Habari za Punde

WANANCHI WA KATA YA CHITA MELELA WAISHUKURU TARURA

Wahandisi kutoka Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) wakiwa katika ujenzi wa Daraja la Chuma (Mabey Bridge) lililopo Mto Kihansi katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero, Mkoani Morogoro.
Na. Erick Mwanakulya.
Wananchi wa Kata ya Chita Melela iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro, wameshukuru Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) baada ya kutatuliwa kwa kero yao ya muda mrefu kwa kujengewa Daraja la Chuma (Mabey Bridge) lililopo Mto Kihansi ambalo linajengwa na TARURA chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo ya Kimataifa la Uingereza (DFID).
Hayo yameelezwa na wananchi waliojitokeza kushuhudia ujenzi wa Daraja hilo linalojengwa na Wahandisi wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA), wakisaidiana na Mhandisi Mshauri Ebenezer Mollel pamoja na Mtaalamu wa Ufundi  John Hinderer kutoka Kampuni ya Mabey Bridge ya nchini Uingereza.
Wakielezea furaha yao juu ya ujenzi wa daraja hilo, wananchi hao wamesema kuwa wanaishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuwajengea daraja maana walikuwa wanapata shida kubwa hapo awali katika kusafirisha bidhaa zao na kupata huduma mbalimbali za kijamii kwani walikuwa wanatumia mtumbwi kuvuka Mto ambapo ni umbali takribani Km 1.5.
Kwaupande wake, Diwani wa Kata ya Chita Melela Mhe. Chelele John amesema, Serikali ya Awamu ya Tano inastahili kupongezwa kwa maana Daraja hilo ni kiungo muhimu katika uchumi wa Kata yake pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero kwa maana vyanzo vya mapato katika Kata za Mlimba, Chita, Mgeta, Mangula pamoja na Mchombe vitakusanywa kwa urahisi kutokana na uwepo wa daraja hilo.
“Tulikuwa tunatumia mtumbwi kuvuka Mto na wananchi walipata adha kubwa katika Kijiji chetu kwani kufikia huduma za kijamii ilikuwa changamoto kubwa, leo hii naona Wahandisi wa TARURA wapo hapa katika ujenzi wa Daraja hili, hii inadhihirisha kuwa Wakala upo katika kuhudumia wananchi ipasavyo nasi tunawaunga mkono”, alisema Diwani huyo.
Naye, Mratibu wa TARURA Mkoa wa Morogoro, Mhandisi Godwin Mpinzile amesema Daraja la Chuma (Mabey Bridge) la Mto Kihansi limewekwa baada ya kutengeneza barabara ya Chita Melela yenye urefu wa Km 11.5 na litakuwa mkombozi kwa wananchi wa Chita kutokana na shida wanayoipata wakati wa mvua na kwamba Wakala utaendelea kuikarabati Barabara hiyo hadi kuunganisha Kata ya Mlimba ili kuwarahisishia wananchi kufanya shughuli zao za kila siku.
Pia, amewasihi wakazi wa Chita kutunza miundombinu ya Barabara pamoja na Daraja kwani gharama kubwa zimetumika katika ujenzi wa Daraja hilo.
Daraja la kisasa la Chuma (Mabey Bridge) ambalo limegharimu zaidi ya shilingi milioni 700 ni moja kati ya kazi za Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) katika kuboresha Barabara na kufanya matengenezo pamoja na ujenzi wa Madaraja ili kuwawezesha wananchi kufanya shughuli zao za kiuchumi.
Daraja hilo linalenga kutatua kero ya kudumu kwa wananchi wa Chita Melela kutokana na Madaraja ya hapo awali kusombwa na maji pale mvua zinaponyesha na linatarajiwa kuzinduliwa hivi karibuni.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.