Habari za Punde

Maafisa Michezo wa Mikoa na Halmashauri waagizwa kubadilika kiutendaji

Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe akizungumza na wadau wa michezo wa Jiji la Arusha alipokua katika ziara ya kujadili maendeleo ya sekta hiyo pamoja na kutatua changamoto wanazokutana nazo wadau hao iliyofanyika Januari 25,2020.Kulia ni Katibu tawala Wilaya ya Arusha mjini Bw.Davis Mwaiposa.
Na Shamimu Nyaki – WHUSM Arusha
Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe amewaagiza maafisa michezo wote chini kubadilika katika utendaji wao kutokana na kulalamikiwa na wadau wengi wa michezo namna ambavyo wanashughulikia sekta hiyo
Waziri Mwakyembe ametoa agizo hilo jana Jijini Arusha alipokutana na wadau wa michezo kujadili maendeleo ya sekta hiyo ambapo amewataka maafisa michezo kuhakikisha masuala ya michezo katika maeneo yao hayakwami kutokana na wao kutowajibika.

“Nyinyi ni watumishi wa Serikali mnaposhindwa kutatua kero za wanamichezo na kusimamia sekta hii basi nyie hamtoshi na mimi sitawavumilia kuona mnakwamisha maendeleo ya michezo nchini”alisema Dkt.Mwakyembe.

Aidha Mhe.Waziri ameliagiza Baraza la Michezo la Taifa (BMT) ifikapo Februari mosi 2020,liwe limewasilisha mapendekezo ya mabadilio ya Katiba ya Chama cha Riadha nchini ili kupata muongozo wa mchezo huo.

Mhe.Waziri ameongeza kuwa Serikali imerudisha michezo ya UMITASHUMTA na UMISETA ili kuhakikisha sekta hii inaendelea kukua na kuletea heshima taifa, huku akieleza kuwa Serikali inadhamiria kutofautisha viwanja vya sanaa na vya michezo kwasabu sekta hizi zina wadau wengi ambao wamekuwa na matukio yanayofanana na  yanayofanyika kwa wakati unaofanana hivyo ni vyema kila sekta ikajitegema katika maonyesho yake.

Vile vile Dkt.Mwakyembe amevitaka vilabu vya michezo na mashirikisho kuona umuhimu wa kutumia wanamichezo wa ndani ili kuinua vipaji walivyonavyo lakini pia kuwapatia ajira kuliko kusajili wachezaji wa nje wengi na kuwaacha wazalendo.

Kwa upande wake Afisa Michezo wa Mkoa Bibi  Mwamvita Okeng’o amesema kuwa Mkoa wa Arusha unaendelea kufanya vizuri katika michezo na unaendelea kukuza sekta hiyo kwa kuongeza idadi ya viwanja na tayari mipango imeanza ya kujenga uwanja kila Wilaya ya mkoa huo.

Katika hatua nyingine Makamu Mwenyekiti wa Shirikisho la Riadha Bw.Wiliam Kalaghe amesema kuwa maandalizi ya wanamichezo Alphonce Simbu na Failuna Abdu ambao wataliwakilisha Taifa mwaka huu katika mashindano ya Olympiki  huko Japan yanaendelea vizuri  na tayari shirikisho hilo limetoa kiasi cha Sh. Milioni 03 kama chagizo la maandalizi  hivyo watanzania wanapaswa kuwaunga mkono.


Naye Bw.Hamis mdau wa mchezo wa mpira wa miguu ameshauri wanamichezo kujifunza lugha na namna bora ya kufanya mahojiano ili wanapokuwa wamepata nafasi ya kucheza soka nje wasikwame kwa kigezo cha kushindwa kujibu maswali au kutumia lugha Fulani.
Baadhi ya wadau wa Michezo  wa mkoa wa Arusha wakitoa maoni yao wakati wa kikao cha Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe na wadau hao   kujadili maendeleo ya sekta hiyo pamoja na kutatua changamoto wanazokutana nazo iliyofanyika 

Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Mkoa wa Arusha pamoja na wadau wa michezo mkoa huo mara baada ya kumaliza mkutano wa  kujadili maendeleo ya sekta hiyo pamoja na kutatua changamoto wanazokutana nazo wadau hao uliofanyika Januari 25,2020.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.