Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano
na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akitoa cheti cha kuhitimu mafunzo ya
wakaguzi wa mazingira kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa Mkoa wa Dodoma kwa Afisa
Mazingira kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa, Theodory Mulokozi wakati wa
kilele cha maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano
na Mazingira Mhe. Mussa Azzan Zungu akizungumza na washiriki wa mafunzo ya
Wakaguzi wa Mazingira katika Siku ya Mazingira Duniani
Na Lulu Mussa-Dodoma
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Mhe. Mussa Azzan Zungu
amesema suala la mabadiliko ya tabianchi halitambui mipaka ya kijiografia wala
ya kisiasa, hivyo, juhudi za kukabiliana na changamoto hii zinahitaji
ushirikiano wa pamoja baina ya Jumuiya za Kimataifa.
Hayo ameyasema hii leo Jijini Dodoma katika kilele cha Siku ya
Mazingira Duniani ambapo ameitaka jamii ya watanzania kuendelea kulinda
mazingira kwa mustakabali wa maendeleo endelevu.
Amebainisha kuwa nchi yetu ni Mwanachama wa Jumuiya za Uhifadhi
na Usimamizi wa Mazingira za kikanda na za Kidunia, hivyo inatekeleza Sera na
Sheria za mazingira kuendana na makubaliano na maazimio yanayofikiwa katika
Jumuiya hizo kwa kadri inavyowezekana.
“Nchi yetu ni Mwanachama wa Mkataba wa Kimataifa wa kukabiliana
na Mabadiliko ya Tabianchi unaojulikana kama Mkataba wa kulinda mazingira wa
Paris (Paris Agreement). Katika
kutekeleza Mkataba huu, Nchi wanachama zimekubaliana kupunguza uzalishaji wa
gesijoto kwa pamoja na kuongeza juhudi za kuhimili athari za mabadiliko ya
tabianchi” Zungu alisisitiza.
Amesema kuwa Tanzania imeandaa miradi
ya kimkakati kwa lengo la kupunguza uzalishaji wa gesijoto ikiwa ni pamoja na
ujenzi wa reli ya kisasa (Standard Gauge) na ujenzi wa bwawa la
uzalishaji wa umeme wa megawati 2115 (Mwalimu Nyerere Hydropower – Stieglers
Gorge).
“Malori na mabasi hutumia dizeli ambayo
huzalisha gesijoto aina ya hewa ukaa. Reli ya kisasa inayojengwa
haitatumia dizeli bali itatumia umeme ambao unatokana na nguvu ya maji, pia kwa
kujenga bwawa la umeme la Mwalimu Nyerere tutaongeza kiasi kikubwa cha umeme
unaozalishwa kwa nguvu ya maji, na kupunguza kwa kiasi kikubwa matumizi ya gesi
asilia na dizeli katika uzalishaji wa umeme” Zungu alisisitiza.
Amebainisha
kuwa umeme wa uhakika utakaozalishwa na Bwawa la Mwalimu Nyerere utasaidia
wananchi walioko vijijini na mijini kupata nishati ya uhakika na kwa gharama
nafuu na hivyo kupunguza kwa kiasi kikubwa ukataji wa miti kwa ajili ya kupata
nishati ya kuni na mkaa. Jitihada hizi zitachangia kwa kiasi kikubwa kwenye
hifadhi ya mifumo asilia ya kimaumbile/bioanuai.
Awali
Waziri Zungu amewatunuku vyeti Wakaguzi wa Mazingira 22 kutoka Wilaya za Mkoa
wa Dodoma ambao walishiriki mafunzo yalitolewa na Ofisi ya Makamu wa Rais
pamoja na Baraza la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira NEMC.
Siku
ya Mazingira Duniani huadhimishwa tarehe 5 Juni kila mwaka. Kaulimbiu yam waka
huu ni ”Tutunze Mazingira: Tukabiliane na Mabadiliko ya Tabianchi”.
Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa
Rais Muungano na Mazingira Mhandisi Joseph Malongo akizungumza kwenye
maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani iliofanyika katika ukumbi wa
LAPF Dodoma.
Sehemu ya Maafisa Mazingira
kutoka Wilaya na Halmashauri za Jiji la Dodoma ambao leo wamepewa Vitambulisho
rasmi vya wakaguzi wa Mazingira baada ya kuhitimu mafunzo ya Siku tatu jijini
Dodoma. Mafunzo haya yameandaliwa na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa kushirikiana
na Baraza la Taifa la Hifadhi na
Usimamizi wa Mazingira (NEMC).
No comments:
Post a Comment