Habari za Punde

WAZIRI KAIRUKI AIPONGEZA TIRDO KUSAIDIA WAWEKEZAJI WADOGO


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kairuki akitazama bidhaa ya nyama iliyochakatwa na kuwa soseji inayozalishwa na Kiwanda cha ORI Meat Product Ltd kilichopo Jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kutembelea kiwanda hicho leo Jumatano (Desemba 18, 2019) na kujionea uzalishaji. Kushoto ni Mfanyakazi wa Kiwanda hicho, Martha Gwali.


 Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji), Angellah Kariuki akizungumza jambo na Viongozi wa Kiwanda cha ORI Meta Product Ltd kinachochakata bidhaa ya nyama na kuwa soseji wakati alipofanya ziara yake katika Kiwanda hicho leo Jumatano (Desemba 18, 2019). Kushoto ni Meneja Uzalishaji wa Kiwanda hicho, Mitesh Dhokie na katikati ni Mkurugenzi Mtendaji, Goodluck Hussein. 

(PICHA NA MAELEZO) 


Na Mwandishi Wetu,MAELEZO DAR ES SALAAM 18.12.2019
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji) Angellah Kairuki amelipongeza Shirika la Utafiti wa Maendeleo ya Viwanda Tanzania (TIRDO) kwa kuweka msukumo na mkakati endelevu wa kuwaendeleza na kuwasaidia wafanyabiashara na wawekezaji wadogo nchini.
Akizungumza na Uongozi na Wafanyakazi  wa Kiwanda cha kuchakata nyama cha ORI Meat Product Ltd leo Jumatano (Desemba 18, 2019), Waziri Kairuki alisema TIRDO imeendelea kutekeleza vyema majukumu kupitia shabaha iliyowekwa na  Serikali ya Awamu ya Tano katika ujenzi wa viwanda  unaochochea katika kukuza mnyororo wa thamani  na kuleta tija iliyokusudiwa.
Aliongeza kuwa msukumo uliowekwa na Wizara ya Viwanda na Biashara pamoja Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji) ni kuhakikisha kuwa wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo wanakuwa na fursa kuwa katika kukuza uchumi kwa kuwawezesha kujenga viwanda vidogo vidogo na kuchakata bidhaa zenye ubora.
‘’Niwapongeze TIRDO kwa kutambua wajibu wenu katika masuala ya utafiti na viwanda lakini pia kutoa eneo lenu lenye ukubwa square (mraba) mita  600-700 na ghorofa moja na kukodisha kwa kiwanda cha ORI na kwa msukumo huu tutaweza kuwasaidia wajasiriamali, wafanyabiashara na wenye viwanda vidogo kuweza kufikia malengo yaliyokusudiwa’’ alisema Waziri Kairuki.
Aidha Waziri Kairuki aliitaka TIRDO kuhakikisha kuwa mpango huo unakuwa endelevu ili kuwafanya wafanyabiashara, wawekezaji na wajasiriamali wadogo wanaendelea kupata maeneo makubwa zaidi kupitia miradi yake hatua itakayowawezesha kuweza kuongeza mnyororo wa thamani ya uzalishaji na hivyo kuleta tija kwa taifa.
Waziri Kairuki pia aliipongeza Kampuni ya ORI Meat Product Ltd kutokana na juhudi na ubunifu mkubwa walioufanya katika kuchakata bidhaa za nyama kupitia soseji za ng’ombe na kuku, na kuongeza kuwa Ofisi yake itawasiliana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili kuona namna bora mauzo na uzalishaji wa bidhaa za kampuni hiyo.
‘’Ndani ya muda mfupi wa kipindi cha mwaka mmoja vijana hawa wa Kitanzania wameweza kuwekeza mtaji wa Tsh Bilioni 1.1, walianza na wafanyakazi 50 lakini sasa wapo 64 lakini pia wameweza kuongeza mnyororo wa thamani kupitia label (alama), vifungashio vya plastiki, wazalishaji wa kuku ambapo wajasiriamali wanaweza kuuza kuku katika kiwanda hiki’’ alisema Waziri Kairuki.
Akifafanua zaidi Waziri Kairuki aliitaka Kampuni hiyo kuendelea kupanua shughuli zake ikiwemo kuimarisha mtandao wa masoko ya ndani na nje ya nchi, ikiwemo soko la Nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC), Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) pamoja na kuzalisha bidhaa zenye viwango na ubora unaostahiki.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TIRDO, Humphery Ndossi Ofisi yake imeendelea kufanya kazi na wawekezaji wa ndani kwa kuweka mazingira wezeshi ya kufanya biashara zao, na miongoni mwao ni Kiwanda cha ORI Meat ambapo wamekuwa wakitoa msaada mbalimbali ikiwemo upimaji wa ubora wa bidhaa za kiwanda hicho.
Aliongeza kuwa TIRDO imeendelea kusimamia wajibu wa msingi wa majukumu yake kwa kuwasisitiza wafanyabiashara kuzingatia ubora wa bidhaa mbalimbali zinazozalishwa nchini ili kuweza kuliepusha taifa na mlundikano wa bidhaa bandia na zisizo na ubora na kuzuia matumizi yake ili kulinda afya za  wananchi.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa ORI Meat Product Ltd, Goodluck Hussein alisema Ofisi yake imeendelea kupata ushirikiano mkubwa kutoka kwa Serikali na imeweza kuuza pakiti 1200-1500 kwa mwaka, jambo ambalo lilikuwa gumu kwa miaka ya nyuma kutokana na uwepo wa bidhaa nyingi za nyama kutoka nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.