Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na
Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akifungua mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa
Ofisi hiyo kilichofanyika jijini Dodoma leo ambapo aliwataka kuwajibika
ipasavyo mahali pa kazi.
Waziri
wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu amemtaka
kila mtumishi katika Ofisi hiyo kuwajibika ipasavyo mahali pa kazi na kuepuka
kujihusisha na vitendo visivyokuwa vya kimaadili.
Zungu ametoa kauli
hiyo leo jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa
Ofisi hiyo ambapo aliwakumbusha kuwa Serikali ya awamu ya tano imedhamiria kwa
dhati kuimarisha utendaji kazi ili kufanikisha dhana ya Tanzania ya viwanda.
“Ninafahamu kwamba watumishi wana malalamiko yanayohusu kutopandishwa vyeo kwa muda mrefu na upungufu wa watumishi katika Idara na Vitengo, malalamiko haya ni mtambuka katika Wizara zote kwani yametokana na uhakiki wa vyeti vya elimu ya sekondari na ualimu zoezi lililoendeshwa na Serikali kuanzia mwaka 2016. Ninawasihi muwe na subira wakati Serikali ikiimarisha mifumo yake ya Usimamizi wa Rasilimaliwatu,” alisisitiza.
Aidha, Waziri Zungu alibainisha kuwa Baraza la wafanyakazi ni jukwaa muhimu mahali pa kazi kwani ni kiunganishi kati ya Menejimenti na Wafanyakazi hivyo aliwataka kuendeleza ushirikiano ili kuleta ufanisi katika kutekeleza majukumu ya Ofisi na Taifakwa ujumla.
“Watumishi wenzangu
hakikisheni mshahara mnaopewa mnautendea haki! Msitake kupata mshahara wa bure!
Fanyeni kazi kwa bidii” Zungu alisisitiza.
Aliongeza kuwa kuwepo kwa Mabaraza ya Wafanyakazi katika Taasisi ni takwa la Kisheria kwa madhumuni ya kuishauri Serikali katika ngazi za Idara na Ofisi ambapo malengo yake ni kuhakikisha kuwa majukumu yanatekelezwa ipasavyo, kulinda haki na wajibu wa waajiri na wafanyakazi, kutoa ushauri kuhusu kujenga mazingira bora ya kazi, maslahi ya watumishi na kusimamia haki na ustawi katika sehemu za kazi.
Aliwakumbusha kuwa wajibu wa Mabaraza haya kama vyombo vya ushauri na usimamizi ni kuhakikisha kuwa waajiri na watumishi wanatambua wajibu na haki zao na kuzingatia maadili ya utumishi wao ili kuleta matokeo chanya katika utendaji kazi.
Agenda na madhumuni
ya mkutano huu ni kutoa Taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya Ofisi ya Makamu
wa Rais kwa kipindi cha nusu mwaka cha utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2019/20.
Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Balozi Joseph Sokoine akimkaribisha
mgeni rasmi kwa ajili ya kufungua mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi
hiyo uliofanyika leo jijini Dodoma.
Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Watumishi la Ofisi ya
Makamu wa Rais wakiwa katika mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo
uliofanyika leo jijini Dodoma na kufunguliwa na Waziri Mussa Azzan Zungu.
Sehemu ya wajumbe wa Baraza la Watumishi la Ofisi ya
Makamu wa Rais wakiwa katika mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo
uliofanyika leo jijini Dodoma na kufunguliwa na Waziri Mussa Azzan Zungu.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na
Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa
Baraza la Wafanyakazi wa Ofisi hiyo baada ya kufungua mkutano leo jijini
Dodoma.
No comments:
Post a Comment