Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akijumuika na Wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba katika Futari Maalum aliyowaandalia katika viwanja vya Ikulu Ndogo Chakechake Pemba kushoto Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabi na kulia Naibu Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Mahmoud Mussa Wadi, wakijumuika katika futari hiyo iliofanyika jana 16-5-2019 na Mufn
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed
Shein amefutari pamoja na wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba na kuwataka kuendeleza
amani na utulivu uliopo nchini ili maendeleo zaidi yazidi kupatikana.
Hafla hiyo ya futari iliyoandaliwa
na Rais Dk. Shein kwa ajili ya wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba ilifanyika katika viwanja vya Ikulu
ndogo Chake Chake, na kuhudhuriwa na
viongozi mbali mbali wa Serikali, dini, vyama vya siasa pamoja na wananchi wa
Mkoa huo.
Akitoa neno la
shukurani kwa niaba ya Rais Dk. Shein, Mkuu wa Mkoa huo Hemed Suleiman alieleza
kuwa amani na utulivu ndio msingi wa maendeleo hivyo kila mmoja anapaswa
kuilinda na kuiendeleza kwa nguvu zake zote.
Alisisitiza kuwa
maendeleo yote yaliopatikana nchini yametokana na kuwepo kwa amani na utulivu mkubwa
ambayo ndio chachu ya mafanikio hayo na kusisitiza kuwa Serikali itaendelea
kuyakuza maendeleo hayo kwa kadri uwezo utakapopatikana.
Alhaj Dk. Shein
aliwatakia Ramadhani njema wananchi wa Mkoa huo na kuwasisitiza kuutukuza mwezi
huo mtukufu kwa kusoma sana Qur-an kwani ndio mwezi ulioshuka kitabu hicho
kitakatifu.
Alhaj Dk. Shein
aliwataka wananchi wa Mkoa huo kuendelea kushirikiana na kupendana sambamba na
kuwa wamoja huku akiwataka kuachama na mambo yote yaliyokatazwa ndani ya mwezi
huu na miezi mengineyo ili waendelee kupata neema za Allah.
Aidha, alisisitiza umuhimu
wa kupambana na vitendo na matukio yanayovunja maadili ya dini ya kiislamu na
ambayo hayapaswi kufanyika katika jamii ukiwemo udhalilishaji wa wanawake na
watoto pamoja na matumizi ya dawa za kulevya ambayo hayaleti taswira nzuri
katika jamii.
Pia, Alhaj Dk. Shein
alisisitiza haja ya kuendelezwa na kudumishwa kwa usafi hasa katika kipindi
hichi cha msimu wa mvua huku akieleza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
katika kupambana na athari za mvua kwa Unguja na Pemba.
Pamoja na hayo, Alhaj
Dk. Shein aliwashukuru wananchi wote waliohudhuria katika futari hiyo aliyowaandalia
na kupongeza jinsi walivyoonesha upendo mkubwa kwake wa kukubali muwaliko wake
huo.
Nao wananchi wa Mkoa
wa Kusini Pemba wakitoa neno la shukurani kwa upande wao ambalo lililotolewa na
Sheikh Mohamed Suleiman ambaye pia, ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Istiqama Pemba walieleza
kufarajika kwao na futari hiyo maalum waliyoandaliwa na Rais wao na kueleza
jinsi walivyoifurahia.
Wananchi wa Mkoa huo
walieleza kuridhishwa kwao na juhudi kubwa anazozichukua Rais Dk. Shein kwa
kuwapelekea maendeleo makubwa wananchi wa Zanzibar wakiwemo wa kisiwa cha Pemba
ukiwemo Mkoa wao wa Kusini.
Sheikh Mohamed
alieleza kuwa Rais Dk. Shein amekuwa akifuata sunna na fadhila za Mtume
Mohammad (S.A.W) ya kuwafutarisha watu katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhan
jambo ambalo limesisitizwa katika mwezi huu kutokana na fadhila zake.
Aidha, wananchi hao walitumia
fursa hiyo kumuombea dua Rais Dk. Shein kwa ukarimu na upendo wake mkubwa aliyowaonesha
wananchi hao pamoja na ukarimu anaoendelea kuwaonesha wananchi wote wa Zanzibar
katika kipindi hichi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani na katika kipindi chote cha
uongozi wake.
Wakati huohuo, nae Mama Mwanamwema
Shein kwa upande wake alishirikiana kikamilifu na viongozi wanawake wa kitaifa
pamoja na wananchi wa Mkoa huo wa Kusini katika futari hiyo maalum aliyoianda
Rais Dk. Shein.
Akitoa neno la
shukurani Mshauri wa Rais Pemba Dk. Mauwa Abeid Daftari alitoa shukurani kwa
Rais Dk. Shein kwa ukarimu wake anaoendelea kuuonesha kwa wananchi wake
sambamba na kusisitiza umoja na mshikamano miongoni mwa wananchi.
Leo Alhaj Dk. Shein
anatarajiwa kuungana pamoja na wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba katika
futari maalum aliyowaandalia.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment