Habari za Punde

SMZ Kuungwa Mkono Kiuchumi na Kimaendeleo na Nchi za Nordic ni Faraja Kubwa : Dk Hussein Mwinyi

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali  Mwinyi akizungumza na  Ujumbe wa Mabalozi  kutoka Nchi za Nordic  (kutoka kulia) Balozi Elizabeth Jocobse Nchini Norway,Balozi Anders Sjoberg nchini Sweden,Balozi Mette Nargaard Dissing-Spandet nchini Denmark na Balozi Ritta Swan Nchini Finland (hayupo pichani)  walipofika Ikulu Jijini Zanzibar leo. 
Mabalozi kutoka Nchi za Nordic wakifuatilia kwa makini wakati wa Mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali Mwinyi (hayupi pichani) yaliyofanyika Ikulu Jijini Zanzibar leo (kutoka kulia) Balozi Elizabeth Jocobse Nchini Norway,Balozi Anders Sjoberg nchini Sweden,Balozi Mette Nargaard Dissing-Spandet nchini Denmark na Balozi Ritta Swan Nchini Finland
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ali  Mwinyi alipokuwa akiagana na    Ujumbe wa Mabalozi  kutoka Nchi za Nordic ikiwemo Denmark,Finland,Norway na Sweden walipofika Ikulu jijini Zanzibar baada ya mazungumzo yao yaliyofanyika leo

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameeleza kuwa azma ya nchi za Denmark, Finland, Norway na Sweden ya kuendelea kuiunga mkono Zanzibar kiuchumi na kimaendeleo inaleta faraja.

Rais Dk. Mwinyi alieleza hayo leo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Mabalozi wa nchi hizo akiwemo Balozi  Mette Norgaard Dissing-Spandet kutoka nchini Denmark, Balozi Riitta Swan kutoka nchini Finland, Balozi Anders Sjoberg kutoka nchini Sweden na Balozi Elizabeth Jacobse kutoka Norway.

Katika maelezo yake Rais Dk. Mwinyi aliwaeleza Mabalozi hao hatua za makusudi zilizochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Nane katika kuuimarisha uchumi na kukuza maendeleo ikiwa ni pamoja na kuanzisha uchumi wa Buluu.

Aidha, Rais Dk. Mwinyi aliwaleza Mabalozi hao juhudi za makusudi zilizochukuliwa na Serikali katika kuimarisha mazingira ya uwekezaji ikiwa ni pamoja na kuweka Sera na sheria rafiki na kuanzisha kituo maalum cha uwekezaji ambacho kitawahushisha watendaji wote kwa pamoja “One Stop Center”.

Rais Dk. Mwinyi alitoa shukurani kwa utayari waliouonesha Mabalozi hao kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha utalii, afya, elimu, uchumi wa buluu, sekta ya nishati, viwanda, utoaji wa mafunzo kwa wafanyakazi na uhifadhi wa mazingira na mengineyo.

Kwa upande wa sekta ya afya, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa itakuwa ni vyema iwapo nchi hizo zitaisadia Zanzibar katika uimarishaji wa mifumo na ujenzi wa miundombinu ya afya.

Aidha, aliwataka mabalozi hao kushirikiana nja Serikali katika utekelezaji wa azma ya Serikali iliyopo ya kuanzisha Bima ya Afya, kamka hatua muhimu ya kupunguza gharama za uendeleshaji wa sekta hiyo.

Kadhalika, Rais Dk. Mwinyi alieleza juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kuimatrisha sekta ya utaliii ambayo ndio muhimili mkuuu wa uchumi wa zanzibar.

Alifahamisha kwamba kuzuka kwa maradhi ya COVID 19 kumeathiri sana maendeleo ya sekta hiyo na hatimae kuathiri kasi ya uchumi wa Zanzibar na ukusanyaji wa mapato na kuzitaka nchi hizo kuunga mkono juhudi katika kuimarisha sekta hiyo.

Alisema kwamba Serikali yake imejipanga kushirikiana na sekta binafsi na washirika wa maendeleo hasa katika kuziendeleza sekta zote muhimu za kiuchumi na kijamii na kutoa nafasi kwa wawekezaji kutoka nchi mbali mbali kuja kuekeza Zanzibar.

Mabalozi hao wote walitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Mwinyi kwa ushindi wake mkubwa alioupata katika uchaguzi mkuu uliopita wa mwaka 2020 na kumuweza kuiongoza Zanzibar chini ya Serikali ya Umoja wa Kitaifa ambayo imeanza kupata mafanikio makubwa.

Mabalozi hao pia, walieleza kufarajika na mwanga wa matumaini ya Zanzibar kupata maendeleo ya haraka kutokana na kasi ya uongozi wa Rais Dk. Mwinyi huku wakieleza matarajio yao makubwa ya kuimarika kiuchumi, kisiasa na kijamii.

Katika mazungumzo hayo Balozi wa  Denmark nchini Tanzania Mette Norgaard Dissing-Spandet alimueleza Rais Dk. Mwinyi azma ya nchi yake kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuendeleza miradi mbali mbali ya maendelo ikiwemo miradi katika sekta ya afya.

Nae Balozi Riitta Swan kutoka nchini Finland alimpongeza Rais Dk. Mwinyi kwa Serikali anayoiongoza kuja na Sera za uchumi wa buluu na kueleza kuwa hatua hiyo itaipa kwa kiasi kikubwa Zanzibar kutokana na mazingira yake sambamba na kuwepo vyanzo vingi vya uchumi huo.

Hivyo, Balozi Swan alimuhakikishia Rais Dk. Mwinyi kwamba Serikali yake itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kuimarisha uchumi wa Buluu.

Balozi wa Anders Sjoberg kutoka nchini Sweden  alimueleza Rais Dk. Mwinyi kuwa nchi yake itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo miradi ya elimu, mazingira

Nae Balozi wa Norway  Elizabeth Jacobse alieleza azma ya Serikali yake kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuendeleza sekta ya nishati hasa katika kuliimarisha Shirika la Umeme la Zanzibar (ZECO) pamoja na kuuimarisha Mfuko wa TASAF.

 

Wakati huo huo, Rais Dk. Mwinyi alikutana na Timu ya Madaktari kutoka China waliopo Zanzibar wakiongoza na  Wang Yiming ambapo aliwapongeza kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kutoa huduma kwa jamii kwa miaka mingi.

 

Rais Dk. Mwinyi aliieleza timu hiyo ya Madaktari kwamba wananachi wa Zanzibar wanafurahishwa na huduma zao wanaozitoa kwa jamii huku akieleza juhudi wanazozichukua za kutoa mafunzo kwa madaktari wazalendo kwamba hatua hiyo imekuwa ikileta tija kubwa kwa Taifa.

 

Nao ujumbe huo kupitia kiongozi wao Wang Yiming alieleza kuwa timu hiyo ya 30 ya Madaktari kutoka nchini china jumla yao ni 21 wakiwemo madaktari 18 ambao wanatoa huduma katika hospitali ya Mnazi Mmoja na Hospitali ya Abdalla Mzee.

 

Wang Ying alieleza kwamba mbali ya kutoka huduma katika Hospitali hizo kubwa hapa Zanzibar pia, wamekwua wakitoa huduma za afya katika jamii zikiwemo hospitali ndogo ndogo ikiwemo kutoa dawa, tiba hasa katika siku za mwisho wa wiki pamoja na kutoa mafunzo ya udaktari kwa madaktari wazalendo.

 

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.