Waziri wa Nishati Mhe.Januari Makamba akiongoza Ujumbe wa Tanzania katika mkutano wa 15 wa Baraza la Mawaziri la Sekta ya Nishati la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) mkutano uliofanyika Jijini Arusha leo 11 Febuari 2022.
Mawaziri
wa Sekta ya Nishati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wamekutana leo tarehe 11
February 2022 jijini Arusha, Tanzania kwaajili ya kuhudhuria Mkutano wa 15 wa Baraza
la Mawaziri la Kisekta la Nishati la Jumuiya hiyo.
Mkutano
huu ulitanguliwa na mikutano ya awali ngazi ya Wataalamu/Maafisa waandamizi
uliofanyika tarehe 8 na 9 Februari 2022 na kufuatiwa na mkutano ngazi ya
Makatibu Wakuu uliofanyika tarehe 10 Februari 2022.
Ujumbe
wa Tanzania kwenye mkutano huu umeongozwa na Waziri wa Nishati, Mhe. January
Makamba (Mb.) ambaye ameambatana na; Katibu Mkuu Wizara ya Nishati - Tanzania
Bara, Mhandisi Felschesmi Mramba; Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini
-Zanzibar; Dkt. Mgereza Miraji; Dkt. Mkurugenzi Mtendaji Shirika la Maendeleo
ya Petroli Tanzania (TPDC), Dkt. James Mataragio; Kamishna wa Petroli na Gesi
kutoka Wizara ya Nishati; na Maafisa Waandamizi kutoka Wizara ya Nishati na
Taasisi zake kwa ujumla.
Akihutubia
wakati wa ufunguzi wa mkutano huo Waziri Makamba aliwakaribisha wajumbe wa
mkutano huo nchini na kuwahakikishia kuwa mkutano utafanikiwa kuyafikia malengo
yake kufuatia uongozi imara wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mhe.
Peter Mathuki.
Vilevile
akaeleza ukanda wa Afrika Mashariki umejaaliwa rasilimali nishati za kutoka
hivyo, ni wakati sasa kwa kila nchi kuwa na mikakati imara ya kuhakikisha
nishati ya uhakika inapatikana ili kuihakikishia jamii upatikanaji wa huduma
zote zinazohitaji nishati.
“Tukiwa
tunapitia changamoto za ugonjwa wa COVID-19 tumeshuhudia namna gani nishati ya
umeme na gas zilihitajika katika kusaidia kuleta nafuu na kuokoa maisha ya
wananchi wetu” alisema Mhe. Makamba.
Naye
mwenyekiti wa mkutano huo na Waziri wa Nishati wa Jamhuri ya Kenya, Mhe. Dkt.
Monica Juma alitumia nafasi hiyo kuwashukuru Watalamu na Mkatibu Wakuu kwa
kufanya maandalizi mazuri ya Mkutano huo na kusisitiza kuwa upatikanaji wa
umeme wa uhakika ni moja ya viashiria vya kukua kwa uchumi wa nchi yeyeote.
Pia akaeleza kukua kwa uchumi husaidia kupunguza utegemeze na hivyo jitihada za makusudi zinahitajika kuziwesha Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki kufanya uzalishaji wa kutosha viwandani na katika sekta ya kilimo.
Mkutano huu wa 15 wa Baraza la Mawaziri wa Kisekta la Nishati pamoja na mambo mengine utapitia na kutoa maamuzi juu ya; Tarifa ya hali ya utekelezaji wa maagizo ya mikutano iliyopita; Hatua iliyofikiwa hadi sasa katika sekta za Nishati Jadidifu, Nishati ya Umeme na Nishati ya Mafuta; pamoja na utekelezaji wa miradi mbalimbali ya Kitaifa na Kikanda ya Sekta za Nishati inayotekelezwa ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Kadhalika mkutano huu utajadili kwa kina utekelezaji wa mradi wa kituo cha Nishati Jadidifu cha Afrika Mashariki; Mradi wa Kufua Umeme wa Nsongezi; Mradi wa kufua Umeme wa Murongo/Kigagati (14MW) na Taasisi ya Mamlaka ya udhibiti wa Nishati katika Nchi za Afrika Mashariki.
No comments:
Post a Comment