Mwakilishi wa Katibu
Tawala wa Mkoa wa Kigoma Bi. Savera Salvatory akifungua
kikao kazi cha wadau wa maendeleo ya Wanawake na Jinsia waliokutana na Wizara
kujadili na kutoa maoni ya kuhuisha Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia kwa
mikoa ya Kanda ya Magharibi mkoani Kigoma.
Na Mwandishi Wetu Kigoma
Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia ya mwaka 2000 pamoja na mapungufu
ya kutekelezwa kwa muda mrefu kabla ya kuhuishwa bado imeonesha mafanikio katika
kukuza ushirikishi wa wanaume, kukuza uelewa wa masuala ya wanawake na kuhimiza
uzingatiaji wa jinsia katika mipango ya kisekta.
Hayo yameelezwa na Mtaalam Mwelekezi Bi. Linah Mhando wakati
akitambulisha zoezi la ukusanyaji wa maoni ya uboreshajai wa Sera ya Maendeleo
ya Wanawake na Jinsia ya Mwaka 2000 na Mkakati wa utekelezaji wake (2005) ili kuhuisha
Sera iliyopo katika kuzingatia malengo ya mikataba ya kimataifa, Dira ya
Maendeleo ya Taifa ya 2025, Mpango wa pili wa Taifa wa Maendeleo wa miaka
mitano na mahitaji ya kijinsia.
“Sera ya Maendeleo ya Jinsia na Wanawake pamoja na mapungufu yake imeonesha
mafanikio katika eneo la ushiriki wa wanaume,imesaidia kukuza uelewa kuhusu masuala
ya wanawake, kuanzishwa kwa mifumo wezeshi, kuwa na mipango inayozingatia
jinsia, kuimarisha upatikanaji wa elimu, huduma ya miundombinu na uwezeshaji wa
kiuchumi”. Alisema Bi. Linda.
Mwakilishi wa Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma Bi. Savera Salvatory amefungua
kikao cha Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ambacho kinawashirikisha
wadau kutoka Kanda ya Magharibi
inayojumuisha mkoa wa Rukwa, Katavi na Kigoma ambao wamekutana kutoa maoni yao
ili kuhakikisha Sera inaingiza masuala muhimu yanayochochea kasi ya maendeleo hapa
nchini na duniani kote.
Bi. Savera amewataka wadau wanaoshiriki mapitio ya sera mpya kupendekeza
mikakati mipya ya kusaidia kufikia usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa
wanawake.
Ameongeza kuwa kutokana na mapendekezo ya wadau Wizara imezingatia
kufanya tathmini ya kina inayozingatia masuala yote muhimu yanayopendekezwa na
kuendelea kuimarisha mengine yaliyopo ambayo yanakidhi vipaumbele vya kijinsia.
Zoezi hili linafanyika kwa kuhusisha wadau, taasisi na makundi mbalimbali
katika jamii ili kuhakikisha kuwa hakuna anayeaachwa nyuma.
Mkutano wa tano unaofanyika Kanda ya Magharibi katika mkoa wa Kigoma ulitanguliwa
na Mkutano wa Kanda ya Ziwa, Kanda ya Kati, Kanda ya Kasikazini na Kanda ya
Mashariki. Mikutano hii shirikishi ilianza mwezi Septemba 2019 naitaendelea
hadi Februari 2020 kwa ajili ya kuwapa fursa wadau kutoa maoni yao katika kuzingatia
usawa wa jinsia na uwezeshaji wanawake.
Bi Severa amesema kuwa maoni yanayokusanywa kutoka kwa washiriki yatawezesha
Wataalam waelekezi pamoja na wawikilishi wa Wizara kutoa taarifa kuhusu tathmini
ya jumla ya zoezi la ukusanyaji maoni ya wadau kuhusu mafanikio na changamoto ya
sera kwa kipindi cha utekelezaji wake ili kuboresha sera iliyopo.
Mkurugenzi Msaidizi wa Maendeleo ya Jinsia Bi. Grace Mwangwa amesema kuwa
Serikali inahitaji Sera ya Jinsia iliyoboreshwa ambayo inazingatia masuala
jumuishi ikiwa ni pamoja na teknolojia, mabadiliko ya tabia nchi, elimu, ajira
na masuala mengine ili kuingizwa kwenye matamko ya kisera. Wadau mbalimbali
watafikiwa ili kupata wigo mpana wa ukusanyaji maoni kutoka kwa wadau wa
makundi mbalimbali.
“zoezi la kuboresha sera ya maendeleo ya wanawake na jinsia ni shirikishi
na tunaamini kuwa michango ya wadau itawezesha kupata mapendekezo stahiki kwa
ajili ya kuboresha sera iliyopo”. Alisema Bi. Grace.
