Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali
Mwinyi amepongeza utayari wa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika jitihada zake za maendeleo.
Rais Dk. Mwinyi amesema hayo leo kwa nyakati tofauti Ikulu Zanzibar wakati alipofanya mazunguzo na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania Chen Mingjian aliyekuja kujitambulisha pamoja na Balozi wa Switzerland nchini Tanzania Didier Chassot.
Mapema akizungumza na Balozi wa Jamhuri ya Watu wa China nchini Tanzania Balozi Chen Mingjian, Rais Dk. Miwnyi alisema kuwa Zanzibar inathamini sana uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na nchi hiyo na kuahidi kuuendeleza kwa manufaa ya pande zote mbili.
Rais Dk. Mwinyi alitumia fursa hiyo kuipongeza Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya afya, elimu na nyenginezo hatua ambayo imechangia kwa kiasi kikubwa kuimarika kwa uchumi wa Zanzibar.
Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Mwinyi alimueleza Balozi huyo wa China mikakati iliyowekwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha uchumi wake kupitia Sera ya Uchumi wa Buluu.
Nae Balozi Chen Mingjian alimuahidi Rais Dk. Mwinyi kwamba Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta zake za maendeleo ikiwa ni pamoja na kuunga mkono Sera yake ya uchumi wa Buluu.
Balaozi huyo wa China katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alimpongeza Rais Dk. Mwinyi kutokana na uhusiano mzuri na mashirikiano mema inayopata Ubalozi Mdogo uliopo Zanzibar.
Rais Dk. Mwinyi pia, alipata fursa ya kuzungumza na Balozi wa Switzerland nchini Tanzania Didier Chassot na kumpongeza kutokana na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika nyanja mbali mbali ikiwa ni pamoja na kusaidia sekta ya afya, kuanzisha Bima ya Afya, utawala Bora, kuijengea uwezo Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi (ZAECA), Ofisi ya Mkuu wa Mashtaka pamoja na kuzisaidia Asasi za Kiraia (NGOs) za hapa nchini.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Serikali ya Switzerland kwa kusaidia juhudi za Serikali za kuanzisha Bima ya Afya hapa Zanzibar ambapo matarajio makubwa kwamba katika mwaka ujao wa fedha Bima hiyo itaanza sambamba na kusaidia vifaa katika kupambana na ugonjwa wa UVIKO 19.
Nae Balozi wa Swiitzerland Didier Chassot alitoa ahadi kwa Rais Dk. Mwinyi kwamba Serikali yake itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika nyanja mbali mbali ikiwemo afya pamoja na Utawala Bora.
Katika maelezo yake Balozi huyo wa Switzeland alimueleza Rais Dk. Mwinyi hatua zinazochukuliwa na nchi yake katika kuhakikisha inafikia malengo iliyojiwekea katika kuisaidia Zanzibar.
Balozi Didier Chassot alitumia fursa
hiyo kumpongeza Rais Dk. Mwinyi kwa juhudi zake za kuwa karibu na Asasi za
Kiraia pamoja na juhudi zinazochukuliwa na Serikali anayoiongoza katika
kuziwekea mazingira mazuri Asasi hizo.
No comments:
Post a Comment