Habari za Punde

Waziri wa Afya Maendeleo ya Jinsi Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalim Azindua Bodi ya Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akikata utepe kuashirika kuzindua Bodi ya Pili ya Uendeshaji wa Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru leo mkoani Arusha kushoto ni Katibu Mkuu Idara Kuu ya Maendeleo ya Jmaii Dkt. John Jingu na Kulia ni Mwenyekiti wa Bodi hiyo Dkt. Rose Mwaipopo.
Na Mwandishi Wetu Arusha
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu ameizindua Bodi ya pili ya uendeshaji wa Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru na kuitaka kuleta chachu ya mabadiliko katika Sekta ya Maendeleo ya Jamii nchini.
Waziri Ummy ameyasema hayo leo Mkoani Arusha wakati akizungumza na wajumbe wa Bodi hiyo ambayo ina jukumu ya kuratibu na kusimamaia shughuli zinazofanyawa na Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru.
Waziri Ummy amewataka wajumbe wa Bodi hiyo kuisaidia Serikali katika kuhakikisha Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru inaleta matokeo chanya kwa jamii hasa inayowazunguka na kuhakikisha itakuwa kituo cha mfano cha Taaluma ya Kada ya Maendeleo ya Jamii nchini.
Ameitaka Taasisi hiyo kuzingatia mafunzo kwa vitendo kwa kuongeza uhusiano mzuri kati ya nadharia na vitendo katika mitala iliyopo na kuweka mkazo katika kuhakikisha mafunzo wanayoyatoa yanawasaidia wahitimu kuwa na nandhari ya kujiajiri zaidi kuliko kuajiriwa.
Pia ameitaka Bodi hiyo kuweka mkazo katika kutatua changamoto za ajira kwa kuhakikisha inawapa wanafunzi stadi za kuwawezesha kujiajiri na kutengeneza ajira kwa wengine kupitia fani walizosoma hasa fani ya Maendeelo ya Jamii.
“Niwatake mjenge ushirikiano kati ya Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru na Taasisi zingine ili wahitimu waweze kujitolea na wengine kuweza kupata ajira katika Taasisi hizo hasa Mashriika Yasiyo ya Kiserikali” alisema Waziri Ummy
Waziri Ummy ameongeza kuwa Taasisi hiyo ina umuhimu katika jamii hivyo kuitaka kutoa mchango katika jamii katika utatuzi wa changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii inayoizunguka Taasisi hiyo ili kupata jawabu za changamoto hizo.
Aidha Waziri Ummy ameitaka Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru kuhakikisha wanachangia katika mfuko wa Serikali kwa kutekeleza agizo la Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli ya kila Taasisi ya Serikali kuchangia katika mfuko wa Serikali ndani ya siku 60.
“Agizo hili msije mkasema sisi hatuzalishi faida mnatakiwa kutoa mchango wenu kama Taasisi ya Serikali katika mfuko wa Serikali ambao ni muhimu kwani ndio unasaidia kutoa huduma muhimu kwa wananchi” alisema Waziri Ummy
Kwa upande wake Katibu Mkuu Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu amesema kuwa Bodi iliyopita iliweza kuandaa programu mbalimbali za mafunzo, walifanya maandalizi Sera 13 za usimamizi wa Taasisi mbalimbali  waliwezesha kuongozeka kwa udahili wa wanafunzi   276 kwa mwaka wa masomo 2014/2015 mpaka 1204 kwa mwaka 2018/2019 na kufanikisha ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya kujifunzia.
Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru Dkt. Rose Mwaipopo amesema Bodi hiyo inafanya majukumu yake kwa mujibu wa Sheria na kuzingatia umuhimu wa kada ya Maendeleo ya Jamii katika kuchochea maendeleo ya nchi.
“Tunatazamia kuleta chachu katika Sekta ya Maendeleo ya Jamii hasa katika kuleta mapinduzi ya kifkra kwa wananchi katika kujiletea maendeleo yao wenyewe” alisema Dkt. Rose.
Bodi ya pili ya Uendeshaji wa Taasisi ya Maendeleo ya Jamii Tengeru imezinduliwa ikiongozwa na Mwenyekiti wake Dkt. Rose Mwaipopo na itahudumu kwa muda wa miaka mitatu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.