Habari za Punde

SERIKALI NA WADAU WAJA NA ELIMU JUU YA CORONA KWA WATOTO

Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Watoto Wadogo Tanzania (TECDEN) Bruno Ghumpi (mwenye shati la batiki) akitoa maelezo kuhusu umuhimu wa uwepo wa elimu kwa wazazi na walezi ili kuwaelimisha watoto kuhusu kujikinga na maambukizi ya Virusi vya Corona katika kikao kilichofanyika jijini
Baadhi ya wadau wakifuatilia hoja mbalimbali katika kikao kilichowakutanisha Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii kwa lengo la kuandaa ujumbe utakaowalenga wazazi kuwaelimisha watoto   jinsi ya kujikinga na maambukizi ya Virusi vya Corona.
Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano WAMJW

Na Mwandishi Wetu Dar es Salaam.                                                                                  
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii) kwa kushirikiana na Mtandao wa Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Watoto Wadogo Tanzania (TECDEN), Taasisi ya Chakula na Lishe, Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Watoto (UNICEF) wameandaa mkakati wa kufikisha ujumbe kwa watoto kuhusu kujikinga na maambukizi ya Virusi vya Corona.
Akizungumza leo katika kikao kazi kilichowakutanisha wadau hao jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Watoto Wadogo Tanzania (TECDEN) Bruno Ghumpi amesema kumekuwepo na ujumbe mbalimbali katika kujikinga na maambukizi ya Virusi vya Corona ila kumekosekana ujumbe maalum unaolenga makundi maaalum ikiwemo wanawake wajawazito na watoto wadogo kuanzia miaka 0 hadi minane.
Ameongeza kuwa kuwepo kwa elimu sahihi kwa watoto hao kuhusu ugonjwa wa COVID 19 itawasaidia wazazi au walezi na watoto wenyewe kupata taarifa zitakaziwasaidia kujikinga na Virusi hivyo ili kupunguza au kuondokana na maambukizi ya Virusi hivyo katika maeneo yao.
“Ujumbe huu kwa watoto ni muhimu sana kwani kundi hili kwa sasa lipo nyumbani kutokana na kufungwa kwa shule hivyo ni vizuri wazazi na walezi wakazingatia masuala muhimu ya kuwafundisha watoto wao kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona” amesema
Kwa upande wake Afisa Maendeleo ya Jamii Mkuu kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Bw. Mathias Haule amesema kuwa ni muhimu kwa wadau kuhakikisha wanafikisha elimu katika ngazi ya chini kuanzia familia, kijiji/mtaa ili kuwezesha watu hao kupata taarifa na elimu sahihi juu ya kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona.
“Elimu ifike katika ngazi ya familia hasa katika maeneo ya vijijini ambako bado elimu haijawafikia kwa kasi inayotakiwa ili kuondokana na maambukizi ya virusi vya Corona nchini.” Amesema

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.