Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Zanzibar Dk. Hussein Ali
Mwinyi amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kuwekeza katika sekta ya elimu ili
wanafunzi wapate mazingira mazuri ya kusoma na kufanya vyema katika mitihani
yao.
Dk. Mwinyi alisema hayo leo huko katika Ikulundogo ya Pagali Kisiwani
Pemba, katika hafla ya kuwapongeza wanafunzi wa Kidato cha Nne 2021 na Sita
waliofanya vizuri katika mitihani yao
ya Kitaifa ya mwaka 2022 sambamba na kula nao
chakula kwa pamoja alichowaandalia.
Sambamba na hilo alieleza kuwa Serikali itaekeza katika vyuo vya
mafunzo ya amali kwa wale wanafunzi ambao hawakupata nafasi ya kuendelea pamoja na kuwapatia mikopo ya elimu ya juu
katika bodi zote mbili ikiwemo ile ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
jambo ambalo litawawezesha kujiendeleza kielimu.
Katika kuzithamini juhudi za wanafunzi hao Rais Dk. Mwinyi ametoa
nafasi za udhamini wa masomo “Scholaship” kwa wanafunzi 30 waliofanya vizuri
katika mitihani yao ili kuendelea na masomo katika vyuo mbali mbali.
“Kupata Division one kwa mwanafunzi sio jambo rahisi sisi tuliosoma
Tanzania tunajua lazima afanye kazi ya ziada hivyo, Serikali imeona haja ya
kuwapongeza kwa kuwapatia nafasi hizo pamoja na kuwapatia zawadi ikiwemo
Kompyuta mpakato (Lop top) kwa wanafunzi wote waliofanya vyema katika mitihani
yao wakiwemo wale wa kidato cha Sita 2022
na kidato cha Nne 2021”, alisema.
Alifahamisha kuwa kulingana na takwimu zilizotolewana ufaulu wa
wanafunzi ni dalili njema kuwa Zanzibar
itafikia malengo ya kufanya Mapinduzi makubwa katika sekta ya elimu na
kuhakikisha wanafunzi wanafaulu vizuri katika madaraja ya juu.
Rais Dk. Mwinyi alieleza kuwa kutokana na hilo ni wazi kuwa Wizara ya
Elimu na Mafunzo ya Amali imeweza
kutimiza kwa vitendo maagizo yake aliowapatia juu kukuza kiwango cha juu cha ufaulu kwa wanafunzi wa Zanzibar.
Alisema kuwa Wizara ya Elimu imekuwa ikifanya kazi kubwa na maandalizi mazuri kwa siku za usoni kwa
sababu alikaa nao na kuwaambia haridhiki na matokeo ya wanafunzi wanaofaulu
katika mitihani yao kwa sasa na lazima watafute njia mbadala.
“ Mimi binafsi nilikaa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali
nikawambia mimi siridhiki natambuwa na nyinyi hamridhiki na matokeo
tunayoyapata sasa lazima tutafute njia ya kuyafanya matokeo yanakuwa mazuri
zaidi bahati nzuri wamechukuwa juhudi
hizo nawapongeza sana”, alisema Dk. Mwinyi.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi alieleza kuwa pamoja na Wizara kuunda timu ya
wadau kufanya maboresho ya elimu na Serikali inayasubiri na itahakikisha
inayatekeleza yale ambayo yanapendekezwa katika ripoti hiyo ili hatimae Elimu
ya Zanzibar inakuwa bora zaidi na ufaulu
unakuwa mkubwa zaidi.
Hata hivyo, aliwashukuru walimu
wengine wote pamoja na walimu wakuu kwa kufanya kazi nzuri licha ya mazingira
magumu waliokuwa nayo sambamba na wazazi na walezi kwa kuwasimamia vijana wao
wasome vizuri jambo ambalo matokeo yake wamejumuika pamoja katika hafla hiyo.
Dk. Mwinyi alisema kuwa iwapo wadau wa elimu wataendeleza mwenendo
huo Serikali ya Mapinduzi Zanzibar
itafanikiwa kwani asilimia hizo
zilizotajwa 2.8 mpaka asilimia 18 hiyo
ni hatuwa nzuri zaidi kwani kuna mwanga unaonekana na kuahidi yeye na wenzake
watahakikisha kuwa hilo wanalikamata vyema ili huko mbele ya safari wazungumze
lugha nyengine ili asilimia hiyo iwe kubwa zaidi.
