Habari za Punde

Wananchi Waaswa Kufanya Kazi Kwa Bidii na Weledi

Mkurugenzi  Mtendaji  wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino Bw. Athmani Masasi akisisitiza  umuhimu wa wananchi wa Wilaya ya Chamwino hasa Vijiji vilivyopatiwa mafunzo ya kuwajengea uwezo baada ya kurasimisha mashamba yao na  kupatiwa hati za haki miliki za kimila za kumiliki ardhi ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kuwakwamua wakulima ili waweze kuzalisha kwa tija. Mafunzo hayo yameratibiwa na Ofisi ya Rais, Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA).
Meneja Urasimishaji  Ardhi   Vijijini kutoka Ofisi ya Rais, Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) Bw. Anthony Temu akiwaasa wananchi wa Wilaya ya Chamwino kutumia fursa zinazojitokeza baada ya kurasimisha mashamba yao ili kuongeza tija, Mafunzo  hayo yakuwaongezea ujuzi  ni moja ya mkakati wa Serikali kuwakwamua wakulima baada ya kurasimisha mashamba yao.
Sehemu ya wakulima  wa Kijiji cha Mahama Wilayani Chamwino  wakifuatilia mafunzo ya kuwajengea uwezo ili waweze kuongeza tija katika uzalishaji baada ya mafunzo yaliyoendeshwa  na Ofisi ya Rais, Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino.
Kikundi cha ngoma kikionesha umahiri wake wakati wa hafla ya kufunga mafunzo kwa wakulima zaidi ya 100 wa kijiji cha Mahama Wilayani Chamwino.  Mafunzo yaliyoendeshwa  na Ofisi ya Rais, Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya hiyo.

Mkurugenzi  Mtendaji  wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino Bw. Athmani Masasi akiwa kwenye picha ya pamoja na sehemu ya wakulima  walioshiriki katika mafunzo yakuwajengea uwezo ili waweze kuzalisha kwa tija.
(Picha zote na Frank Mvungi- Dodoma)



Na; Frank Mvungi- MAELEZO, Dodoma                                                                                              
Wananchi  Wilayani Chamwino Wameaswa Kufanya Kazi kwa Bidii ili kuendana na azma ya Serikali ya Awamu ya Tano kuwaletea wananchi maendeleo kwa kutumia rasilimali zilizopo katika maeneo yaoikiwemo Ardhi.

Akizungumza  wakati wa kufunga mafunzo kwa wakulima zaidi ya mia moja wa kijiji cha Mahama Wilayani humo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo Bw. Athmani Masasi amesema kuwa wananchi wote wanapaswa kuunga mkono juhudi za Serikali  kwa kufanya kazi kwa kufuata mfano wa Mhe. Rais, Dkt. John Pombe Magufuli ili ili kufikia maendeleo endelevu.

" Hati za  haki milki ya kimila zimepunguzwa bei kutoka  elfu ishirini hadi elfu mbili mia saba tu ili kila mwananchi wa Wilaya ya Chamwino aweze kuunga mkono juhudi za Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli kuwaletea wanyonge maendeleo na kuwakwamua kiuchumi" Alisisitiza Masasi

Akifafanua amesema kuwa Halmashauri hiyo itaendelea kuweka mikakati yakuwezesha wananchi wote wanamiliki maeneo yaliyopimwa na kuwa rasmi kwa ajili ya shughuli za kiuchumi hali itakayosaidia kuongeza kasi ya maendeleo.

Pia alipongeza Ofisi ya Rais, Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge Tanzania (MKURABITA) kwa hatua inazochukua katika kuwajengea uwezo wananchi ili waweze kuwa na uzalishaji wenye tija hasa kupitia urasimishaji wa mashamba yao.

Kwa upande wake Meneja Urasimishaji Ardhi Vijijini  kutoka MKURABITA Bw. Antony Temu amesema kuwa wakulima wa kijiji cha Mahama wamewezeshwa kutekeleza dhana ya kilimo chenye tija,  ufugaji wa kisasa, utunzaji wa kumbukumbu, utafutaji wa fursa na kuzitumia, utunzaji kumbukumbu, namna ya kukuza mitaji, ushirika na utunzaji wa mazingira.

Aliongeza kuwa Dhamira ya MKURABITA ni kuona wananchi wanakuwa na ustawi unaotokana na rasilimali zilizopo katika maeneo yao ikiwemo ardhi.

Aidha, alimshukuru Mhe. Rais, Dkt. John Pombe Magufuli  kwa kuendelea kuwezesha mpango huo kutekeleza jukumu la kuwawezesha wananchi kiuchumi ili wachangie katika kujenga uchumi wa viwanda kwa kuzalisha malighafi zenye ubora kupitia  sekta ya kilimo.

MKURABITA  imewajengea uwezo wakulima zaidi ya mia mbili katika Vijiji vya Mahama na Membe ambapo kila kijiji kilifanikiwa kutoa wakulima mia moja kushiriki katika mafunzo hayo yaliyolenga kuwapa ujuzi wa kuongeza tija katika sekta ya kilimo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.