Waziri wa Nchi Ofisi
ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mussa Azzan Zungu hii leo
ametembelea eneo la Karakata Mji mpya kujionea changamoto za Mto Msimbazi,
katika ziara hiyo ameambatana na Mbunge wa Segerea Mhe. Bona Kamoli.
Na
Lulu Mussa. Dar
es Salaam
Waziri wa Nchi Ofisi ya
Makamu wa Rais Mhe. Mussa Zungu amesema katika
kipindi hiki cha miezi tisa (9) tangu Kanuni za Usimamizi wa Mazingira za
Kupiga marufuku mifuko ya Plastiki za mwaka 2019 zianze kutekelezwa, Serikali
imefanya jitihada za kutoa elimu kwa wadau mbalimbali, kuandaa viwango vya
ubora wa mifuko mbadala ya Non-woven, kufanya kaguzi katika maeneo ya
uzalishaji, usambaji na uuzaji wa mifuko mbadala.
Akifungua
kikao cha wadau katika ukumbi wa LAPF, Kijitonyama chenye
lengo la kukuza uelewa wa Sheria na
Utekelezaji wa Kanuni ya Katazo la Mifuko ya Plastiki kwa wazalishaji,
waingizaji, wasambazaji na wauzaji wa mifuko mbadala Jijjini Dar es Salaam,
Zungu ameainisha kuwa mifuko mbadala
inayoruhusiwa kisheria kutumika kubebea bidhaa hapa nchini ni lazima ikidhi matakwa
ya kisheria.
“Mwongozo umeainisha viwango vya ubora wa mifuko mbadala ya
“Non-woven” ni uzito usiopungua 70GSM; iwe inayoweza kurejelezwa (recyclable);
iwe na anuani ya mzalishaji au nembo ya biashara (trade mark); ionyeshe uwezo
wake wa kubeba (carrying capacity); na iwe imethibitishwa ubora wake na Shirika
la Viwango-TBS” Zungu alisisitiza.
Waziri Zungu amesema kuwa
hadi sasa tani 54 za mifuko aina ya non-Woven zimekamatwa na kusisitiza kuwa
hivi sasa adhabu kali zitatolewa ikiwa ni pamoja na faini, kufunga viwanda na
kusisitiza kuwa msako mkali unaanza kwa wazalishaji na wasambazaji wa mifuko
isiyokidhi viwango.
“Katika kipindi cha miezi tisa kuanzia
Juni, mosi 2019 shehena ya mifuko mbadala isiyokidhi viwango isiyopungua tani
54.035, katoni 12,767 na vipisi 11,191, 919 imekamatwa katika mikoa yote ya
Tanzania Bara wakati wa kaguzi na hatua stahiki kwa mujibu wa Sheria ya
Usimamizi wa Mazingira na Kanuni zake, zimechukuliwa kwa waliokutwa na makosa.
Hatutishani lakini tunatoa tahadhari! Wenye viwanda wanaoendelea kukaidi
wakikamatwa watashtakiwa kwa kuhujumu uchumi” Zungu alisisitiza.
Katika hatua nyingine,
Waziri Zungu amemuagiza Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na
Usimamizi wa Mazingira nchini (NEMC) kuitisha kikao cha wakurugenzi na
Wataalamu wa Mazingira katika Halmashauri zote nchini kuwakumbusha majukumu yao
ya kusimamia ipasavyo katazo la Mifuko ya Plastiki na kuendelea na utoaji wa elimu
kwa umma.
Naye Mkurugenzi wa Baraza la
Taifa la Hiifadhi na Usimamizi wa Mazingira Nchini Dk. Samuel Gwamaka amesema
Serikali imefanikiwa kusimamia katazo la Mifuko ya Plastiki ingawa kuna
changamoto ambazo Ofisi yake inazifanyia kazi kwa karibu.
Amesema kuwa changamoto
kubwa ni kutojitangaza kwa wafanyabiashara wa mifuko mbadala kwa kutumia vyombo
vya habari.
“Inakuwa vita hivi tunapiga
sisi wenyewe, tunaowapigania wao wamekaa pembeni, natoa wito kwa jamii
kushiriki kikamilifu, tunalinda mazingira kwa vizazi vijavyo, suala hili
linahitaji elimu endelevu na sisi tutaendelea kufanya hivyo” amesisitiza Dkt.
Gwamaka.
Dkt. Gwamaka amelipongeza
Jeshi la polisi Makao Makuu (Kitengo cha Mazingira) kwa mchango mkubwa wanaotoa
kwa Baraza ikiwa ni pamoja na kusimamia kikamilifu Katazo la Mifuko ya
Plastiki.
Dkt Gwamaka amesema kuwa
mpaka sasa Viwanda 72 vya kuzalisha mifuko mbadala vinafanya kazi hapa nchini
na kutoa ajira takriban 2761.
Kikao cha kukuza uelewa wa
Sheria na Utekelezaji wa Kanuni ya Katazo la Mifuko ya Plastiki kwa
Wazalishaji, waingizaji, wasambazaji na wauzaji wa Mifuko mbadala ya Plastiki
kimefanyika katika Ukumbi wa LAPF, Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Nchi Ofisi
ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mussa Azzan Zungu hii leo
ametembelea eneo la Karakata Mji mpya kujionea changamoto za Mto Msimbazi,
katika ziara hiyo ameambatana na Mbunge wa Segerea Mhe. Bona Kamoli.
Picha ikionyesha mmomonyoko
wa ardhi eneo la Karakata ambao Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais
(Muungano na Mazingira) ameelekeza wataalamu wa NEMC na Jiji la Dar es Salaam kushirikiana
na kupata ufumbuzi wa haraka.
Waziri wa Nchi Ofisi
ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mussa Azzan Zungu akiongea na wadau
katika kikao
cha kukuza uelewa wa Sheria na Utekelezaji wa Kanuni ya Katazo la Mifuko ya
Plastiki kwa Wazalishaji, waingizaji, wasambazaji na wauzaji wa Mifuko mbadala
ya Plastiki. Kikao hicho kimefanyika katika Ukumbi wa LAPF, Jijini Dar es
Salaam. Wengine katika picha (kushoto) Ni Mkurugenzi wa Baraza la Taifa la
Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Dkt. Samwel Gwamaka, Bi. Kemilembe
Mutasa Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mazingira na Bw. Jabir Abdi Kaimu
Mkurugenzi Mkuu Shirika la Viwango
Tanzania.
Bw. Mushtak Waliji
Mwenyekiti wa Chama cha Wazalishaji wa Plastiki nchini akichangia mada katika kikao
cha kukuza uelewa wa Sheria na Utekelezaji wa Kanuni ya Katazo la Mifuko ya
Plastiki kwa Wazalishaji, waingizaji, wasambazaji na wauzaji wa Mifuko mbadala
ya Plastiki. Kikao hicho kimefanyika katika Ukumbi wa LAPF, Jijini Dar es
Salaam.
No comments:
Post a Comment