Waziri wa
Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe akizungumza leo
Novemba 30,2019 Jijini Mwanza na Wanamichezo ambao ni wafanyakazi (hawapo
pichani) wakati alipofungua mashindano ya Michezo kwa Wafanyakazi wa Mashirika ya Umma na Binafsi yanayofanyika Jijini humo kuanzia tarehe 27
Novemba hadi 01 Desemba 2019,yanayongozwa na Kauli mbiu “SHIMMUTA 2019 Familia
Moja”lengo ikiwa ni kuimarisha afya na kubadilishana uzoefu kazini. Kulia ni
Mwenyekiti wa SHIMMUTA Bw. Khamis Mkanachi na Kushoto ni Mkuu wa Wilaya
Mhe.Dkt.Fillis Nyimbi.
Na. Shamimu Nyaki
–WHUSM ,Mwanza
Waziri wa
Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe ametangaza
kuwachukulia hatua Wanamichezo wasiokuwa Wafanyakazi maarufu kwa jina la “Mamluki”
wanaoshiriki Mashindano ya Michezo kwa Wafanyakazi
inayojulikana kama SHIMUTA na
SHIMIWI endapo watabainika.
Dkt.Mwakyembe amesema
hayo leo Jijini Mwanza wakati akifungua
michezo ya Mashirika ya Umma na Binafsi maarufu kwa jina la SHIMMUTA kwa niaba ya
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mama Samia Suluh Hassan
ambaye pia ndiye mlezi wa mashindano
hayo ambapo amesema kuwa lengo la
mashindano hayo ni kuimarisha afya za wafanyakazi,kubadilishana uzoefu pamoja
na kutangaza Taasisi zao.
“Kuna hili suala la
Wachezaji ambao sio wafanyakazi maarufu kwa jina la MAMLUKI kushiriki karika
michezo hii,tena nakumbuka kuna kiongozi aliwahi kuwaita “viongeza nguvu
bambikizi”,Hapa sio mahala pao nawataka wajiondoe mapema maana tukiwabaini wao
pamoja na Taasisi zao tutawachukila hatua”alisema Waziri Mwakyembe
Mhe.Waziri Mwakyembe
ameongeza kuwa wakati mwaka jana mashindano hayo yalipofanyika Jijini Dodoma Mhe.Makamu wa Rais Mama Samia hakuridhishwa na
idadi ya washiriki kutokana na Idadi ya Makampuni na Mashirika yaliyopo nchini,hivyo
kuagiza mkutano ufanyike kujua sababu na kuzipatia majibu ambapo maazimio yameleta matunda kwani mashindano ya
mwaka huu idadi imeongezeka kutoka 26 hadi
46.
Hata hivyo Mhe.Waziri
amewataka waamuzi wa mashindano hayo
kuchezesha michezo hiyo kwa haki na kufuata sheria zote za michezo na atakayesababisha vurugu au masononeko
atawajibishwa kupitia kiapo alichoapa leo.
Kwa upande wake
Mwenyekiti wa SHIMMUTA Bw.Khamis Mkanachi amesema kuwa Menejimenti za Taasisi
za Umma pamoja na Makampuni binafsi zinatakiwa kuelewa kwamba wafanyakazi wao
wanatakiwa kufanya michezo mbalimbali ili kuimarisha afya zao kwa ajili ya
kuongeza ufanisi wanapokuwa kazini,hivyo ni wajibu wa kila Taasisi na mashirika
kuona haja ya kutenga siku ya kufanya
michezo.
“Michezo hii
inafanyika kwa mwaka mara moja ni vyema viongozi wa Taasisi na Mashirika
binafsi kuona umuhimu huo na kuwapa wafanyakazi wao muda wa kushiriki michezo
hiyo inayoleta ari katika kufanya kazi” aliongeza Bw.Mkanachi.
Naye Mkuu wa Wilaya
ya Nyamagana Dkt.Fillis Nyimbi amesema Jiji la Mwanza hususan Wilaya ya
nyamagana imeshukuru ujio wa mashindano hayo kwakua itaongeza kipato kwa
wenyeji kutokana ongezeko la watu waliokuja kwa ajili ya mashindano hayo ambapo
pia amewahakikishia amani na usalama.
Vilevile mwanamichezo
Eliud Felix kutoka timu ya Jiji la Mwanza amesema michezo hiyo imewasaidia
kujuana pamoja na kubadilishana uzoefu wa majukumu ya kila mmoja katika taasisi
yake na kupendekeza iendelee kufanyika kila mwaka.
Mashindano hayo
yalianza rasmi tarehe 27/11/2019 na yanatarajiwa kumalizika Desemba mosi 2019
ambapo jumla ya Mashirika na Taasisi 46 zimeshiriki ikiwemo wenyeji Ofisi ya
Mkoa wa Mwanza,Chuo Kikuu Dodoma,Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro na nyingine.
No comments:
Post a Comment