RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameungana pamoja na Wapiganaji wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama waliovyoshiriki katika Maadhimisho ya sherehe za kutimiza miaka 55 ya Mapinduzi ya Zanzibar katika chakula maalum cha mchana alichowaandalia.
Chakula hicho maalum
cha mchana aliwaandalia kutokana na ushiriki wao kwenye sherehe hizo za miaka
55 ya Mapinduzi zilizofanyika Januari 12 mwaka huu 2019 huko katika uwanja wa
Gombani Chake Chake Pemba.
Hafla hiyo ya chakula
maalum ilifanyika leo katika Kambi ya Mafunzo
ya Jeshi ya Chukwani ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar wakiwemo Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali
Maulid, Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu, Mawaziri, Manaibu Mawaziri na
viongozi wengine pamoja na Wapiganaji wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama vya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
Katika shukurani zake
Dk. Shein kwa Wapiganaji hao zilizotolewa kwa niaba yake na Waziri wa Nchi
Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Haji Ussi Gavu alitoa
pongezi kwa Wapiganaji hao kwa kushiriki kikamilifu katika sherehe hizo adhimu.
Alieleza kuwa hatua
hiyo ya Dk. Shein ya kuwaandalia chakula maalum cha mchana ni utamaduni
aliouweka kila mwaka baada ya kumaliza sherehe hizo ambayo inaonesha wazi jinsi
alivyokuwa na upendo pamoja na imani kubwa na wananchi wote anaowaongoza.
Hivyo, Waziri Gavu alisisitiza haja kwa Vikosi hivyo
vya Ulinzi na Usalama kuendelea kutimiza wajibu wao wa kulinda amani, utulivu
na mshikamano ambapo pia, alitumia fursa hiyo kutoa pongezi maalum kwa ushiriki
wao mzuri katika sherehe hizo.
Waziri Gavu alitoa
shukurani za dhati kwa vikosi hivyo kwa kuazimisha kwa hali ya juu kilele cha
miaka 55 ya Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.
Waziri Gavu alisema
kuwa gwaride hilo lililovutia sana lilikuwa ni kielelezo cha kutosha cha
Mapinduzi ya Januari 12.1964 yaliyowakomboa Wazanzibari wote ambayo yataendelea
kulindwa, kuenziwa na kutunzwa daima.
“ Imani ya kiongozi
mwema siku zote haitafutwi kwenye jarida bali inatafutwa katika nafsi na nyonyo
za watu anaowaongoza........na sote tunaona jinsi ya upendo ulionao kwa
wananchi wa Zanzibar na Tanznia nzima kwa jumla”.
“ .....hongereni sana
sana sana Vikosi vyetu vya Ulinzi na Usalama kwa kazi kubwa mliyoifanya katika
kilele cha miaka 55 ya Mapinduzi yetu ”,alisisitiza Waziri Gavu.
Aidha, alitoa
shukurani kwa Wapiganaji wote pamoja na viongozi wao kwa kufanikisha kilele cha
sherehe hizo na kusisitiza haja kwa vikosi hivyo kuendelea kusimamia amani,
utulivu na mshikamano hatua ambayo itawapelekea viongozi wengine kutekeleza
majukumu yao ya kuwaletea maendeleo wananchi kwa ufanisi mkubwa.
Nae Kaimu Brigedi
Kamanda 101 KV Zanzibar Kanal Salum Serengo Mugoba alitoa shukurani na pongezi
kwa Dk. Shein kwa kuendelea kuvijali vikosi vya Ulinzi na Usalama pamoja na
kuendeleza utamaduni wake huo aliouweka kwa kila mwaka mara baada ya sherehe za
Mapinduzi ambapo Dk. Shein huwandalia chakula maalum cha mchana Wapiganaji hao na
kula nao pamoja.
Kanal Mugoba alieleza
kufarajika kwao na hatua hiyo ya Dk. Shein na kutoa pongezi na shukurani kwa
niaba ya Wapiganaji wote walioshiri katika hafla hiyo adhimu.
Ni utamaduni aliouweka
Dk. Shein wa kuwaandalia chakula cha mchana Vikosi vya Ulinzi vinavyoshiriki
katika gwaride la sherehe za Mapinduzi pamoja na vijana na Wanafunzi ambao
hushiriki sherehe hizo kwa kila mwaka ambapo hapo jana aliwaandalia vijana na
Wanafunzi chakula hicho huko katika Makao
Makuu ya KVZ, Mtoni mjini Zanzibar.
Katika hafla hiyo pia,
Kikundi cha Taarab cha Taifa kilitumbuiza pamoja na Grassbanda ya JWTZ.
Rajab
Mkasaba, Ikulu
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment