Homa ya mapafu (Pneumonia) kwa watoto
MWILI wa binadamu una mapafu
mawili yenye maumbile yanayofana na kazi kuu ya mapafu ni sehemu ya mwili
inayoingiza oksijeni mwilini na kuipeleka kwenye seli za mwili. Ni kiungo kikuu
kwenye mfumo wa upumuaji.
Inapotokea mtu au mtoto
kapata homa ya mapafu, vifuko hivi hujaa maji au usaha, hivyo huathiri
upitishaji wa hewa safi kwenye damu na kusababisha tatizo la kupumua.
Homa ya mapafu au ‘pneumonia’
ni ugonjwa unaoshambulia mfumo mzima wa hewa, ni aina ya maambukizi
yanayoathiri mapafu. Aidha ni ugonjwa unaoua watoto wengi hasa katika nchi
zinazoendelea duniani ikiwemo Zazibar. Inakadiriwa kwamba watoto karibu milioni
1.6 walio chini ya miaka mitano wanakufa kila mwaka kutokana na ugonjwa huu.
Vihatarishi vya homa ya mapafu
v Watoto wenye ukosefu wa
kinga mwilini
v Ukosefu wa lishe bora hasa
kwa watoto wachanga ambao hawanyonyeshwi ipasavyo.
v Aidha uwepo wa magonjwa
mengine, kwa mfano, maambukizi ya virusi vya UKIMWI, saratani na ugonjwa wa
surua hupelekea kinga ya mwili kuwa dhaifu.
v Mazingira duni yenye moshi
wa sigara au moshi ndani ya nyumba unaosababishwa na kupikia kuni au mkaa.
v Msongamano ndani ya nyumba
kutokana na watu kuwa wengi sehemu moja nayo huweza kusababisha watoto kupata
homa ya mapafu.
Sababu za ugonjwa wa homa ya mapafu
Homa ya mapafu inasababishwa
na vimelea vya maradhi kama vile bacteria, virusi, parasiti na fangasi.
Kwa kawaida vimelea
hushambulia mwili wa binadamu kulingana na umri na kinga ya mwili. Kwa mfano,
bakteria wanaosababisha homa ya mapafu kwa watoto wachanga ni tofauti na wale
wanaosababisha ugonjwa huo kwa watoto wakubwa.
Baadhi ya vimelea wa
bakteria wanaoshambulia watoto ni pamoja na ‘streptococcus pneumoniae’ ambao ni
aina ya bakteria wanaoongoza kusababisha homa ya mapafu kwa watoto katika
visiwa vyetu.
Wapo pia ‘haemophilus
influenzae’ aina b (HIB) ambao ni aina ya pili ya bacteria walio maarufu zaidi
kwa kusababisha ugonjwa wa homa mapafu kwa watoto.
‘Staphylococcus aureus’ ni
aina nyingine ya bacteria ambao hushambulia zaidi watoto wachanga. Kuna pia group
B streptococci, ambao pia hushambulia zaidi watoto wachanga.
Kwa upande wa virusi, virusi
wa aina ya ‘respiratory syncytial virus’, ndiyo wanaoongoza kwa kusababisha
homa ya mapafu kwa watoto.
Aidha, vimelea wa ‘pneumocystis
jiroveci’ ambao kwa sasa huwekwa kwenye kundi la parasiti ni maarufu zaidi
miongoni mwa parasiti wanaosababisha homa ya mapafu kwa watoto wenye upungufu
wa kinga mwilini hususani watoto wenye VVU.
Aina nyingine za bakteria
ambao hushambulia zaidi watoto wakubwa ni pamoja na ‘mycoplasma pneumonia’ na
‘chlamydia pneumonia’.
Jinsi homa ya mapafu inavyoenezwa
Mara nyingi inapotokea kinga
ya mwili ya mtoto imeshuka kwa sababu yeyote ile, vimelea hivi huweza kusambaa
na kufika mpaka sehemu ya chini ya mfumo wa njia ya upumuaji (lower respiratory
tract) na hatimaye kushambulia mapafu.
Halkadhalika, vimelea hawa
wanaweza kuenea kwa njia ya damu kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto kabla ya
kuzaliwa, yaani kipindi cha mimba.
Dalili za ugonjwa wa homa ya mapafu
Kwa watoto wadogo, dalili za
awali zinaweza kuwa homa kali pamoja na mtoto kuhangaika, kunyong’onyea kung’ang’anaa.
Watoto wanaozaliwa wakiwa na uambukizi wa bakteria aina ya ‘streptococcus’
kundi ‘B’ wanaweza kuwa na homa na kupumua kwa shida.
Wakati mwingine mtoto
anaweza kuwa na dalili ambazo si maalum kama vile kuhangaika na kushindwa
kunyonya au kula vizuri bila kuwa na dalili yeyote ya kushindwa kupumua. Hali
hii inaweza kutokea kwa mtoto wa umri wowote ule.
