Mkurugenzi Idara ya Mswaada wa Kisheria Zanzibar Bi Hanifa Ramadhan Said akifungua mafunzo kwa wanufaika wa huduma ya Mswaada wa Kisheria kutoka Taasisi tofauti
Mashirikiano ya pamoja kutoka kwa wanufaika wa huduma ya msaada wa kisheria na watoaji huduma hio ndio chachu
itakayopelekea utekelezaji mzuri wa
majukumu ya Idara ya Msaada wa Kisheria katika kuleta ufanisi wa majukumu ya kazi
zao
Mkurugenzi wa Idara ya Msaada wa Kisheria Bi Hanifa Ramadhan
Said ameyasema hayo kwenye mkutano uliowashirikisha baadhi ya wanufaika wa
msaada wa kisheria uliofanyika katika ukumbi wa mkutano Wizara ya Katiba na
Sheria Mazizini
Bi Hanifa amesema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeanzisha Idara ya Msaada wa Kisheria ili
kuratibu utoaji na upatikanaji wa huduma ya kisheria kwa wananchi wote bila ya
kujali uwezo wa kifedha kwa mtaka huduma
Aidha Bi Hanifa amewashukuru wanufaika hao waliopatiwa
msaada kutoka vituo vinavyotoa huduma za msaada wa sheria kwa kukubali kufuata taratibu na kutoa
mashirikiano pale wanaposhughulikiwa malalamiko yao jambo ambalo linarahisisha
kupata haki zao stahiki kwa muda muafaka
Pia ametoa pongezi za
dhati kwa watoaji wa huduma ya msaada wa Kisheria kwa kuwapokea na
kuwashughulikia matatizo yao wananchi
bila upendeleo jambo ambalo limepelekea kutokuwepo kwa malalamiko kutoka
kwa wanufaika waliofika katika vituo vyao
“nimefarijika na michango iliyotolewa leo hii kutoka kwenu
hakuna hata mmoja aliyelalamika kuwa hakutendewa haki wakati alipotaka huduma
ya msaada wa Kisheria na mmeona mafanikio yake hivyo msisite kuwafahamisha na
wengine pale wanapopata matatizo hasa wanapodai haki zao za msingi wasiyamalize
kienyeji au kuona muhali bali wafuate
taratibu vituo hivi vipo kwa ajili
yenu”alisisitiza
Hata hivyo ameomba
kutosita kutoa maoni ama ushauri kwa
Idara ya Msaada wa Kisheria ili kuenda
sambamba na kasi ya maendeleo kwani lengo la Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ni
kukuza ustawi wa wananchi wake katika nyanja zote za maisha kwa kuwahudumia na
kuwaletea maendeleo na kuwaondolea uzito wa maisha yao ya kila siku
Bi Hanifa ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuweza kufanikisha kupatikana Sera,
Sheria na Kanuni inayosimamia sekta nzima ya msaada wa kisheria
Wakitoa mada kuhusu huduma za msaada wa kisheria watoa mada
na uchambuzi wa vifungu vya kanuni katika mafunzo hayo wanasheria ndugu Amour Omar Mbwana na ndugu Omar Haji Gora wamesema huduma za
msaada wa Kisheria zinajumuisha ushauri
wa kisheria, uwakilishi mahakamani au katika mabaraza, kutoa elimu ya kisheria,
pamoja na kutayarisha nyaraka za kisheria na taarifa kuhusiana na mambo ya
kisheria
Aidha wamefafanua baadhi ya vifungu kwa watu wasiokuwa na
sifa ya kupatiwa msaada wa kisheria kuwa ni pamoja na kampuni, shirika, taasisi
ya umma, Jumuiya ya kiraia , Jumuiya isiyokuwa ya kiserikali au mtu mwengine wa
kisheria .
Msisitizo pia umewekwa kuwa watoaji wa msaada
wa kisheria hawatatoa huduma za msaada wa kisheria kuhusiana na kesi za
madai zikiwemo masuala yanayohusu ulipaji wa kodi, ulipaji wa madeni na katika
kesi za ufilisi na kutoweza kulipa madeni
Nao washiriki wa mafunzo hayo wametoa shukurani zao kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa
kuanzisha Idara ya Msaada wa Kisheria na
kuomba idara hio kuendelea kutoa elimu na kuielimisha jamii ili waweze
kuifahamu na kuona umuhimu wa kufikisha malalamiko yao pale wanapohitaji
usaidizi wa huduma ya msaada wa kisheria
Washiriki hao wamezungumzia kuwa utaratibu huo wa kuwasaidia
kisheria wananchi wasiokuwa na uwezo Serikali inastahili kupongezwa kwa sababu
wamo wananchi wengi wanyonge wenye vilio vya muda mrefu, lakini hawana pa
kuvipeleka kutokana na unyonge.
Wameeleza kuwa jambo la muhimu kwa Taasisi inayohusika na
Utoaji wa Huduma za msaada wa Kisheria kuhakikisha wasiokuwa na uwezo ndio
wanaonufaika na utaratibu huo na kuomba kufanywa kila liwezekanalo kuwazuia wale
wenye uwezo wa kujisimamia ama kuendesha kesi ili waweze kupata haki zao
wenyewe kutojingia katika utaratibu huo na kuwazuia walengwa.
Wamesema kwamba wamo wananchi wengi ambao uwezo wao na
mwamamko wa kupigania haki zao ni mdogo, huku baadhi ya wananchi hao
wanashindwa na hata nauli ya kuwawezesha kufika mahakamani, hivyo uamuzi huo ni
jambo la kupongezwa kwa sababu umelenga hasa kuwakomboa wenye mahitaji.
No comments:
Post a Comment