Habari za Punde

WAZIRI MKUU ATAKA MIKOA ILIYOBAKIA ITEKELEZE AGIZO LAKE KUHUSU UWEKEZAJI

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa  akizungumza wakati alipofungua Kongamano la Uwekezaji Mkoa wa Pwani  kwenye ukumbi  wa Mkuu  wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani mjini Kibaha, Oktoba 19, 2019. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ameitaka mikoa ambayo bado haijatekeleza agizo lake la kuandaa makongamano ya uwekezaji ihakikishe inafanya hivyo mara moja.

Ametoa agizo hilo leo mchana (Jumamosi, Oktoba 19, 2019) wakati akifungua Kongamano la Uwekezaji kwa mkoa wa Pwani katika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa huo.

“Nitumie fursa hii kuwapongeza viongozi wa mkoa wa Pwani kwa kutekeleza agizo nililolitoa Juni 18, 2018 wakati wa kongamano la tatu la uwezeshaji wananchi kiuchumi la kuhakikisha mikoa yote inaandaa kongamano la uwekezaji na inakuwa na mwongozo wa uwekezaji wa mkoa. Mikoa ambayo haijatekeleza agizo hilo, ifanye hivyo mara moja,” amesema.

Waziri Mkuu amesema mkoa huo umeweza kubaini fursa zilizopo katika mkoa wa Pwani na kuzitangaza kupitia mwongozo wa uwekezaji ambao pia ameuzindua leo.

Amesema kaulimbiu ya kongamano hilo isemayo: ‘‘Ijenge Tanzania, wekeza Pwani mahali sahihi kwa uwekezaji (Build Tanzania, Invest in Pwani, the Best Place for Investment)” ina maana kuwa, licha ya mkoa wa Pwani kubainisha na kutangaza fursa za uwekezaji na biashara zilizopo, unajipambanua vizuri na kuonyesha kuwa ni kwa namna gani umejiandaa na umetengeneza mazingira bora yanayovutia wawekezaji wa ndani na nje.

“Ili kudhihirisha dhamira ya dhati ya kukuza uchumi kupitia viwanda, nimeelezwa kuwa mkoa umetenga hekta 53,016 kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda ambavyo vitatumia rasilmali zilizopo ndani ya mkoa na maeneo mengine ya nchi kwa lengo la kuchochea ukuaji wa uchumi na kuboresha maisha ya wanachi,” amesema. 

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri wahakikishe wanasimamia miundombinu inayoelekea kwenye viwanda vilivyopo kwenye maeneo yao.

"Kila mmoja ahakikishe maji, umeme na barabara vinafika kila eneo ambalo mwekezaji anataka kujenga kiwanda. Nitumie fursa hii kuwaomba mlete mabadiliko chanya yanayotokana na maboresho yanayofanywa na Serikali ya awamu ya tano." 


Mapema, akimkaribisha Waziri Mkuu kuzungumza na washiriki wa kongamano hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Bibi Angella Kairuki alisema kwamba Serikali imeanza kutekeleza mapendekezo ya mpango wa kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini (Blueprint for Improving Business Environment Regulatory Licensing in Tanzania) kwa kuondoa tozo 163 zilizokuwa zikilalamikiwa na wawekezaji.

“Pia tumetenganisha majukumu ya TBS ya TFDA ambayo sasa ni TMDA. TBS itashughulika na vyakula na TMDA itashughulika na dawa na vifaatiba. Vilevile, tumeondoa ada za usajili sehemu za kazi ambazo zamani ilikuwa ni sh. 28,000 na sasa hivi zinatolewa bure,” alisema.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhandisi Evarist Ndikillo aliwataka watu wote wanaotaka kuwekeza nchini waufikirie kwanza mkoa wa Pwani kwa sasabu uko kimkakati na una fursa nyingi ikiwemo hali nzuri ya usalama na kwa maana hiyo mitaji yao italindwa.

“Mkoa wetu uko kwenye eneo la kimkakati la kuwezesha biashara kwa kuwa uko karibu na bandari ya Dar es Salaam na uwanja wa ndege; uko karibu na soko kubwa ambalo ni Dar es Salaam; unapitiwa na reli zote kwenda mikoani na nchi jirani; unapitiwa na barabara kuu itokayo Dar es Salaam na pia una bandari kavu ya Kwala.”

Mbali ya hivyo, Mkuu huyo wa Mkoa alisema faida nyingine ambayo mkoa huo unayo ni uwepo wa miundombinu ya maji, umeme na nishati ya gesi asilia ambayo imeanza kutumiwa na baadhi ya viwanda kama Goodwill na Lodhia Steel.

Naye Dkt. Tausi Kida, Mkurugenzi wa Taasisi ya Uchumi ya Kijamii (ESRF) ambayo ilisimamia uandaaji wa mwongozo wa uwekezaji kwa mkoa wa Pwani, alisema taasisi yao inasaidia kuandaa na kuchambua fursa zilizopo kwenye mikoa mbalimbali. “Hadi sasa tumekwishaisadia mikoa 17 kuandaa miongozo ya uwekezaji na kwa sasa mikoa 12 imeshakamilisha na mikoa mitano iko kwenye hatua mbalimbali,” alisema.

Akitoa taarifa kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa CRDB, Abdulmajid Nsekela ambao ni wadhamini wakuu, Afisa Mkuu wa Biashara, Benki ya CRDB, Dkt. Joseph Witts alisema benki hiyo imeendelea kugusa sekta zote za uchumi na hivyo kuongeza tija kwenye mnyororo mzima wa uzalishaji.

Alisema huduma zao zimelenga kuongeza tija na ufanisi katika sekta ya viwanda nchini ikiwemo utoaji wa mikopo ya biashara kwa ajili ya kuongeza mikopo ya uendeshaji (working capita loans) na mikopo ya uwekezaji (investment loans).

“Benki yetu inatoa mikopo ya biashara na uwekezaji katika maeneo mbalimbali ambapo mikopo ya kilimo ni shilingi bilioni 357, uzalishaji wa viwanda (shilingi bilioni 214), biashara (shilingi bilioni 347), mahoteli (shilingi bilioni 87) na sekta ya madini (shilingi bilioni 91),” alisema.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAMOSI, OKTOBA 19, 2019.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.