Habari za Punde

Rais Dk Mwinyi: Sijaridhika na jinsi sekta ya Utalii inavyoendeshwa

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar, wakati wa kuwasilisha taarifa yao ya utekelezaji wa maagizi ya Rais aliyoyatoa kwa Mawaziri na Makatibu Wakuu wakati wa kuwaapisha katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar

RAISwa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameeleza haja kwa Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale kubadilika kwani hariziki na jinsi sekta ya Utalii inavyoendeshwa hasa ikizingatiwa kwamba uchumi wa Zanzibar unategemea sekta hiyo.                                                                                                  

Rais Dk. Mwinyi aliyasema hayo leo Ikulu Jijini Zanzibar wakati alipokutana na uongozi wa Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale pamoja na baadhi ya Watendaji wa Wizara hiyo katika mkutano maalum wa kuwasilisha taarifa ya Utekelezaji wa maagizo waliyopewa Mawaziri pamoja na Makatibu Wakuu wakati wa hafla ya kuapishwa.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa uchumi wa Zanzibar kwa kiasi kikubwa unategemea sekta ya utalii lakini bado hajarizika na utalii unavyoendeshwa na kuna haja ya mambo mengi katika sekta hiyo kuyafanywa kinyume na ilivyo hivi sasa.

Rais Dk. Mwinyi alieleza kwamba miongoni mwa juhudi ambazo zinahitajika kwa kiasi kikubwa ni kuitangaza zaidi sekta ya utalii ili kuona maendeleo yanapatikana kama ilivyokusudiwa.

Aliongeza kuwa dhima ya mikutano hiyo anayoiendesha Ikulu ni kurekebisha utendaji hivyo kuna kila sababu kwa Wizara hiyo kubadilika ili kuhakikisha sekta ya utalii inafikia yale malengo yaliyokusudiwa katika kuimarisha uchumi wa Zanzibar.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi alieleza haja ya kuwa na chombo maalum cha Utalii kikiwa na azma ya kuimarisha uchumi wa Zanzibar.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Mwinyi akaeleza kutokuwa na ulazima wa kuwepo kwa programu nyingi katika Wizara hiyo na badala yake zikapunguzwa kwa lengo kufikia mafanikio yaliyokusudiwa.

Akieleza kuhusu makumbusho, Rais Dk. Mwinyi alieleza haja ya kuyafanyia utaratibu maalum makubusho ya Zanzibar ambayo utapelekea makumbusho hayo kufanya kazi badala ya kuwa kama yalivyohivi sasa kwani moja ya vitu vinavyochangia mapato ya utalii ni makumbusho.

Pia, alieleza umuhimu wakukusanywa fedha kwa njia ya elektroniki hatua ambayoitaondosha kupotea ama kuvuja kwamapato katika sekta ya utalii.

Kwa upande wa nyumba za Mji Mkongwe wa Zanzibar, Rais Dk. Mwinyi alisisitiza haja kwa Wizara hiyo kutafuta wawekezaji wa kuekeza kwa baadhi ya nyumba walizozitenga sambamba na kuimarisha miundombinu ya Mji huo ili uwe Mji Mkongwe wa kitalii.

Rais Dk. Mwinyi pia, alieleza kwamba ni vyema historia ikahifadhiwa na kwa wale waliovamia maeneo ya kihistoria waondoshwe.

Nae Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi Mhandisi Zena Ahmed Said alieleza haja kwa Wizara hiyo kuimarisha miundombinu ya Mji Mkongwe wa Zanzibar.

Mapema Waziri wa  Wizara yaUtali na Mambo ya Kale Lela Muhammed Mussa alimpongeza Rais Dk. Mwinyi kwa kasi anayokwenda nayo ya kuwatumikia wananchi wa Zanzibar kwa kuhakikiisha wanapata maendeleo bila ya kujali itikadi za kisiasa, dini, rangi au ukabila.

Alieleza dhamana ya Wizara hiyo ikiwa ni pamoja na kusimamia sekta kuu mbili ambazo ni Utalii na Mambo ya Kale ambazo sekta hizo hujumuisha Kamisheni moja, Idara nne, mamlaka moja na Ofisi Kuu Pemba.

Waziri Lela alieleza miongoni mwa vipaumbe vya Wizara hiyo kwa miaka mitano ijayo 2021-2025 ikiwa ni pamoja na kuibua vivutio vipya na kuimarisha vivutio vya utalii vilivyopo nchini ili kufikia lengo la wageni 850,000 pamoja na kuongeza siku za ukaazi kutoka siku nne hadi siku tisa ifikapo mwaka 2025.

Aidha, alieleza Sheria ambazo zinahitaji kurekebishwa hasa ikizingatiwa kwamba Wizara hiyo inasimamia sheria tatu ambazo zinahitaji kufanyiwa mapitio ili ziende sambamba na mipango ya ukuaji uchumi ya kitaifa kama vile Dira ya Maendeleo 2050, Sera zinazoiongoza sekta hiyo pamoja na mitizamo mipya katika uendeshaji wa seta ya utalii.

Nae Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Fatma Mabrouk Khamis alieleza jinsi hatua zilivyochukuliwa na Wizara hiyo katika kuyafanyia kazi maagizo waliyopewa na Rais ikiwa ni pamoja na kushirikiana na vyombo vya habari kwa kutoa taarifa ya kazi zinazofanywa na Wizara hiyo. 

Nao viongozi wa Wizara hiyo wakitoa michango yao walieleza mafanikio yaliyopatikana katika kuimarisha sekta ya utalii hapa nchini huku wakieleza kwamba licha ya kuwepo kwa ugonjwa wa COVID 19, ulioikumba dunia nzima lakini makusanyo katika sekta hiyo yaliweza kuimarika.

Viongozi hao walieleza hatua ambazo zinachukuliwa katika kuhakikisha kuna kuwa na mfumo maalum wa kukusanya mapato kwa njia ya kielektroniki kwakushirikiana na Ofisi ya Rais Fedha na Mipango.

Pia, viongozi hao walieleza jinsi Mji Mkongwe wa Zanzibar utakavyokuwa na mvuto na haiba yake badaa ya baada ya miradi kadhaa iliyopangwa kutekelezwa.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.