STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS
SECRETARY
PRESS
RELEASE
Zanzibar January 06, 2021
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amewakumbusha Viongozi wa chama cha Mapinduzi (CCM) wajibu wa kurudi kwa wananchi
kuwatumikia pamoja na kushirikiana nao katika kuzitafutia ufumbuzi changamoto
mbali mbali zinazowakabili, baada ya uchaguzi mkuu kumalizika.
Dk. Mwinyi amesema hayo katika Ufunguzi wa Kongamano la
Jumuiya za CCM za UWT, Wazazi pamoja UVCCM lililofanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdul-wakil Kikwajuni Jijini Zanzibar, likiwa na lengo la
kuwapongeza Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli pamoja an Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi kwa ushindi mkubwa waliopata katika uchaguzi Mkuu uliofanyika mwezi
Oktoba, 2020.
Amesema wananchi wana shida mbali mbali zinazohitaji misaada
kutoka kwa viongozi wao, hivyo akawataka
kutokuwasahau wale waliowachagua na kubainisha kuwa huo ndio mwelekeo sahihi wa
Viongozi wanaotoka CCM.
Alisema uchaguzi umemalizika, hivyo kazi kubwa ilioko mbele ya
viongozi wa chama hicho ni kuwatumikia wananchi kwa kuyatekeleza mambo mbali mbali
waliyoyaahidi katika kampeni pamoja na kuitekeleza Ilani ya Uchaguzi wa CCM ya 2020,- 2025.
Aidha, aliwakumbusha
wanachama wa chama hicho wajibu walionao katika kujiandaa na uchaguzi ndani ya
chama hicho ifikapo mwaka 2022, hivyo
akawataka kujiandaa kwa msingi kuwa
hatua hiyo itatoa fursa ya kupanga safu za uongozi katika chama hicho.
“Nasaha zangu kwenu wakati utakapofika, wachagueni viongozi wenye mapenzi ya dhati na CCM na sio wanaotafuta maslahi yao wenyewe kupitia CCM”, alisema.
Alieleza kuwa ni muhimu kupata viongozi wenye uwezo wa
kukitumikia Chama hicho ili waweze kukivusha katika uchaguzi mkuu ujao,
akiamini Chama hicho kina hazina kubwa ya viongozi bora.
Aidha, Dk. Mwinyi alisema
hatua zilizoanza kuchukuliwa katika kupambana na vitendo vya ubadhirifu wa mali
ya umma, uzembe na ukiukwaji wa sheria pamoja na rushwa zinalenga kuleta
nidhamu katika matumzi ya fedha za Serikali.
Alisema serikali imeanza kuchukua hatua za kupambana na
vitendo vya ubadhirifu wa mali ya Umma, uzembe, ukiukwaji wa sheria, pamoja na
rushwa miongoni mwa watendaji wake kwa dhamira njema ya kuleta nidhamu katika
matumizi ya fedha za Serikali kwa manufaa ya wananchi.
Aliwahakikishia wana CCM kuwa wale wote watakaohusika na
matukio ya vitendo hivyo watachukuliwa hatua za kisheria bila kumuonea mtu,
hivyo akawataka wananchi kuunga mkono hatua hiyo.
“Nafahamu kuwa hatua hizi tunazozichukua kuna wengi
wanazifurahia, ingawa wapo wachache zinawaumiza lakini ni vyema watuvumilie”,
alisema.
Akigusia maudhui ya kufanyika kwa Kongamano hilo, Dk. Mwinyi
alisema ushindi mkubwa iliopata chama hicho katika uchaguzi mkuu uliofanyika
mwezi Oktoba 2020 katika pande mbili za Muungano na katika ngazi zote, ni
kielelezo cha imani na matumaini waliyonayo Watazania kwa chama chao.
Alisema Watanzania wanaridhishwa na utendaji wa chama hicho na
ndio maana wakafanya maamuzi ya kuendelea kukichagua kwa kura nyingi.
