Habari za Punde

Ushirikiano Serikali ya SMT na SMZ wazidi kupaa

Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara ya Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Bw.Petro Lyatuu akizungumza katika kikao cha kujadili maeneo ya ushirikiano baina ya Serikali ya SMT na SMZ.Kulia ni Mwenyekiti wa kikao hicho Bw Mahmoud Omar Hamad ambaye ni Mkurugenzi wa Mipango,Sera na Utafiti kutoka Wizara ya Habari,Utalii na mambo kale Zanzibar. Kikao hicho kilichofanyika Machi 02,2020 Mjini Zanzibar. 

Na Shamimu Nyaki – WHUSM,Zanzibar
Katika kuimarisha Muungano Serikali ya Tanzania Bara  na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika  Sekta za Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo zimeendelea kutekeleza vizuri maeneo ya ushirikiano ambayo yameridhiwa na pande hizo.

Hayo yamebainika leo visiwani Zanzibar katika Kikao cha Wataalam wa Sekta hizo kutoka pande mbili za serikali wakati walipokuwa wakijadili utekelezaji wa maazimio yaliyoridhiwa na Mawaziri wanaosimamia sekta hizo mwezi julai 2019 ambapo Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) pamoja na Shirika la Utangazaji Zanzibar(ZBC) yameendelea kushirikiana katika kuhabarisha umma kwa wakati na kwa usahihi shughuli zote zinazotekelezwa na Serikali ikiwemo Miradi ya Maendeleo pamoja na kubadilishana utaalamu katika sekta hiyo.

Akizungumza katika kikao hicho Mwenyekiti Bw.Mahmoud Omar Hamad ambaye ni Mkurugenzi wa Mipango,Sera na Utafiti wa Wizara ya Habari,Utalii na Mambo kale amesema kuwa lengo la kikao hicho ni kupitia taarifa ya utekelezaji iliyotokana na kikao cha mawaziri kilichofanyika julai 2,Jijini Dodoma kilichoelekeza kuimarisha maeneo ya ushirikiano baina ya serikali zote mbili ambayo yana tija katika Muungano.

“Kikao hichi kina lengo la kutafuta suluhisho katika maeneo ambayo yana changamoto katika ushirikiano wetu lakini pia kuibua maeneo mapya ya ushirikiano ambayo yatakuwa na faida kwa pande zote mbili za muungano wetu”alisema Bw.Mahmoud Omari.

Katika maeneo ambayo Serikali hizo zinashirikiana katika sekta ya habari zimefanikiwa kuwapatia maafisa habari ufadhili wa masomo katika ngazi ya Shahada ya Uzamili nchini China ambapo maafisa mawili kutoka SMT na SMZ walipata nafasi hiyo na sasa wapo masomoni.

Vilevile katika Sekta ya Utamaduni Baraza la Kiswahili la taifa (BAKITA) pamoja na Baraza la Kiswahili Zanzibar (BAKIZA) zimafanikiwa kuandaa Kanzidata ya kusajili wataalamu wa lugha ya kiswahili ngazi ya shahada ya kwanza,Uzamili na Uzamivu ambapo hadi sasa jumla ya waalimu wa kufundisha Kiswahili 1,224 kutoka SMT na 414 kutoka SMZ wamesajiliwa.

Hata hivyo katika Sekta ya Michezo ushirikiano umeendelea kuwepo kwa kuwa WHUSM,OR TAMISEM na Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia zimekua zikiendesha mashindano ya michezo shuleni ya UMISSETA na UMITASHUMTA  ambapo kwa upande wa Zanzibar michezo ya UMISSETA ndio inayoshiriki na  tayari Serikali zote mbili zimekubaliana kuanzisha mashindano ya UMITASHUMTA visiwani humo.


Kikao hicho ni cha awali ambacho kitafuatiwa na kikao cha Makatibu Wakuu na baadae kufuatiwa na kikao cha Mawaziri wanaosimamia sekta hizo.
Mwenyekiti wa kikao cha kujadili maeneo ya ushirikiano baina ya Serikali ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) Bw Mahmoud Omar Hamad ambaye ni Mkurugenzi wa Mipango,Sera na Utafiti kutoka Wizara ya Habari,Utalii na mambo kale Zanzibar. Kikao hicho kilichofanyika Machi 02,2020 Mjini Zanzibar. 
Mwakilishi kutoka Kampuni ya magazet ya Serikali akitoa maoni katika kikao cha kujadili maeneo ya ushirikiano baina ya Serikali ya Serikali ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ).Kulia ni Mkurugenzi msaidizi Idara ya Habari -Maelezo SMT.
Baadhi ya washiriki wa kikao cha kujadili maeneo ya ushirikiano baina ya Serikali ya Serikali ya Muungano wa Tanzania (SMT) na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ).Kulia ni Mkurugenzi msaidizi Idara ya Habari Maelezo SMT.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.