Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk.Ali Mohamed Shein. Atembelea Kiwanda cha Kampuni ya Kimataifa ya Utafiti na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia "RAK GAS" Ras Al Khaimah leo.


 Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mh.Dk Ali Mohamed Shein akipata maelezo kutoka kwa Meneja Mkuu wa kiwanda cha Kampuni ya Kimataifa ya Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia cha Ras Al Khaimah (RAK GAS) Peter Deibel wakati alipotembelea kiwanda hicho, akiwa katika ziara yake Ras Al-Khaimah leo.
Mwangalizi Mkuu wa Uzalishaji wa kiwanda cha Kampuni ya Kimataifa ya Uchimbaji wa Mafuta na Gesi  Asilia cha Ras Al Khaimah (RAK GAS) Deepu Thomas Akimueleza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe. Dk Ali Mohamed Shein jinsi ya kiwanda hicho kinavyoendesha shughuli zake za uzalishaji wa Gesi wakati Mh.Rais alipofanya ziara katika kiwanda hicho.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametembelea kiwanda cha Kampuni ya Kimataifa ya Utafiti na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia  ya Ras Al Khaimah “RAK GAS” iliyopo nje kidogo ya mji wa Ras Al Khaimah na kujionea shughuli za kiwanda hicho.

Katika kiwanda hicho ambacho kimekuwa kikifanya shughuli mbali mbali za kupokea gesi kutoka katika maeneo maalum ya uchimbaji, kuisambaza sambamba na kuihifadhi kwa lengo la kuweza kuitumia.

Akiwa na ujumbe wake, Dk. Shein alipata maelezo kutoka kwa viongozi wa Kampuni hiyo ya Kimataifa ya Utafiti na Uchimbaji wa Mafuta na Gesi Asilia  ya Ras Al Khaimah “RAG GAS” akiwemo Meneja Mkuu Peter Deibel, Msaidizi Meneja Mwendeshaji  Jody Labbie na Mwangalizi Mkuu wa Uzalishaji Deepu Thomas ambaye alitoa ufafanuzi juu ya uzalishaji pamoja na usambazaji wa gesi asilia kiwandani hapo.

Rais Dk. Shein alieleza kuvutiwa na shughuli mbali mbali zinazofanywa na kiwanda hicho katika eneo hilo lililopo nje kidogo ya mji wa Ras Al Khaimah ambalo ni muhimu katika shughuli za gesi asilia ambayo imekuwa na mchango mkubwa katika maendeleo ya Ras Al Khaimah.

Alipongeza hatua kubwa za maendeleo pamoja na mchango mkubwa wa mradi huo wa gesi kwa uchumi na maendeleo ya Ras Al Khaimah unatokana na mikakati madhubuti iliyowekwa katika kuhakikisha juhudi hizo zinachangia na kuendeleza soko la ajira, ukuaji wa uchumi na maendeleo ya viwanda katika nchi hiyo.

Viongozi hao wa kiwanda hicho cha Kampuni ya “RAG GAS” walimueleza Rais Dk. Shein shughuli mbali mbali zinazofanywa katika eneo hilo la kiwanda cha gesi na kutoa maelezo yanayohusiana na usafirishwaji kutoka maeneo inayozalishwa gesi hiyo hadi kiwandani hapo.
  
Aidha, walimueleza Rais Dk. Shein hatua na njia zinazotumika kusafirisha gesi hiyo asilia kutoka kiwandani hapo hadi katika maeneo inayotumika ambapo kwa maelezo ya viongozi hao wakuu Kampuni ya “RAG GAS”, gesi hiyo imekuwa na mchango mkubwa wa uchumi wa Ras Al Khaimah.

Viongozi hao walimueleza Rais Dk. Shein pamoja na ujumbe wake kuwa gesi hiyo imekuwa ikisaidia kwa kiasi kikubwa katika matumizi ya ndani ya nchi na nje ya Ras Al Khaimah sambamba na kuhangia katika kuimarisha viwanda vikiwemo viwanda vya saruji pamoja na viwanda vya vifaa vya ujenzi.

Kwa maelezo ya viongozi wa Kampuni hiyo ya “RAG GAS”, Ras Al Khaimah imekuwa ikichangia sana katika sekta ya ujenzi kwa nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) kutokana na rasilimali mbali mbali zinazozalishwa nchini humo.

Walieleza kuwa rasilimali hizo zimeweza kuendeleza viwanda na kukuza uchumi mchanganyiko, kukuza soko la ajira pamoja na kuongeza thamani ya bidhaa mbali mbali zinazozalishwa nchini humo ambazo zina ubora mkubwa na zimekuwa maarufu sana duniani.

Mapema katika ukumbi wa Hoteli ya Waldorf Astoria mjini Ras Al Khaimah,  Rais Dk. Shein akiwa na viongozi wa ujumbe aliofuatana nao walikutana na viongozi wa ngazi za juu wa Kampuni ya “RAS GAS” na kumpa taarifa juu ya hatua zilizofikiwa katika utafiti wa mafuta na gesi asilia unaofanywa Zanzibar.

Katika utoaji wa taarifa hiyo, viongozi hao wakiongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya “RAG GAS” Nishant Dighe pamoja na viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wote kwa pamoja walisisitiza haja ya kuendeleza zaidi ushirikiano katika shughuli hiyo ya utafiti, uendelezaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia Zanzibar.

Sambamba na hayo viongozi wa Kampuni hiyo walitoa pongezi kwa viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wake kwa mashirikiano makubwa wanayoyapata hatua ambayo inarahisisha zaidi utekelezaji wa utafiti huo.

Nao viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa upande wao waliahidi kuendeleza ushirikiano uliopo kati yake na Kampuni hiyo kwa lengo la kufikia mipango na mikakati iliyowekwa yenye tija kwa  pande mbili hizo na kuipongeza Kampuni hiyo kwa mashirikiano hayo makubwa inayoonesha kwa Serikali.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.