Bi. Grace amesema kuwa Wizara imetuma wataalam katika ngazi ya jamii ili
kupata maoni yao kuhusu maeneo ya vipaumbele katika kushughulikia matatizo, changamoto
zilizopo na mapendekezo ya kisera katika kuhuisha sera inayofanyiwa mapitio ili
kukidhi usawa wa kijinsia.
Naye Afisa Maendeleo ya Jamii kutoka mkoa wa Rukwa Bi.Aziza Kalyatila
amesema kuwa Sera inayoandaliwa itaondoa pengo la unyanyapaa kwa wanaume na wanawake
na kuwajumuisha katika mahudhui na maelekezo ya kisera ili kwenda sambamba na juhudi
za Serikali za kupeleka maendeleo kwa makundi yote jambo ambalo litasaidia
kuondokana na ukatili katika jamii.
Kwa upande wake Meneja Biashara kutoka CRDB Bank mkoa wa Kigoma Bw. Erick
Mgalla amesema kuwa wanawake wanakabiliwa na changamoto kubwa ya kupata mikopo
katika taasisi za kifedha maana wanawake wameachwa nyuma katika huduma za
kifedha. Amesisitiza kuwa Sera hii inapoandaliwa isaidie kuondoa vikwazo vya
upatikanaji wa mikopo na huduma ya biashara kwa wanawake ili kutoa fursa sawa
kwa wanawake na wanaume.
“Kwa kiasi kikubwa wanawake wameachwa nyuma bila kupata huduma za
kibiashara kutoka taasisi za fedha. Kwa mfano masoko 254 yaliyoko katika mji wa
Kigoma- Ujiji kiasi cha asilimia 90 ya wafanyabiashara walioko katika masoko
hayo ni wanawake hata hivyo kundi hili la wanawake linachangamoto ya kukosa
dhamana ya kuaminiwa na kupata mikopo na huduma nyingine za kibiashara”.
Alisema Bw. Erick.
Ameongeza kuwa Sera ya jinsia inayoboreshwa ijikite kuwanufaisha pia
wanawake ili kuweza kupata dhamana ya kumiliki ardhi na kuwezeshwa kufungua
akaunti kwa kupewa haki ya umiliki wa mali kwa mujibu wa sheria.
Mapitio ya sera
yanayofanyika hivi sasa yanatoa vipaumbele katika maeneo mapya ikiwa ni pamoja
na jinsia na maendeleo ya mji/vijiji, jinsia na
haki za umiliki ardhi, jinsia, maji na mazingira, haki za mtoto wa kike, jinsia
na ulemavu, ukatili wa kijinsia, jinsia, sayansi ,teknolojia na ufumbuzi ,
jinsia, afya uzazi na ukimwi, jinsia, uongozi na maamuzi, jinsia, ajira na
kazi, jinsia, sheria na haki za binadamu na jinsia na hifadhi ya jamii.
Maeneo mengine yatakayoangaziwa ni jinsia na
kuwawezesha wanawake kiuchumi, jinsia na ujumuishwaji wa kifedha, jinsia na
mabadiliko ya tabianchi, jinsia na nishati, jinsia na miundombinu, jinsia na
takwimu, jinsia na madini, jinsia na vyombo vya habari na mawasiliano, jinsia
na mila na desturi, jinsia na jamii za ufugaji, ufadhili na jinsia na jinsia na
uvuvi.
Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na
Watoto ipo katika machakato wa kukusanya maoni ya wadau kutoka katika mikoa 26
ya Tanzania Bara ili kuboresha Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia ya Mwaka
2000 kwa ajili ya kuwezesha kufikia upatikanaji wa maendeleo jumuishi kwa
kuzingatia haki na usawa wa kijinsia.
Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Maendeleo ya
Jinsia kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bi.
Grace Mwangwa akitao neno la utangulizi
wakati wa kikao kazi cha wadau waliokutana kutoa maoni ya kuboresha Sera
ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia katika mikoa ya Kanda ya Magharibi mkoani
kigoma.
Mtaalam Mwelekezi Bi. Linah
Mhando akifafanua hoja kwa wadau wa Kanda ya Magharibi walioshiriki zoezi la
kukusanya maoni kuhusu uboreshajai wa Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia katika
ili Sera hiyo wakati wa kikao kilichofanyika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa
Kigoma.
Baadhi ya washiriki wa kikao cha wadau cha
kuibua maoni maalum ya kuboresha Sera ya Maendeleo ya Wanawake na jinsia wakifuatilia
kwa makini nasaha za Mgeni Rasmi wakati wa ufunguzi wa kikao cha wadau hao
katika Kanda ya Magharibi Mkoani Kigoma.
Baadhi ya wadau wa
maendeleo ya jinsia kutoka Kanda ya Magharibi wakiwa katika vikundi kazi vya
kuibua maoni ya uboreshaji wa Sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia katika
kikao kilichofanyika ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Kigoma.
No comments:
Post a Comment