Habari za Punde

Naibu Waziri Dkt.Mabula Aitaka Chemba Kuaza Mkakati wa Kuandaa Mpango Kabambe.

Naibu Waziri wa Ardhi Dkt Angeline Mabula akizungumza na viongozi pamoja na watendaji wa sekta ya ardhi wilaya ya Chemba mkoani Dodoma akiwa katika ziara yake ya kukagua utendaji kazi wa sekta ya ardhi wilayani humo
 Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Dodoma Thadei Kabonge akizungumza wakati wa kikao kati ya Naibu Waziri wa Ardhi Dkt Angeline Mabula na watumishi wa sekta ya ardhi katika halmashauri ya wilaya ya Chemba
Sehemu ya watendaji wa sekta ya ardhi katika halmashauri ya wilaya ya Chemba mkoani Dodoma wakifuatilia maekekezo ya Naibu Waziri wa Ardhi Dkt Angeline Mabula wakati wa ziara yake wilayani humo kukagua utendaji kazi wa sekta ya ardhi

Na Munir Shemweta, CHEMBA

Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula ameitaka halmashauri ya wilaya ya Chemba mkoani Dodoma kuanza mikakati ya kuandaa Mpango Kabambe katika halamashauri hiyo.

Dkt Mabula alisema hayo tarehe 21 Septemba 2021 wakati wa ziara yake ya kukagua utendaji kazi wa sekta ya ardhi katika mkoa wa Dodoma.

Alisema, wilaya ya Chemba, Chamwino pamoja na Bahi ziko ziko katika uso wa jiji la Dodoma hivyo ni lazima ziwe na mipango katika upangaji miji ili kuepuka ujenzi holela kushamiri.

‘’Bila kuwa na mpango Kabambe huwezi kuwa salama, mko katika high way halafu mji umekaa tu bila kuwa na mpangilio na Chemba inaweza kunufaika na makao makuu’’ alisema Dkt Mabula.

Naibu Waziri wa Ardhi ameitaka halmashauri ya wilaya ya Chemba kuanza utaratibu wa kuandaa mpango huo kwa kuandika andiko la kuomba fedha Wizarani ili kupanga, kupima na kumilikisha maeneo yake.

Aidha, Dkt Mabula ameitaka halmashauri ya wilaya ya Chemba mkoani Dodoma kuanzaa kuandaa pia maeneo kwa ajili ya uwawekezaji  kwa kuyapima ili wawekezaji watakapokuja wasipate tabu ya kupata maeneo.

Alisema, halamashauri  hiyo ikiandaa maenneo ya uwekezaji mapema itakuwa ni fursa kwa wawekezaji kutohangaika wakati watakapoenda kuwekeza wilayani humo.

Sambamba na hayo, Dkt Mabula alisikitishwa na idara ya ardhi katika halmashauri ya wilaya ya Chemba kuandaa hati chache katika kipindi cha mwaka mmoja ambapo halmashauri hiyo imeweza kuandaa jumla ya hati 120.

‘’Huwezi kuandaa hati 120 kwa mwaka mzima na hii haiwezekani na nataka kila mwezi muandae hati zisizopungua mia moja na nakuagiza kamishna mwezi ujao nipate mwenendo wa hati katika halmashauri hii’’ alisema Dkt Mabula.

Kwa upande wake Kamishna wa Ardhi Msaidizi mkoa wa Dodoma Thadei  Kabonge aliwataka watendaji wa sekta ya ardhi kujipanga na kuhakikisha wanafanya kazi kwa bidii kwa lengo la kumilikisha maeneo mengi ili kuiongezea serikali mapato kupitia kodi ya pango la ardhi.

‘Wizara ya ardhi imejipanga kuhakikisha inapanga, kupima na kumilikisha maeneo mapya katika mkoa wa Dodoma kupitia mradi wa Kupanga, Kupima na Kumilikisha maarufu KKK’’. Alisema Kabonge

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.