Habari za Punde

Taasisi za Uchukuzi zipange bajeti ya michezo



  • Makamu Mwenyekiti wa Klabu ya Uchukuzi, Hassan Hemed (wa pili kulia) jana akimkabidhi Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi), Gabriel Migire (wapili kushoto) moja ya vikombe 14 vya ushindi wa mashindano ya Mei Mosi yaliyofanyika Mei 2019 mkoani Mbeya. Katikati ni Katibu Mkuu wa klabu hiyo Mbura Tenga.   



    Na MwandishiWetu
    TAASISI zilizopo katika Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano zimetakiwa kupanga bajeti ya michezo katika bajeti zao za mwaka ili kuhakikisha wanashiriki vizuri katika michezo, imeelezwa.
    Hayo yalisemwa jana na Kaimu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Sekta ya Uchukuzi,  Gabriel Migire baada ya kukabidhiwa vikombe vya ushindi wa Mashindano ya  Mei Mosi  2019 kutoka kwa Makamu Mwenyekiti wa Uchukuzi Sports Klabu (USC),  Hassan Hemed.
    Akijibu changamoto zilizotolewa na Katibu Mkuu wa Uchukuzi  Sports  Club,  Mbura Tenga,  ambaye katika risala yake ya utangulizi alieleza moja ya changamoto zinazowakabili ni kwa baadhi ya taasisi kushindwa kutenga fedha kwa ajili ya michezo.
    Tenga alisema kuwa hilo  la kushindwa kutenga fedha linatokana na taasisi hizo kutokuwa na bajeti kabisa ya michezo na wengi wa maofisa rasilimali watu wake kutojua kabisa umuhimu wa michezo na kuona kama ni kupoteza muda na fedha tu.
    Migire alisema kuwa taasisi nazo zinatakiwa kuiweka michezo katika bajeti za idara zao za kila mwaka ili kuhakikisha wachezaji wao wanashiriki na kutoa wachezaji katika Uchukuzi  Sports  Club.
    Migire pia aliipongeza Uchukuzi  Sport  Klabu kwa kutwaa ubingwa wa jumla kwa mara ya pili mfululizo katika Mashindano ya  Mei Mosi,  baada  ya  mwaka huu kutwaa jumla ya vikombe tisa,  vinne vikiwa katika nafasi ya  kwanza, ambavyo ni Kuvuta Kamba kwa Wanaume na Wanawake na Baiskeli kwa Wanauame na Wanawake.
    Uchukuzi  Sports  Klabu katika Mashindano ya  Mei  Mosi mwaka huu yaliyofanyika Mbeya,  walitwaa vikombe tisa kati ya  14, ambavyo hushindaniwa kila mwaka.
     Uchukuzi pia ndio klabu pekee katika mashindano hayo kupeleka timu za michezo yote  14  ya mashindano hayo, tofauti na wizara zingine, ambazo wakati mwingine hupeleka timu au mchezaji mmoja.
    Akijibu kuhusu timu ya Uchukuzi mara mbili kualikwa  Zanzibar  (Unguja na Pemba) na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ya Zanzibar (ZAA) na kufanya utalii wa ndani,  alisema hilo ni suala ni muhimu sana,  hasa ukizingatia linahusu Muungano,  ambapo liwataka kupanga utaratibu kuona USC wanafanyaje ili kuwaalika Bara  Wazanzibari.


    Pia alisema changamoto ya kutokuwa na ofisi inayoikabili  USC linaweza kushughulikiwa,  hasa ukizingatia kuwa Katiba ya USC  inaeleza kuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo,  lazima atoke wizarani,  hivyo itakuwa rahisi kuwepo kwa ofisi wizarani kwa ajili ya klabu yao.
    Akielezea kuhusu ushindi huo wa jumla, alisema kuwa ni mkubwa sana,  hivyo hauwezi kupita kimyakimya, kwani lazima na wakubwa nao wajue nini kimeletwa na USC,  hivyo hafla hiyo itaandaliwa tena kwa ukubwa wake.
    Aidha,  Tenga alisema wanatarajia Februari 7, 2020 kufanya Mkutano mkuu kwa ajili ya mabadiliko ya Katiba pamoja na kuchagua viongozi wapya,  ambapo kila taasisi inakuwa na mwakilishi katika klabu hiyo, tofauti na sasa ambapo taasisi moja inaweza kuwa na zaidi ya mjumbe mmoja na nyingine isiwe nayo kabisa.

    No comments:

    Post a Comment

    ZanziNews Copyright © 2014

    Theme images by Bim. Powered by Blogger.