Habari za Punde

Ajali ya Moto Kagera Zimamoto Yatoa Tamko Uunguaji wa Shule Nchini

Kaimu Kamishna wa Operesheni wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, DCF Charo Mangare akimpa pole mmoja wa wazazi wa watoto waliokuwepo eneo la tukio la ajali ya moto iliyosababisha vifo vya wanafunzi 10 katika Shule ya Msingi ya Byamungu iliyoko Kata ya Itera,Wilayani Karagwe mkoa wa Kagera
Kaimu Kamishna wa Operesheni wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, DCF Charo Mangare akimsikiliza Muuguzi Mkuu Msaidizi wa Hospitali ya Nyakahanga, Justine Katalaiya (kulia), juu ya hali ya mmoja wa majeruhi wa ajali ya moto iliyosababisha vifo vya wanafunzi 10 baada ya ajali ya moto katika Shule ya Msingi ya Byamungu iliyoko Kata ya Itera,Wilayani Karagwe mkoa wa Kagera.
Kaimu Kamishna wa Operesheni wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, DCF Charo Mangare akifanya ukaguzi baada ya kuwasili eneo la tukio la ajali ya moto iliyosababisha vifo vya wanafunzi 10 katika Shule ya Msingi ya Byamungu iliyoko Kata ya Itera,Wilayani Karagwe mkoa wa Kagera.
Picha na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji
Na Mwandishi Wetu
Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini limewataka wamiliki wa shule nchini kuhakikisha wanafunga vifaa maalumu vya awali vya kuzimia moto ili kuweza kudhibiti majanga pindi yanapotokea na kupunguza athari za majanga hayo
Hayo yalisemwa na Kaimu Kamishna wa Operesheni wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, DCF Charo Mangare baada ya kutembelea Shule ya Msingi ya Byamungu Islamic iliyopo Kata ya Itera, wilayani Kyerwa mkoa wa Kagera ambapo kulitokea ajali ya moto na kusababisha vifo vya wanafunzi 10 na majeruhi sita.
“Pamoja na kuwaagiza wamiliki wa shule kufunga vifaa maalumu vya kudhibiti moto pia nawaagiza makamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini kukagua shule zote na zoezi hilo liwe endelevu ili kuweza kudhibiti madhara ya ajali hizo pindi zinapotokea” alisema DCF Mangare
Akizungumzia chanzo cha ajali hiyo DCF Mangare alisema Kamati ya Ulinzi na Usalama inaendelea na uchunguzi na pindi utakapokamilika taarifa itatolewa kwa wananchi ili kuwepo sasa mbinu za kudhibiti ajali kama hizo.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo Muuguzi Mkuu Msaidizi, Justine Katalaiya alisema majeruhi wanne kati ya sita waliolazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Wilaya ya Karagwe wamehamishiwa Hospitali ya Bugando jijini Mwanza kwa matibabu zaidi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.