi yao, kuhakikisha
huduma zote muhimu zinapatikana zikiwemo maji na umeme.
Mambo mengine ni
kugharamia huduma za ulinzi kwa muda wote katika eneo la kiwanja, kulipa
gharama zote za utoaji wa vifaa bandarini na wuanja wa ndege, kujenga ukuta
wenye urefu wa mita 220 upande wa Magharibi, kujenga kwa kujaza zege eneo lote
la pembezoni mwa uwanja pamoja na kuweka mfumo wa kutoa maji kwenye uwanja kwa
kuchimba chini mashimo 36 ambayo hupeleka maji kwenda chini.
Viongozi mbali mbali
wa vyama vya siasa na Serikali pamoja na mamia ya wananchi walihudhuria katika
sherehe hiyo ya uzinduzi wa uwanja huo ikiwa ni miongoni mwa shamrashamra za
kuadhimisha miaka 55 ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment