Habari za Punde

Tutailinda Amani iliyopo Nchini-Waziri Masauni

Na Mwandishi Wetu
Serikali imesema haitakua tayari kuona Amani na Utulivu wa Nchi inachezewa  huku ikisisitiza uwepo wa Umoja kati ya wananchi bila kujali tofauti ya imani, kabila au itikadi yoyote.
Hayo yamesemwa  na  Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mhandisi Hamad Masauni wakati akifungua Semina ya siku mbili iliyofanyika jijini Dar es Salaam ikiwahusisha  Viongozi wa Taasisi za Kiislamu lengo ikiwa ni kuwakumbusha kuhubiri amani katika sehemu zao
Amesema muelekeo na malengo ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kukuza maendeleo katika sehemu mbalimbali nchini lengo ikiwa kuinua maisha ya wananchi nan chi kwa ujumla
“Serikali hii imejidhatiti kuhakikisha maendeleo yanakuja kwa kasi na maendeleo hayawezi kuja ikiwa amani na utulivu haupo, sisi kama serikali tutahakikisha tunalinda amani iliyopo ili wananchi wapate kufanya shughuli za kiuchumi bila wasiwasi wowote” alisema Masauni
Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Sheikh wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhaji Mussa Salum aliihakikishia serikali kutokuwepo kwa mifarakano kati ya taasisi mbalimbali kama ilivyokuwepo awali huku akisisitiza kuendelea kwa umoja huo ili jamii ipate kuendelea
“Sisi kama Bakwata tunaihakikishia serikali uwepo wa umoja na ushirikiano baina ya baraza na taasisi zingine na tofauti zetu hazipelekei kukoseana au kuvunjiana heshima kwahiyo tunaomba serikali iamini uwepo wa maelewano mazuri tu kwa maendeleo ya nchi hii” alisema Sheikh Mussa
Semina hiyo ya Siku mbili imejumuisha viongozi wa Taasisi mia moja huku mada ya Nafasi ya Taasisi za Kiislam katika Kuleta Umoja na Kuishi kwa Amani itajadiliwa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.