Dalili za kawaida za homa ya
mapafu ambazo huwapata karibu watoto wote wanaoathirika na ugonjwa huu ni
pamoja na; homa kali, kuhisi baridi, kikohozi, kupumua kwa haraka kuliko
kawaida, kutoa sauti isiyo ya kawaida wakati wa kupumua, mbavu za mtoto kuingia
ndani wakati wa kupumua na maumivu ya tumbo.
Dalili nyengine kupoteza
hamu ya kucheza, kupoteza hamu ya kula na kushindwa kunyonya, mtoto kubadilika
rangi na kuwa na rangi buluu katika midomo na kucha (CYANOSIS).
Hata hivyo, si lazima dalili
zote hizi ziwepo kwa kila mtoto. Baadhi ya watoto huonesha kupumua kwa haraka
kama dalili pekee ya homa ya mapafu.
Iwapo vimelea vimeshambulia
sehemu za chini ya mapafu karibu ya tumbo, sehemu ijulikanayo kama kiwambo au ‘diaphragm’,
mtoto anaweza asioneshe hali yeyote ya kushindwa kupumua ingawa anaweza kuwa na
homa na kujihisi maumivu makali ya tumbo, vichomi na pia kutapika.
Kwa watoto wachanga zaidi
wanaweza kushindwa kunyonya na pia kupoteza fahamu na kupata degedege.
Uchunguzi na vipimo
Daktari humchunguza mtoto
kwa kusikiliza dalili za ugonjwa kutoka kwa
kutumia kipimo kinachoitwa ‘stethoscope’.
Vipimo hivyo ni pamoja na
X-ray ya kifua, au CT-scan ya kifua, pamoja na damu ili kuchunguza madhara
yaliyoletwa na homa hii ya mapafu.
X-ray ya kifua na CT-scan ya
kifua vina uwezo wa kuonesha tatizo hata pale ambapo daktari ameshindwa kusikia
sauti maalum kwa kutumia kifaa chake cha ‘stethoscope’.
Matibabu
Matibabu homa ya mapafu hutegemea
ni aina gani ya vimelea ya maradhi, umri na hali ya yule mtoto ilivyo.
Mara nyingi dawa za maji za ‘antibiotics’
kama vile ‘erythromycin’, ‘benzylpenicillin’, ‘cefotaxime’, ‘amoxycillin’, ‘clarithromycin’
nakadhalika hutumika kutibu homa na
maambukizi huku dawa za panadoli na ‘ibumex’ hutumika kushusha homa ya mwili.
Ikumbukwe kwamba dawa za ‘antibiotics’
hazina uwezo wowote wa kutibu homa inayosababishwa na virusi (viruses), kwa
hiyo hupona kwa kutumia tu dawa za kushusha homa, lishe, mazingira yenye hewa
safi na kumpa mtoto maji mengi.
Na hii ieleweke kwambaa ni
daktari pekee ndiye anayeweza kufahamu kama mtoto wako anahitaji ‘antibiotics’
au dawa za aina nyingine. Kwa hiyo ni muhimu kwa mzazi ama mlezi kumpeleka mtoto
kituo cha afya au hospitalini haraka pindi anapoonesha dalili za ugonjwa badala
ya kuamua kumpa dawa bila kufuata ushauri wa wataalamu wa afya.
Kinga homa ya mapafu
Homa ya mapafu inaweza kuzuiliwa
kwa chanjo, chanjo dhidi ya Hib, pneumococcus, surua na kifaduro ni njia
mojawapo ya kuzuia homa ya mapafu.
Mtoto kuishi katika
mazingira yenye hewa safi.
Lishe ya kutosha ni muhimu
kwa kuboresha kinga ya mwili ya mtoto ambapo inashauriwa mama kunyonyesha mtoto
bila kuchanganya na kitu chochote walau kwa miezi sita ya mwanzo ya maisha
yake.
Kuhimiza usafi katika makaazi
kama kutotumia jiko la mkaa au kuni ndani ya nyumba na uvutaji wa sigara ni
jambo linaloshauriwa pia.
Kwa watoto wenye virusi vya UKIMWI,
matumizi ya dawa ya ‘cotrimoxazole’ kila siku husaidia kupunguza uwezekano wa
kupata homa ya mapafu.
Indhari
Tafiti nyingi duniani
zimeonyesha kwamba kinga na tiba sahihi ya homa ya mapafu inaweza kuzuia vifo
milioni moja kwa watoto duniani kila mwaka. Hivyo ni wajibu wetu sote
kushirikiana kupambana na ugonjwa huu.
Imetayarishwa na:
Mohammed Sharksy
Mkufunzi Msaidizi,
Skuli ya Afya Sayansi za Tiba,
Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar, SUZA
0777432493 email:
ruruma96@gmail.com
No comments:
Post a Comment