|
TUME YA
HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
Kitalu
Na. 339, Mtaa wa Nyerere - Kilimani
S.L.P
1049, DODOMA
Simu:
+255 22 2135747/8; 2137125; 2135222
Faksi:
+255 22 2111281
Barua
Pepe: info@chragg.go.tz
Tovuti:
www.chragg.go.tz
|
Desemba 16, 2019
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Pongezi kwa Mheshimiwa Rais Dkt. John Magufuli kwa
uamuzi wake wa kutoa msamaha kwa wafungwa zaidi ya 5000.
Itakumbukwa kuwa Desemba, 9, 2019 katika Sherehe za
Maadhimisho ya Miaka 58 ya Uhuru, Mheshimiwa
Rais John Magufuli alitangaza msamaha na kuwaachia huru wafungwa 5,533.
Uamuzi huo wa Rais wa kuwasamehe wafungwa alioutoa wakati
akihutubia wananchi kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, jijini Mwanza umekuwa
ukitekelezwa na wakuu wa nchi tangu tupate uhuru mwaka 1961. Hata hivyo, uamuzi
wa Rais kuwasamehe wafungwa 5533 ni wa kipekee tangu Tanzania ipate uhuru
kutokana na idadi kubwa ya wafungwa aliowasehe.
Kufuatia uamuzi huo, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala
Bora (THBUB) inampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake huo uliojaa
upendo kwa wananchi anaowaongoza.
Tume inachukulia uamuzi huo wa Rais kama jambo ambalo linaweka nguvu na mkazo
katika sehemu ya majukumu yake ya kuhakikisha
haki za binadamu zinafurahiwa na watu wote ikiwemo wale walio
magerezani.
Aidha, Tume imefurahishwa na kauli aliyoitoa Mhe. Rais
katika maadhimisho hayo kuhusu kusikitishwa kwake na hali ya magereza, kwani
kauli hiyo inaonesha dhamira ya dhati aliyonayo yeye binafsi na serikali yake
katika kulinda na kuhifadhi haki za Wafungwa na Mahabusu katika magereza hapa
nchini.
Moja ya Jukumu la Tume kwa mujibu wa ibara 130 (1) ya
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Kifungu cha 6 (1) cha sheria ya
Tume ni kutembelea magereza ili kuangalia uhifadhi wa haki za binadamu katika
sehemu hizo na kutoa mapendekezo yanayofaa katika kuimarisha na kuboresha
mazingira ya magereza yetu.
Tume imekuwa ikifanya ziara za mara kwa mara katika
Magereza mbali mbali kwa lengo la kutekeleza jukumu hilo. Katika ziara zake
Tume imekuwa ikigundua changamoto kadhaa zinazowakabili wafungwa na mahabusu
zikiwemo mlundikano wa wafungwa na mahabusu, na kesi zao kuchukua muda mrefu kumalizika.
Tume imekuwa ikitoa mapendekezo kwa taasisi husika kurekebisha hali hiyo.
Kwa kauli hiyo ya Mhe. Rais, Tume inaamini kuwa
taasisi zenye dhamana ya kuhifadhi wafungwa na mahabusu wataongeza kasi katika
kulinda na kuhifadhi haki za makundi hayo.
Tume inaamini pia,
kauli hiyo itazifanya taasisi zenye dhamana ya upelelezi kufanya kazi hiyo kwa
haraka ili kupunguza muda wa mahabusu kukaa magerezani kwa muda mrefu. Kwa
upande mwingine Mahakama na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka hazina budi
kuongeza juhudi katika kusikiliza na kumaliza kesi za jinai kwa haraka ili
kupunguza muda wa mahabusu kukaa magerezani .
Tume inaziomba taasisi zote zenye dhamana ya usimamizi
wa jinai kuichukulia kauli hiyo kama ni chachu katika utekelezaji wa majukumu
yao hasa ya kulinda na kuhifadhi haki za wafungwa na mahabusu magerezani.
Mwisho, Tume inatoa ushauri kwa jamii na wanufaika wa
msamaha wa Mhe. Rais kama ifuatavyo;
1.
Wafungwa wote walionufaika na msamaha huo,
watumie mafunzo waliyoyapata wakiwa gerezani kushirikiana na Watanzania wenzao
kuisaidia Tanzania kufikia malengo yake ya kuwa nchi ya viwanda.
2.
Wanufaika
wa msamaha huo wakayatumie vyema mafunzo na maarifa waliyoyapata kufanya kazi
za uzalishaji mali na kujipatia kipato; kwani tume inaamini wakifanya hivyo
ndio njia pekee ya kumpa faraja Mhe. Rais
kwa uamuzi wake.
3.
Tume
inawasihi Watanzania wote kuwapokea ndugu zao hawa kwa mtazamo chanya na
kushirikiana nao katika kazi za ujenzi wa taifa, kwani kinyume na hapo,
wakiwatenga itawajengea picha ya kuona wananyanyapaliwa na hivyo kupelekea uwezekano wa kurudia makosa
yatakayowarudisha tena gerezani.
Jaji
Mstaafu, Mathew Pauwa Mhina Mwaimu
Mwenyekiti
Desemba 16, 2019
No comments:
Post a Comment