Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mh.Dk Ali Mohamed Shein akipata maelezo kutoka kwa Meneja Mkuu wa kiwanda cha Kampuni ya Kimataifa ya Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia cha Ras Al Khaimah (RAK GAS) Peter Deibel wakati alipotembelea kiwanda hicho, akiwa katika ziara yake Ras Al-Khaimah leo.
Mwangalizi Mkuu wa Uzalishaji wa kiwanda cha Kampuni ya Kimataifa ya Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia cha Ras Al Khaimah (RAK GAS) Deepu Thomas Akimueleza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe. Dk Ali Mohamed Shein jinsi ya kiwanda hicho kinavyoendesha shughuli zake za uzalishaji wa Gesi wakati Mh.Rais alipofanya ziara katika kiwanda hicho.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein ametembelea kiwanda cha Kampuni ya Kimataifa ya Utafiti na
Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia ya
Ras Al Khaimah “RAK GAS” iliyopo nje kidogo
ya mji wa Ras Al Khaimah na kujionea shughuli za kiwanda hicho.
Katika kiwanda hicho ambacho kimekuwa kikifanya
shughuli mbali mbali za kupokea gesi kutoka katika maeneo maalum ya uchimbaji, kuisambaza
sambamba na kuihifadhi kwa lengo la kuweza kuitumia.
Akiwa na ujumbe wake, Dk. Shein alipata maelezo
kutoka kwa viongozi wa Kampuni hiyo ya Kimataifa ya Utafiti na
Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia ya
Ras Al Khaimah “RAG GAS” akiwemo Meneja
Mkuu Peter Deibel, Msaidizi Meneja Mwendeshaji
Jody Labbie na Mwangalizi Mkuu wa Uzalishaji Deepu Thomas ambaye alitoa
ufafanuzi juu ya uzalishaji pamoja na usambazaji wa gesi asilia kiwandani hapo.
Rais Dk. Shein alieleza kuvutiwa na shughuli
mbali mbali zinazofanywa na kiwanda hicho katika eneo hilo lililopo nje kidogo
ya mji wa Ras Al Khaimah ambalo ni muhimu katika shughuli za gesi asilia ambayo
imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya Ras Al Khaimah.
Alipongeza hatua kubwa za maendeleo pamoja na
mchango mkubwa wa mradi huo wa gesi kwa uchumi na maendeleo ya Ras Al Khaimah
unatokana na mikakati madhubuti iliyowekwa katika kuhakikisha juhudi hizo
zinachangia na kuendeleza soko la ajira, ukuaji wa uchumi na maendeleo ya
viwanda katika nchi hiyo.
Viongozi hao wa kiwanda hicho cha Kampuni ya “RAG
GAS” walimueleza Rais Dk. Shein shughuli mbali mbali zinazofanywa katika eneo
hilo la kiwanda cha gesi na kutoa maelezo yanayohusiana na usafirishwaji kutoka
maeneo inayozalishwa gesi hiyo hadi kiwandani hapo.
Aidha, walimueleza Rais Dk. Shein hatua na njia
zinazotumika kusafirisha gesi hiyo asilia kutoka kiwandani hapo hadi katika
maeneo inayotumika ambapo kwa maelezo ya viongozi hao wakuu Kampuni ya “RAG GAS”,
gesi hiyo imekuwa na mchango mkubwa wa uchumi wa Ras Al Khaimah.
Viongozi hao walimueleza Rais Dk. Shein pamoja na
ujumbe wake kuwa gesi hiyo imekuwa ikisaidia kwa kiasi kikubwa katika matumizi
ya ndani ya nchi na nje ya Ras Al Khaimah sambamba na kuhangia katika
kuimarisha viwanda vikiwemo viwanda vya saruji pamoja na viwanda vya vifaa vya
ujenzi.
Kwa maelezo ya viongozi wa Kampuni hiyo ya “RAG
GAS”, Ras Al Khaimah imekuwa ikichangia sana katika sekta ya ujenzi kwa nchi za
Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kutokana na rasilimali mbali mbali
zinazozalishwa nchini humo.
Walieleza kuwa rasilimali hizo zimeweza
kuendeleza viwanda na kukuza uchumi mchanganyiko, kukuza soko la ajira pamoja
na kuongeza thamani ya bidhaa mbali mbali zinazozalishwa nchini humo ambazo
zina ubora mkubwa na zimekuwa maarufu sana duniani.
Mapema katika ukumbi wa Hoteli ya Waldorf Astoria
mjini Ras Al Khaimah, Rais Dk. Shein akiwa
na viongozi wa ujumbe aliofuatana nao walikutana na viongozi wa ngazi za juu wa
Kampuni ya “RAS GAS” na kumpa taarifa juu ya hatua zilizofikiwa katika utafiti
wa mafuta na gesi asilia unaofanywa Zanzibar.
Katika utoaji wa taarifa hiyo, viongozi hao wakiongozwa
na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya “RAG GAS” Nishant Dighe pamoja na viongozi wa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar wote kwa pamoja walisisitiza haja ya kuendeleza zaidi
ushirikiano katika shughuli hiyo ya utafiti, uendelezaji na uchimbaji wa mafuta
na gesi asilia Zanzibar.
Sambamba na hayo viongozi wa Kampuni hiyo walitoa
pongezi kwa viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi
wake kwa mashirikiano makubwa wanayoyapata hatua ambayo inarahisisha zaidi
utekelezaji wa utafiti huo.
Nao viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kwa upande wao waliahidi kuendeleza ushirikiano uliopo kati yake na Kampuni
hiyo kwa lengo la kufikia mipango na mikakati iliyowekwa yenye tija kwa pande mbili hizo na kuipongeza Kampuni hiyo
kwa mashirikiano hayo makubwa inayoonesha kwa Serikali.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment