Habari za Punde

MAKAMPUNI MATATU YATAKAYOSAFIRISHA MASHABIKI WA SOKA KULEKEA MISRI NA TAIFA STARS YATANGAZWA

Mkurugenzi wa Michezo Yusuph Singo, akizungmza na Waandishi wa Habari (hawapo pichani), leo Jumamosi, 25 Mei 2019, kuhusu Kutoa kibali kwa Makampuni matatu yatakayosafirisha watanzania kwenda kuiunga mkono Timu ya Taifa (Taifa Stars) katika Michuano ya Mataifa ya Africa (AFCON) Nchini Misri June 21, 2019 hadi Julai 19, 2019, kulia kwake ni Mwakilisha wa kampuni ya Clouds Media Group (CMG), Shafii Dauda na Mwakilishi kutoka World Link, Zaki Admani.
Mwakilisha wa kutoka kampuni ya Clouds Media Group, Shafii Dauda akieleza jambo kuhusu namna ya kuwasafirisha watanzania watakajitokeza kwenda kuiunga mkono Timu ya Taifa (Taifa Stars) katika Michuano ya Mataifa ya Africa (AFCON) Nchini Misri June 21, 2019 hadi Julai 19, 2019, baada CMG kupata kibali hicho kutoka kwa Serikali, Kushoto ni Mwakalishi kutoka Kampuni ya Travel Link, Ephrem Mtuya, Mkurugenzi wa Michezo, Yusuph Singo na Mwakilishi kutoka World Link, Zaki Admani
Mwakalishi kutoka Kampuni ya Travel Link, Ephrem Mtuya, akizungumza mbele ya Waandishi wa Habari (hawapo pichani), kuhusu namna ya kuwasafirisha watanzania watakajitokeza kwenda kuiunga mkono Timu ya Taifa (Taifa Stars) katika Michuano ya Mataifa ya Africa (AFCON) Nchini Misri June 21, 2019 hadi Julai 19, 2019, Baada ya Kampuni hiyo kupata kibali hicho kutoka kwa Serikali Kushoto ni Mkurugenzi Mkuu kutoka Travel Link, Doreen Gafoor na kulia ni Mkurugenzi wa Michezo Yusuph Singo.
(Picha na Paschal Dotto-Maelezo ) 




Na Mwandishi Wetu,Maelezo DAR ES SALAAM. 
SERIKALI kwa kushirikiana na Shirikisho la Soka Nchini (TFF) imeyataja Makampuni matatu yatakayotumika kusafirisha Mashabiki wa Soka na Watanzania kwa ajili ya kuishangilia Timu ya Soka ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ wakati wa Michuano ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) zitakazofanyika Mwezi Juni, mwaka huu nchini Misri.
Akizungumza na Waandishi wa Vyombo ya Habari leo Jumamosi (Mei 25, 2019), Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo, Yusuph Singo aliyataja Makampuni hayo kuwa ni pamoja na Clouds Entertainment Group Ltd, Travel Link na World Link, ambayo yalishinda mchakato wa ushindani na makampuni mengine kutokana na kukidhi vigezo mbalimbali vilivyoanishwa.
Kwa mujibu wa Singo alisema Serikali na kwa kushirikiana na Shirikisho la Soka Nchini (TFF) waliamua kusimamia mchakato wa kupata makampuni hayo ili kuzuia aina yoyote ya utapeli kwa Watanzania hususani Mashabiki wa Soka wa hapa nchini watakaojitokeza kwenda Nchini Misri kuipa nguvu ya ushingiliaji Taifa Stars.
“Katika miaka ya nyuma kulikuwa na utapeli katika haya makampuni ya usafirishaji, hivyo Serikali kwa kushirikiana na TFF tumeyapata Makampuni matatu, bei zao zitakuwa rahisi na wamepanga kuwa na nembo ya pamoja ambayo wataitangaza ili iweze kujulikana na Watanzania” alisema Singo.
Aidha Singo alisema kuhusu utaratibu wa visa za kusafiri makampuni hayo kwa kushirikana na TFF yatatoa taarifa ya jinsi Mashabiki wa Soka watavyoweza kupata huduma hiyo kabla ya kuanza kwa michuano hiyo inayotarajia kuanza kutimua vumbi tarehe 21 Juni mwaka huu.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Kampuni ya Clouds Entertainment Group Ltd, Shaffih Dauda alisema Kampuni yao imejipanga vyema kuhakikisha kuwa inatoa huduma zote muhimu kwa Watanzania watakaosafiri kwenda Nchini Misiri kuishangalia Taifa Stars ikiwemo visa, usafiri wa ndani, malazi katika kipindi cha siku 10 za mechi tatu za makundi itayocheza Taifa Stars.
“Clouds Entertainment Ltd kila mwaka tuna msimu wa kulevya wa soka, mwaka jana tulikuwa na  Msimu wa kulevya wa Kombe la Dunia kule nchini Urusi, na sasa tunarudi Afrika na tutawahudumia vyema mashabiki watakaojitokeza kwa kiasi cha Dola za Kimarekani 1650 na pia tutaoa ofa ya Mashabiki hao kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo nchini Misri” alisema Dauda.
Aliongeza kuwa katika kutoa urahisi wa huduma kwa Watanzania hususani suala la malazi, Kampuni yao tayari kwa kushirikiana na wakala wao aliyopo nchini Misri, wamepata mmoja wa Mitaa maarufu nchini Misri ujulikanao Kilimanjaro ambapo utawezesha Mashabiki wa Watanzania kupata huduma zote muhimu kuwafanya Mashabiki hao huko kujiona kuwa wapo nyumbani.
Kwa upande wake, Meneja Maendeleo ya Masoko wa Kampuni ya World Link, Zaki Admani alisema kampuni hiyo itatoza kiasi cha Dola za Kimarekani 1550 kwa Mashabiki wa Soka, ambayo watasafiri kuelekea Nchini Misri pamoja na kutoa ofa ya kuchagua mechi moja yoyote ambayo mshabiki wa Soka atapenda kuingalia katika timu zitakazochuana na Taifa Stars.
Aliongeza kuwa kuanzia Jumatatu ya wiki ijayo Kampuni hiyo itatoa kifurushi kitakachomwezesha Shabiki wa Soka hapa nchini kuweza kuchagua idadi ya mechi ambazo atapenda kuziangalia wakati akiwa na Timu ya Taifa Stars nchini Misri.
“Wapo wengine watapenda kuangalia mechi moja, na hili tumeliangalia na mapema wiki ijayo kuanzia jumatatu tutatoa utaratibu wake wa namna ya kuwasaidia mashabiki wa aina hii” alisema Admani.
Naye Meneja Utawala wa Kampuni ya Travel Link, Ephrem Mtuya alisema kuwa kwa miaka 15 sasa Kampuni hiyo imekuwa ikifanya kazi pamoja na TFF kwa ajili ya kuwasifirisha wachezaji wa Timu ya Taifa ya Tanzania katika nchini mbalimbali na hivyo amewataka Watanzania kujitokeza kwa wingi kusafiri na Kampuni hiyo ili kwenda kuipa nguvu Timu ya Taifa ya Tanzania ikiwa nchini Misri.
Alisema Kampuni imeweka kiwango cha Dola za Kimarekani 1300 pekee kwa Mtanzania yotote atayapenda kusafiri na Timu hiyo hususani Mashabiki wa Soka ikihusisha Gharama za Tiketi ya Ndege, usafiri, pamoja na huduma za malazi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.