Habari za Punde

Amani na Utulivu Ndio Msingi wa Maendeleo Kila Mmoja Anapaswa Kuilinda na Kuiendeleza Kwa Nguvu Zote.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akijumuika na Wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba katika Futari Maalum aliyowaandalia katika viwanja vya Ikulu Ndogo Chakechake Pemba kushoto Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabi na kulia Naibu Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Mahmoud Mussa Wadi, wakijumuika katika futari hiyo iliofanyika jana 16-5-2019  na Mufn


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein amefutari pamoja na wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba na kuwataka kuendeleza amani na utulivu uliopo nchini ili maendeleo zaidi yazidi kupatikana.

Hafla hiyo ya futari iliyoandaliwa na Rais Dk. Shein kwa ajili ya wananchi wa Mkoa wa Kusini  Pemba ilifanyika katika viwanja vya Ikulu ndogo Chake Chake, na kuhudhuriwa  na viongozi mbali mbali wa Serikali, dini, vyama vya siasa pamoja na wananchi wa Mkoa huo.

Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya Rais Dk. Shein, Mkuu wa Mkoa huo Hemed Suleiman alieleza kuwa amani na utulivu ndio msingi wa maendeleo hivyo kila mmoja anapaswa kuilinda na kuiendeleza kwa nguvu zake zote.

Alisisitiza kuwa maendeleo yote yaliopatikana nchini yametokana na kuwepo kwa amani na utulivu mkubwa ambayo ndio chachu ya mafanikio hayo na kusisitiza kuwa Serikali itaendelea kuyakuza maendeleo hayo kwa kadri uwezo utakapopatikana.

Alhaj Dk. Shein aliwatakia Ramadhani njema wananchi wa Mkoa huo na kuwasisitiza kuutukuza mwezi huo mtukufu kwa kusoma sana Qur-an kwani ndio mwezi ulioshuka kitabu hicho kitakatifu.

Alhaj Dk. Shein aliwataka wananchi wa Mkoa huo kuendelea kushirikiana na kupendana sambamba na kuwa wamoja huku akiwataka kuachama na mambo yote yaliyokatazwa ndani ya mwezi huu na miezi mengineyo ili waendelee kupata neema za Allah.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa kupambana na vitendo na matukio yanayovunja maadili ya dini ya kiislamu na ambayo hayapaswi kufanyika katika jamii ukiwemo udhalilishaji wa wanawake na watoto pamoja na matumizi ya dawa za kulevya ambayo hayaleti taswira nzuri katika jamii.

Pia, Alhaj Dk. Shein alisisitiza haja ya kuendelezwa na kudumishwa kwa usafi hasa katika kipindi hichi cha msimu wa mvua huku akieleza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kupambana na athari za mvua kwa Unguja na Pemba.

Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein aliwashukuru wananchi wote waliohudhuria katika futari hiyo aliyowaandalia na kupongeza jinsi walivyoonesha upendo mkubwa kwake wa kukubali muwaliko wake huo.

Nao wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba wakitoa neno la shukurani kwa upande wao ambalo lililotolewa na Sheikh Mohamed Suleiman ambaye pia, ni Mkurugenzi wa Taasisi ya Istiqama Pemba walieleza kufarajika kwao na futari hiyo maalum waliyoandaliwa na Rais wao na kueleza jinsi walivyoifurahia.

Wananchi wa Mkoa huo walieleza kuridhishwa kwao na juhudi kubwa anazozichukua Rais Dk. Shein kwa kuwapelekea maendeleo makubwa wananchi wa Zanzibar wakiwemo wa kisiwa cha Pemba ukiwemo Mkoa wao wa Kusini.

Sheikh Mohamed alieleza kuwa Rais Dk. Shein amekuwa akifuata sunna na fadhila za Mtume Mohammad (S.A.W) ya kuwafutarisha watu katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhan jambo ambalo limesisitizwa katika mwezi huu kutokana na fadhila zake.

Aidha, wananchi hao walitumia fursa hiyo kumuombea dua Rais Dk. Shein kwa ukarimu na upendo wake mkubwa aliyowaonesha wananchi hao pamoja na ukarimu anaoendelea kuwaonesha wananchi wote wa Zanzibar katika kipindi hichi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani na katika kipindi chote cha uongozi wake.

Wakati huohuo, nae Mama Mwanamwema Shein kwa upande wake alishirikiana kikamilifu na viongozi wanawake wa kitaifa pamoja na wananchi wa Mkoa huo wa Kusini katika futari hiyo maalum aliyoianda Rais Dk. Shein.

Akitoa neno la shukurani Mshauri wa Rais Pemba Dk. Mauwa Abeid Daftari alitoa shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa ukarimu wake anaoendelea kuuonesha kwa wananchi wake sambamba na kusisitiza umoja na mshikamano miongoni mwa wananchi.

Leo Alhaj Dk. Shein anatarajiwa kuungana pamoja na wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba katika futari maalum aliyowaandalia.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.