Na.
Immaculate Makilika – MAELEZO
Tanzania imekuwa kati
ya nchi za kwanza kufungua anga kwa kuruhusu safari za ndege kutoka nchi
mbalimbali duniani kutua nchini baada ya usafiri wa anga kusitishwa kufuatia
janga la ugonjwa wa Covid-19 lililoikumba dunia mwezi Desemba mwaka 2019.
Jitihada hizo za
Serikali za kurejesha safari za ndege baada ya athari ya ugonjwa wa Covid-19
zimekuwa na manufaa ambapo jana (Agosti
5, 2020) ndege ya Shirika la Ndege la Uholanzi (KLM) aina ya Boing 777-200
ilitua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) ikibeba watalii.
Mashirika mengine ya
ndege zilizoanza safari zake nchini ni pamoja na Shirika la Ndege la Ethiopia,
Dreamliner, Boing kutoka Marekani na Gulfstream la Coratia. Ujio wa ndege hizo
unathibitisha kwamba Tanzania inaendelea kuchukua hatua stahiki za kukabiliana
na ugonjwa wa Covid-19.
Mkuu wa Mkoa wa
Kilimanjaro, Anna Mgwira alisema kuwa Serikali ilifuatilia kwa karibu hatua
zote za kutua kwa ndege ya KLM ikiwa ni
pamoja na kuikaribisha ndege hiyo kwa maji kama ilivyo utaratibu. Aidha, kufika
kwa abiria hao nchini kumesababishwa na imani ambayo Serikali imeijengea dunia.
“Tumeijengea dunia
imani kwamba nchi yetu ni salama na ugonjwa wa Covid-19 uliopokuja tulipata na
hofu na sasa tuimeishinda hofu na tumewasaidia na wao kuishinda hofu hiyo kwa
kutojifungia ndani”, alisema Mgwira.
Aliongeza, “Katika
kipindi hiki cha joto katika nchi zao kimewafanya waweze kuja kufurahia maajabu
yaliyopo katika nchi yetu na kurudi na hii inatusaidia sisi kufanya biashara ya
utalii ambapo leo tumepokea wageni 177 wote wakiwa watalii ambao watatembelea
maeneo mbalimbali kwa siku kadhaa”
Naye, Kaimu
Mkurugenzi wa KIA, Christine Mwakatobe alisema kuwa kutua kwa ndege ya KLM
nchini inadhihirisha namna ambavyo Shirika la Afya Duniani (WHO) na Shirika la
Kimataifa la Usafiri wa Anga (IATA) wameiona Tanzania ni sehemu salama.
Aidha, Mwkatobe
alisema hatua hiyo ni muendelezo wa kuirejesha sekta ya utalii nchini ambayo
iliathirika kwa kiasi kikubwa kufuatia janga la ugonjwa wa Covid-19.
“Baada ya shughuli za
sekta ya utalii kurejea katika hali yake ya awali, sasa ajira nazo zimerejea,
fursa mbalimbali za biashara na tunatarajia sekta hii itaendelea kuchangia pato
kubwa katika Serikali”, alisema Mwakatobe
Hivi karibuni
mashirika kadhaa ya ndege yakiwemo
Qatar, Crystal, na Rwanda Air yamefanya safari zake nchini baada ya kuridhishwa
na usalama wa abiria na pamoja na mali, huku hali ya maambukizi ya ugonjwa wa
Covid-19 ikiwa shwari.
No comments:
Post a Comment