Kamishna Jenerali
wa Magereza nchini Phaustine Kasike akizungumza katika kikao na Maafisa na
askari wa vituo vya Magereza Mkoa wa Dar es Salaam ambapo kikao hicho
kilijadili masuala mbalimbali ikmo, viwanda na ufugaji.
Kikao kazi hicho kimefanyika Bwalo Kuu la Maafisa Magereza, Ukonga jijini Dar
es Salaam.
Baadhi ya
Maafisa Waandamizi wa Jeshi la Magereza kutoka vituo vya Magereza Mkoa wa Dar
es Salaam wakimsikiliza Kamishna Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine
Kasike(hayupo pichani) kikao hicho kilijadili masuala mbalimbali ikiwemo
masuala ya utendaji kazi, maadili ya kazi, nidhamu na mikakati mbalimbali ya
Jeshi ikiwemo ya Kilimo, viwanda na ufugaji.
Askari wa vyeo
mbalimbali wa Jeshi la Magereza kutoka katika vituo vya Magereza Mkoa wa Dar es
Salaam wakifuatilia mazungumzo ya kikao kazi na Kamishna Jenerali wa Magereza
nchini Phaustine Kasike jana Desemba 20, 2019(Picha zote na Jeshi
la Magereza).
Na ASP Lucas Mboje, Jeshi la Magereza;
KAMISHNA Jenerali wa Magereza nchini, Phaustine
Kasike amewaasa Maafisa na askari wote wa Jeshi hilo kuendelea kutimiza
majukumu yao kwa kuzingatia nidhamu ya kazi na kufuata taratibu zilizopo ndani
ya Jeshi.
Amesema hayo jana katika kikao kazi na Maafisa na askari wa vituo vya
Magereza Mkoa wa Dar es Salaam ambapo kikao hicho kilijadili masuala mbalimbali
ikiwemo masuala ya utendaji kazi, maadili ya kazi, nidhamu na utekelezaji wa mikakati
mbalimbali ya Jeshi hilo ikiwemo mpango mkakakti wa kilimo, uwekezaji katika viwanda
na ufugaji.
Kamishna
Jenerali Kasike amesisitiza kuwa nidhamu ni muhimu Jeshini na amesema hakuna
mtu aliye juu ya nidhamu kwani msingi wa Jeshi lolote lile ni nidhamu.
"Taswira
ya Jeshi la Magereza inategemea zaidi utekelezaji mzuri wa majukumu yenu kwa
kuzingatia nidhamu na maadili ya kazi. “Kila mmoja lazima atimize
wajibu wake kikamilifu kwa kutumia uweledi, ubunifu na kuzingatia nidhamu ya kazi”,
alisisitiza Kamishna Jenerali Kasike.
Kamishna Jenerali Kasike amesema kuwa wapo baadhi
ya maafisa na askari ambao wanamatatizo ya kinidhamu na hawataki kubadilika hali ambayo inaharibu
taswira ya Jeshi hilo katika jamii.
Aidha, Kamishna Jenerali Kasike amekemea tabia ya
kutokufuata taratibu za uwasilishaji wa malalamiko kupitia utaratibu uliopo
ndani ya Jeshi hilo kwa baadhi ya maafisa na askari kwani tabia hiyo inachangia
sana katika kushuka kwa nidhamu ndani ya Jeshi.
“Jeshi ambalo halina nidhamu ni sawa na genge la
wahuni ambao wamevaa sare za Jeshi. Hivyo natoa wito kwa Maafisa na askari
wenye matatizo ya kinidhamu wajisahihishe na kujirekebisha ili kuendana na
misingi ya Jeshi”, aliongeza Jenerali Kasike.
Pia, amesema kuwa atahakikisha Shirika la Uzalishaji Mali la Magereza
(SHIMA) linajidhatiti zaidi katika miradi yake ili kujiimarisha katika kufanya
shughuli za kibiashara hapa nchini.
Kwa upande wake, Mkuu wa Magereza Mkoa wa Dar es
Salaam, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza, Julius Ntambala
amemhakikishia Mkuu huyo wa Jeshi la Magereza kuwa atahakikisha kuwa Maafisa na
askari katika Mkoa wake wanaendelea kutekeleza majukumu yao ya kazi kwa
kuzingatia Sheria, Kanuni na taratibu zilizopo katika uendeshaji wa Jeshi hilo.
No comments:
Post a Comment