Waziri
wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Selemani Jafo hii
leo ameshiriki kwa njia ya mtandao Mkutano wa Kumi na Nane wa Mawaziri wa
Mazingira Afrika (Amcen) uliofanyika Jijini Nairobi
Nchini Kenya na kuhudhuriwa na Mawaziri wa Mazingira Afrika wapatao 42. Kushoto
ni Mhandisi Juma Limbe na Bwana Daniel Sagata kutoka Idara ya Mazingira Ofisi
ya Makamu wa Rais.
Na Lulu Mussa Dodoma.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Selemani Jafo hii leo ameshiriki kwa njia ya mtandao Mkutano wa Kumi na Nane wa Mawaziri wa Mazingira Afrika (AMCEN) uliofanyika Jijini Nairobi Nchini Kenya kwa njia ya mtandao na umehudhuriwa na Mawaziri wa Mazingira Afrika wapatao arobaini na mbili (42)
Katika mkutano huo
mada mbalimbali zimejadiliwa ikiwa ni pamoja na hali ya nchi za Afrika baada ya
athari za ugonjwa wa UVIKO-19 kwa kutekeleza program ya “Africa green stimulus programme” iliyopitishwa na Mkutano Maalumu
wa nane wa AMCEN.
Waziri Jafo amesema
Serikali ya Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan inatoa
msisitizo wa dhati katika agenda ya mazingira kwa maendeleo endelevu. Amesema
pia, Ofisi yake inaratibu Kampeni Kabambe ya Kitaifa ya Uhifadhi na Usafi wa Mazingira kwa lengo la
kunusuru taifa na majanga yatokanayo na uharibifu wa
mazingira.
Mkutano huu pia
umejadili na kuweka mwongozo wa
kuimarisha ushiriki wa Afrika katika Mikataba ya Kimataifa inayohusu Hifadhi ya
Mazingira hususan Mkutano wa 26 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Kimataifa wa
Mabadiliko ya Tabianchi utakaofanyika kuanzia tarehe 31 Oktoba hadi 12 Novemba,
2021, Glasgow, Scotland na Mkutano wa 15 wa nchi wanachama wa Mkataba wa
Kimataifa wa Hifadhi ya Bioanuai utakaofanyika kwa njia ya mtandao tarehe 11 -
15 Oktoba 2021, pamoja na Mkutano wa Baraza la Mazingira la Shirika la
mazingira la Umoja wa Mataifa utakaofanyika tarehe 28 Februari hadi 2 Machi
2022, Nairobi, Kenya.
Waziri
Jafo amesema Tanzania inapongeza
juhudi zinazofanywa na Afrika katika utekelezaji wa African green stimulus programme ikiwa ni pamoja na kuanzishwa kwa
jukwaa la kimtandao (online platform) kwa ufadhili wa Taasisi ya Maendeleo ya
Umoja wa Afrika.
Amesema Tanzania
inaafiki mapendekezo ya utafutaji fedha ili kusaidia utekelezaji kikamilifu wa African green stimulus programme pamoja
na ubadilishanaji wa taarifa na uzoefu kwa maslahi mapana ya Tanzania na Afrika
kwa ujumla.
Mkutano
wa 18 wa AMCEN pia umejadili namna bora ya kuhakikisha sekta ya mazingira inaimarishwa
kwa kutoa msukumo zaidi wa kuetelekeza makubaliano yanayofikiwa kwa kuwa yanaweza
kuleta athari za kijamii, kiuchumi, kisiasa, kisera, kisheria na kimazingira.
Aidha, Mkutano huo
umepongeza hatua zilizochukuliwa na Kikundi cha Afrika kuhusu Mabadiliko ya
tabianchi, kuendelea kusimamia maslahi ya Afrika katika Mkataba wa mabadiliko
ya tabianchi na kupitisha ujumbe mahsusi wa Afrika katika Mkutano ujao wa
Mabadiliko ya Tabianchi.
Mkutano huo pia umeunga
mkono nia ya nchi ya Misri kuwa mwenyeji wa Mkutano wa 27 wa Mkutano wa
Mabadiliko wa Tabianchi na hivyo nchi wanachama wa AMCEN zinaombwa kushirikiana
na Misri katika kufanikisha Mkutano huo.
Mkutano wa Mawaziri wa Mazingira Afrika (African Ministerial Conference on the
Environment (AMCEN) ulianzishwa rasmi mwezi Disemba 1985, ikiwa ni
moja ya maazimio ya Mkutano wa Mawaziri wa Mazingira wa Afrika uliofanyika
Cairo, Misri kwa lengo la kuhimiza masuala ya hifadhi ya mazingira katika Bara
la Afrika; kuhakikisha upatikanaji endelevu wa mahitaji muhimu ya kibinadamu;
kuhakikisha maendeleo ya kijamii na kiuchumi yanapatikana katika ngazi zote; na
kuhakikisha kuwa shughuli za kilimo zinakuwa endelevu katika kuleta usalama wa
chakula katika jamii.
No comments:
Post a Comment