Na. Jovina Bujulu-MAELEZO
Hivi karibuni Rais John Pombe Magufuli amezindua Bunge la 12 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kufuatia ushindi wa kishindo alioupata katika uchaguzi wa mwezi Oktoba, ambapo alichaguliwa kuiongoza nchi kwa kipindi kingine cha miaka mitano.
Katika hotuba yake ya
uzinduzi, Rais Magufuli alionyesha dira, falsafa, mwelekeo na vipaumbele vya
nchi katika kipindi cha uongozi wake wa miaka mitano. Pamoja na mengi
aliyozungumzia , Rais aliahidi kuboresha vitambulisho vya wajasiriamali ili
waweze kutambulika rasmi na kuweza kupata mikopo katika taasisi za fedha hapa
nchini.
Rais Magufuli alisema
kuwa, kama alivyoahidi wakati wa kampeni kwamba katika kipindi cha uongozi wake
wa miaka mitano ijayo, Serikali itaendelea kuboresha mazingira ya kufanya
biashara kwa wajasiriamali wadogo, machinga, mama lishe, baba lishe waendesha
boda boda na bajaji.
Tangu ilipoingia
madarakani, Serikali ya Awamu ya Tano ilianza kuwatambua rasmi wajasiriamali
wadogo nchini pote kwa kuwapatia vitambulisho ambavyo vilikuwa vinalipiwa
shilingi 20,000 kwa mwaka. Utambuzi huo uliwapa uhuru wajasiriamali hao wadogo
kufanya biashara zao bila kubugudhiwa na mtu au mamlaka yoyote hivyo kujiongezea
kipato.
Vitambulisho hivyo
vya awali vilitolewa na Rais Magufuli mwaka 2018, ambapo jumla ya vitambulisho
670,000 vilitolewa na kuwawezesha wafanyabiashara ndogo ndogo kutambulika
nchini na kuhakikisha wanafanya shughuli zao bila kusumbuliwa na kama ilivyokuwa
awali ambapo walikuwa wanasumbuliwa sana na mamlaka mbalimbali za miji na
halmashauri.
Katika utaratibu wa
awali, kila mkoa ulipewa vitambulisho 25,000, ambapo kila mjasiriamali aliyekihitaji
alikilipia na pesa ilipelekwa TRA na vilikuwa vinatolewa kwa hiari. Utaratibu
huo ulimwezesha kila Mkuu wa Mkoa kukusanya shilingi milioni 500 ambazo ni
mchango wa sekta hiyo ya wafanyabiashara.
“Miaka mitano
iliyopita tulianzisha utaratibu wa kutoa vitambulisha maalum kwa wajasiriamali
wetu wadogo, tunakusudia kuviboresha vitambulisho hivyo kwa kuweka picha na
taarifa nyingine muhimu kama ilivyo kwenye vitambulisho vya Taifa (NIDA) na
kwenye Hati za kusafiria(Pasipoti)”, alisema Rais Magufuli.
Kuboreshwa kwa
vitambulisho hivyo kutakuwa ni fursa nyingine muhimu kwani wataweza kukua na
kutajirika na kuondokana na dhana ya kuwa wafanyabiashara wadogo ambapo hii
itawezekana kwa sababu wataweza kutambulika kwenye taasisi za fedha na kuweza
kupata mikopo kwa ajili ya kukuza biashara.
Aidha, kutokana na
maboresho hayo wajasiriamali hao wataweza kukuza mitaji yao kwa kuwa sasa watakuwa
na uwezo wa kukopa na kuweza kupanua biashara zao nchi nzima. Hivyo ni wakati
muafaka kwao kukuza na kupanua biashara zao kwa sababu ya uwezo wao wa kuongeza
mtaji utakuwa umerahisishwa.
Endapo wajasiriamali
hao wataitumia fursa hii ipasavyo mbali
na kuweza kupata mikopo ya biashara , wataweza pia kupata mikopo mikubwa ambayo
itawanasua katika umaskini ikiwa ni pamoja na kubadilisha biashara zao kutoka
kuwa ndogo ndogo na kuwa za kati hadi za juu.
Vitambulisho hivyo
pia vitawafanya wajiamini zaidi ikiwa ni pamoja nakuongeza bidii katika shughuli zao kwani sasa wataweza kukopesheka kutokana na kuwa na vitambulisho
hivyo vilivyoboreshwa. Hivyo wafanya biashara hawana budi kuchangamkia fursa
hii kwa kuhakikisha kuwa wanavipata pale vitakapokuwa vimeanza kulipiwa.
Kufuatia kauli ya
Rais kuhusu kuboresha vitambulisho hivyo wajasiriamali wameonesha kufurahishwa
na hatua hiyo na kusema kuwa sasa ni wakati wa kukuza mitaji yao na kuinuka kiuchumi. Mama
Lishe, Mwajuma Salum wa soko la Mwananyamala amesema kuwa, “ Rais Magufuli
kweli ni mkombozi wa wanyonge, miaka yake mitano ya mwanzo alitupatia
vitambulisho na hivyo kutuwezesha kufanya biashara zetu kwa amani bila
kusumbuliwa na mtu yeyote, sasa amesema
ataboresha vitambulisho hivyo ili tuweze kukopesheka, Mungu amlinde”.
Naye muuza matunda
katika eneo la Afrika Sana Sinza, Mary Zephania amesema, “ Vitambulisho
vikiboreshwa na nikapata cha kwangu hatua ya kwanza nitakwenda kuomba mkopo ili
nikuze mtaji wa biashara yangu ili ikiwezekana niweze kusafirisha matunda hata
nje ya nchi”.
Baadhi ya
wafanyabishara wadogo wadogo wa soko la Manzese wamesema kuwa wana imani na
Serikali ya Rais Magufuli ambayo wakati wote ina dhamira ya kuwaondoa katika umaskini,
maana tangu Rais aingie madarakani amekuwa akihimiza kuondolewa changamoto
mbalimbali zinazowakabili wajasiriamali.
Tangu kuingia
madarakani mwaka 2015, Rais Magufuli amechukua hatua mbalimbali za kuimarisha
uchumi na kuwakomboa wananchi kutoka katika umaskini na kuwawezesha kufanya
biashara bila kusumbuliwa ili kuwafanya wawe matajiri. Aidha katika hotuba yake
kwa Bunge la 12, ameendelea kusema kuwa Serikali atakayoiunda itaendeleza
jitihada za kukuza uchumi.
No comments:
Post a Comment