Mkurugenzi
wa HUPEMEF, Mchungaji Saimon Chemu
(Kulia) akitoa maelezo mafupi kwa Mwenyekiti wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew
Mwaimu (Kushoto) alipotembelea ofisi za
Taasisi hiyo zilizopo Wilayani Magu, jijini Mwanza Aprili 21, 2020.
Mwenyekiti
wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu (Kushoto) akijadiliana jambo na Mkurugenzi wa HUPEMEF, Mchungaji Saimon Chemu (Kulia) muda mfupi baada ya kumalizika
kwa kikao.
Mwenyekiti
wa THBUB, Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu (Katikati- waliokaa) akiwa katika picha ya
pamoja na Uongozi wa Taasisi ya HUPEMEF. Kulia waliokaa ni Afisa Mfawidhi wa
Ofisi za THBUB Kanda ya Ziwa, Albert Kakengi, na wapili kulia ni Katibu wa
Mtandao AZAKI Wilayani Magu, Emanuel Makanja. Kutoka kushoto ni Kaimu Katibu Mtendaji wa
THBUB, Hajjat Fatma Muya na wapili kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa HUPEMEF,
Mchungaji Saimon Chemu.
Na Mbaraka Kambona,
Mwenyekiti
wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB), Jaji (Mst.) Mathew Mwaimu
amezitaka taasisi zilizoingia mkataba wa
ushirikiano na Tume kuendeleza jitihada za kusaidia wananchi ili kutatua kero
zinazowakabili katika maeneo yao.
Jaji
Mwaimu alitoa kauli hiyo wakati wa mkutano baina ya THBUB na Taasisi ya Huruma,
Peace and Mercy Foundation (HUPEMEF) uliofanyika katika ofisi za taasisi hiyo
zilizopo Wilayani Magu, Mkoani Mwanza Aprili 21, 2020.
Akiongea
katika kikao hicho Jaji Mwaimu alieleza kuwa lengo la THBUB kuingia makubaliano
na Taasisi ni kuendelea kusaidia wananchi kupata huduma pale ambapo Tume
haiwezi kufika.
“Lengo
la ushirikiano ni nyinyi kuisaidia Tume kuwafikia wanachi kule chini ambapo
Tume haiwezi kufika, hivyo tuendeleze jitihada zaidi kusaidia wananchi”,
alisema Jaji Mwaimu
Aliendelea
kuwasisitiza kuzingatia kazi
walizojipangia ili waweze kupata matokea tarajiwa kwa jamii ikiwemo kuwapunguzia migogoro inayoikabili.
Aliongeza
kuwa Tume inafahamu kazi ambazo taasisi hizo zinazifanya na hivyo itaendelea
kushirikiana nazo kupitia mkataba wao wa ushirikiano.
Aidha,
Jaji Mwaimu aliishauri taasisi ya HUPEMEF kufanya kazi kwa ukaribu na Ofisi za
THBUB zilizopo Kanda ya Ziwa ili waweze kushirikiana katika kutatua migogoro ya
wananchi wa eneo la Kanda ya Ziwa.
“Tumieni
vizuri Ofisi zetu za Kanda zilizopo hapa Mwanza, msiache kushirikiana nayo, kwa
kufanya hivyo kutawasaidia kushughulikia kwa urahisi yale malalamiko ambayo
hamna mamlaka nayo na kuyapeleka Tume ambayo ina mamlaka ya kuyashughulikia”,
aliongeza Mwaimu
Mkurugenzi
wa HUPEMEF, Mchungaji Saimon Chemu
aliishukuru THBUB kwa ziara waliyoifanya katika ofisi hizo na kusema kuwa imewapa
nguvu kubwa ya kuendelea kufanya kazi.
“Mwenyekiti
tunakushukuru kwa kutuunganisha na Ofisi ya Kanda, tutafanya nayo kazi kwa
ukaribu ili tushirikiane nao katika kusaidia wananchi”, alisema Mchungaji Chemu
Jaji
Mwaimu alikutana na Uongozi wa Taasisi ya HUPEMEF ikiwa ni sehemu ya ziara yake
jijini Mwanza ambayo lengo lake kubwa ni kutembelea ofisi za Tume zilizopo
kanda ya Ziwa ili kushughulikia malalamiko ya wananchi yaliyowasilishwa katika ofisi hizo.
No comments:
Post a Comment