Alisema CCM kinajipambanua na vyama vyengine vya siasa kwa kuwa
na ukweli katika utekelezaji wa Ilani yake ya Uchaguzi pamoja na ahadi zake kwa
asilimia kubwa katika kila awamu ya Uongozi.
“CCM ina Ilani na sera zinazotekelezeka kulingana hali halisi
ya wananchi hasa walio wanyonge, zikiwa na lengo la kuwaletea maendeleo na
Ustawi wa maisha yao.
Rais Dk. Mwinyi alitoa shukurani kwa Viongozi na wanachama wa
Jumuiya hizo kwa uamuzi wa kuandaa Kongamano hilo lenye lengo la kumpongeza kutokana na ushindi mkubwa wa
asilimia 76.27 aliopata katika Uchaguzi mkuu pamoja na kuipongeza CCM kwa kuwa na utaratibu mzuri wa
Kidemokrasia wa kupata viongozi katika ngazi mbali mbali.
Aidha, aliwapongeza wanachama wa CCM kwa namna wanavyojitokeza
kwa wingi katika hafla mbali mbali za ufunguzi wa miradi ya maendeleo na
Uwekaji wa Mawe ya msingi katika kipindi hiki cha shamrashamra za kuelekea
maadhimisho ya miaka 57 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Mapema, Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Dk. Abdalla Juma Sadalla
‘Mabodi’alisema Chama hicho kinaunga mkono hatua zinazoendelea kuchukuliwa na
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Mwinyi katika
kuimarisha ustawi wa jamii pamoja na mapambano dhidi ya Udhalilishaji, sambamba
na hatua ya kuunda serikali ya umoja wa Kitaifa (GNU).
Alisema hatua ya kuunda
GNU itaendeleza umoja na mshikamano wa Wazanzibari na kudumisha Utawala bora.
Alitoa pongezi kwa kusimamia na kuweka kipaumbele katika uimarishaji wa uchumi
wa nchi kupitia uchumi wa Buluu, akibainisha Bahari kuwa ni rasilimali muhimu
hapa nchini.
Alisema CCM itaendelea kusimamia kikamilifu uibuaji wa matukio
mbali mbali ya ubadhirifu na uwajibikaji.
Aidha, alisema miongozo ya utekelezaji wa Jumuiya hizo
inafanyakazi kwa pamoja na ndio iliosababisha kushuka hadi chini na kukipatia
chama hicho ushindi.
Nae, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Wazazi Taifa Othman Ali Maulid
alisema Kongamano hilo linalenga kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Mwinyi kwa ushindi mkubwa wa asilimia 76.27 aliopata katika uchaguzi
mkuu uliofanyika Oktoba, 2020.
Alisema kwa pamoja Jumuiya hizo zinampongeza Dk. Mwinyi kutokana
na hotuba mbali mbali alizozitoa kwa nyakati tofauti na hivyo kuwapa matumaini
makubwa wananchi katika utumishi wake.
Katika kongamano hilo Mada tatu ziliwasilishwa , ikiwemo ya
‘Uchumi wa Buluu’ ; Utekelezaji wa Ilani ya CCM 2020-2025 pamoja na Historia ya
Mapinduzi ya Zanzibar ya 1964.
Katika Kongamano hilo lililoandaliwa na Jumuiya za CCM za UWT,
Wazazi pamoja na UVCCM, Viongozi mbali mbali wa chama hicho na Serikali
walishiriki, wakiwemo Wake wa Viongozi wakuu wa Kitaifa wakiongozwa na mama
Mariamu Mwinyi pamoja na Wake wa Viongozi wakuu
wastaafu, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Abdalla Juma Sadalla, Naibu Spika wa Baraza
la Wawakilishi Mgeni Hassan Juma,
Wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Mawaziri pamoja
na Wabunge na Wawakilishi .
Abdi
Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422
Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822
E-mail:
abdya062@gmail.com
No comments:
Post a Comment