Habari za Punde

Serikali Yaagiza Miradi ya Maji Inayojengwa Kote Nchini Kukamilika Kabla ya Mwezi Oktoba Mwaka huu.

Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso kulia  na mwenyekiti wa bodi ya Mamlaka ya maji BUWASA Samora Lyakurwa Kushoto akizindua mradi wa maji wa Kanyigo uliopo wilaya ya Missenyi mkoani Kagera uliojengwa na Mamlaka ya maji safi na usafi wa Mazingira Bukoba (BUWASA) Kwa gharama ya shilingi milioni 684.

Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akitoa maagizo kwa meneja wa RUASA Wilaya ya Missenyi ya kutolewa kwa shilingi milioni 170 ili kukamisha mradi wa maji wa Kanyigo na kuweza kuwasambazia wananchi wa vijiji vilivyolengwa kuhudumiwa na mradi huo.
Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso akizungumza na wananchi wa vijiji vya Rubale na kituntu wanaoishi karibu na unapojengwa mradi wa maji wa Kyaka Bunazi wakati wa ziara yake wilayani Missenyi mradi utakao garimu kiasi cha shilingi bilioni 9.4 fedha za kitanzania kwa awamu ya kwanza.
Na Allawi Kaboyo Missenyi.
Naibu Waziri wa Maji Jumaa Aweso amewaagiza wakandarasi, Mamlaka za maji na wakala wa Maji mijini na Vijijini kuhakikisha miradi yote ya Maji wanayoisimamia kwenye maeneo mnbalimbali hapa nchi kuhakikisha inakamilika na kutoa maji kwa wananchi kabla ya mwezi Oktoba mwaka huu.
Aweso ametoa maagizo hayo Agosti 13, mwaka huu alipofanya ziara ya kikazi mkoani Kagera na kutembelea miradi ya maji inayojengwa katika wilaya ya Missenyi ukiwemo mradi wa Kyaka Bunazi ambao ni moja ya ahadi ya Mhe.Rais John Pombe Magufuli alipofika wilayani humo akitokea wilaya ya Karagwe mwaka jana na pamoja na mradi wa maji wa Kanyigo uliodumu kwa miaka mingi bila kutoa huduma ya maji kwa wananchi.
Ameongeza kuwa mpaka sasa serikali imepeleka Zaidi ya shilingi bilioni 1.3 kwaajili ya miradi inayotekelezwa na wataalamu wa ndani ili kuhakikisha wananchi wanapata maji safi nay a uhakika kwa wakati wote hivyo hakutakuwepo na kisingizio chochote cha kuwafanya wananchi kukosa maji kwa wilaya ya Missenyi huku mkoa mzima ukipewa shilingi bilioni 9.7 kwaajili ya kutekeleza miradi ya maji kwa mkoa mzima.
“Serikali ya awamu ya tano ni serikali ya matokeo sio ya maneno wala blaa blaa tumeleta fedha kwaajili ya kujenga miradi ya maji sio kukaa kwenye akaunti na kuishangaa huku wananchi wanateseka na suala la Maji, nimeongea na wahandisi wote wa maji wa moa wa Kagera tumekubaliana na hapa naagiza tena kwa nchi nzima miradi yote kabla ya mwezi oktoba iwe inatoa maji.” Amesema Aweso.
Amesema kuwa serikali imeengia mkataba na chama cha mapinduzi kuwa kufikia mwezi desemba mwaka huu upatikanaji wa maji vijijini uwe asilimia 85% na mijini upatikanaji uwe asilimia 95%  ambapo amesema kuwa kwa mtaalamu atakayeshindwa asimtafute mchawi maana mchawi atakuwa yeye mwenyewe na kazi atakuwa hana.
Akiongea na wananchi waliojitokeza kumsikiliza katika chanzo cha maji cha mradi wa maji wa Kyaka Bunazi Naibu waziri Aweso amesema kuwa wizara ipo mbioni kutekeleza ahadi ya Mhe.Rais Magufuli ya kuhakikisha wananchi wa miji ya Kyaka na Bunazi wanapata maji safi na tosherezi na kumuagiza kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Mwanza MUWASA kuhakikisha mradi huo unakamilika kwa wakati na ikiwezekana kabla ya muda ili wananchi wa miji hiyo waanze kupata maji.
Akiwa katika chanzo hicho wananchi waliibua hoja ya mkandarasi kuwatumia wataalamu wa Kutoka nje ya maeneo yao ambapo Kaimu Mkurugenzi wa MUWASA ambao ndio wasimamizi wakuu wa mradi huo Leonard Musenyele amewaeleza wananchi kuwa mkandarasi bado yupo kwenye hatua za awali ambazo zinahitaji utaalamu Zaidi na pindi ujenzi wa mradi huo utakapoaanza rasmi basi wakazi wa miji hiyo watakuwa watu wa kwanza kupata ajira ambapo ameongeza kuwa Tanki litakalojengwa katika mlima wa kijiji Kituntu utakuwa na uwezo wa kubeba lita milioni mbili.
Hata hivyo wananchi wa vijiji vinavyozingira mradi huo wamemshukuru Mhe.Rais Magufuli kwa kuwatua wakina mama ndoo za maji kwa kuwa wamekuwa wakiteseka kwa kufata maji umbali mrefu na wengine walikuwa wakifa maji walipokuwa wakienda kuchota maji katika mto Kagera.
Aidha Naibu waziri Aweso amezindua mradi wa maji wa Kanyigo uliokuwa ukitekelezwa na Mamlaka ya maji na usafi wa mazingira BUWASA ambapo ameipongeza Mamlaka hiyo kwa kuutekeleza mradi huo kwa wakati hadi kufikia Zaidi ya asilimia 80% na kuanza kutoa maji ambapo amemuagiza meneja wa RUASA wilaya ya Missenyi  kutoa kiasi cha fedha shilingi milioni 170 ili kukamilisha mradi huo.
Ameongeza kuwa kati ya miradi kichefuchefu mmoja wapo ulikuwa mradi huo ambao ulidumu kwa miaka mingi bila kukamilika ambapo amefurahishwa na kazi kubwa iliyofanywa na Mamlaka tena kwa kipindi  kifupi na sasa wananchi wameanza kupata maji  ambao thamani yake ni shilingi milioni 684.
Hata hivyo baada ya uzinduzi huo Naibu waziri alipata fursa ya kuongea na wananchi ambao ni watumia maji wa mradi wa kanyigo ambapo wananchi hao wameonyesha kufurahia ujio wa mradi huo ambapo wameeleza kabla ya kupata mradi huo wa maji walikuwa wakihangaika kwa muda mrefu hali iliyowapelekea wengine kuhatarisha ndoa zao.
Wananchi hao wamesema kuwa kupatikana kwa mradi huo ni ukombozi mkubwa kwa wakina mama wa vijiji hivyo na kumuomba naibu waziri kufikisha salamu za shukrani kwa Rais Magufuli maana amewajali wanyonge.
Awali mkuu wa mkoa Kagera Brigedia Jenerali Marco Gaguti amemuomba Naibu waziri kuwa Mkoa huo katika maeneo mengi unachangamoto ya maji na makandarasi wanaopewa kazi hiyo hushindwa kuimaliza kwa wakati hivyo am,eomba wizara pamoja na Mamlaka kuwasimamia kwa ukaribu Zaidi ili kuhakikisha kero hiyo kwa wananchi inamalizika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.