Aidha, aliwapongeza wadau wengine wa elimu wakiwemo wamiliki wa Skuli
binafsi ambao ni sehemu ya mafanikio yao
ambao walionesha dhahiri kama watashajiishwa basi wataweza kufanya vizuri zaidi kwa vijana.
Alisema wakati Serikali inajenga mfumo
wadau wengine wote wanayo nafasi ya kushirikiana nao ili waweze kufanya
vizuri na wakati anafanya ziara ya
kuangalia miradi mbali mbali kisiwani Pemba ameanza kuona mabadiliko makubwa
kwani kumekuwa na uwekezaji katika sekta ya elimu kwa kuwepo ujenzi wa skuli mpya za Msingi na
Sekondari na ujenzi wa madarasa mapya yanjengwa kila upande.
Aidha, Rais Dk. Mwinyi Serikali itaendelea kuwekeza kwa kuwa na skuli
nyingi zaidi ikiwemo za ghorofa sambamba na kuajiri walimu wapya ili kupunguza
uhaba wa walimu wa masomo mbali mbali
ikiwemo wa Sayansi ambazo zimeshaanza kutangazwa ili kuweza kuongezeka kwa
kiwango cha ufaulu.
“Serikali inachangamoto kubwa ya kielimu wapo idadi kubwa ya wanafunzi
katika madarasa , uhaba wa maabara , maktaba , Kompyuta na uchache wa walimu wa
Sayansi na Hisabati lakini haya yote yako katika mpango wa maendeleo wa elimu
ili kuhakikisha tunakabiliana na changamoto ya elimu na sio muda mrefu tutaona
matokeo,”alisema Rais Dk. Mwinyi.
Alifahamisha kuwa uwekezaji katika elimu ni wa muda mrefu na ukianza
kuekeza sasa unaweza kupata matokeo baadae sana lakini matokeo yake imeshaanza
kuonekana kwa hivyo hukuna sababu kwanini wasiendeleze hapo hapo badala ya
kusubiri matokeo miaka kumi ijayo.
Hata hivyo, Dk. Mwinyi aliwapongeza wadau mbali mbali wamekuwa msaada
mkubwa wa kuunga mkono serikali ya
Mapinduzi Zanzibar katika safari yake ya kielimu .
Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Leila Mohammed Mussa alieleza
hatua zitakazoendelea kuwekwa na Wizara hiyo katika kuhakikisha ufaulu
unaongezeka hasa kwa kidato cha Nne.
Nae Katibu mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Ali Khamis Juma akitowa Takwimu za uafaulu wa
wanafunzi alisema Mtihani ya kidato cha nne ulifanyika mwezi Novemba 2021 na
matokeo yake yalitoka January 2022 ambao jumla ya wanafunzi 15,569 walifanya mtihani huo na wanafunzi
4,403 wamefanikiwa kuendelea
namasomo ya kidato cha tano Julai 2022.
Alifahamisha kuwa ufaulu wao ni kati ya daraja la kwanza hadi la tatu
na ni sawa na asilimia 28.3, kati
ya wanafunzi hao ,wanafunzi 445 walipata
daraja la kwanza ambapo nisawa na
asilimia2.8 tu,ambao hawa wa hapa Pemba 137 ni miongoni mwao.
Alisema takwimu hizo zinaonesha mwenendo na mabadiliko ya kila daraja
ila tunakuahidi watahiniwa wakidato cha nne 2022 watakuja na matokeo mazuri
zaidi.
“Uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali na watendaji wote tutasimamia
utekelezaji wake na Inshaallah matokeo yatakuridhisha kwani kwetu sisi hii ni vita na hakuna sababu ya
kurudi nyuma”,alieleza.
Aliendelea kueleza kuwa Mtihani ya kidato cha sita ulifanyika mwezi
Mei 2022 na matokeo yake yalitoka Julai 2022 ambao jumla ya wanafunzi 3,683 walifanya mtihani huo na
wanafunzi 3,644 wamefanikiwa
kuendelea na masomo elimu ya juu katika
vyuo vya ndani na nje kwafani zozote
ambazo Serikali zitaweka kipaumbele kulingana na mahitaji yaSerikali.
“Kati ya wanafunzi hao,wanafunzi 693
waliopata daraja la kwanza, ambao 151
ni miongoni mwao wapo hapaleo’, alisema.
Alisema Takwimu alizozisoma zinaonesha mabadiliko ya ufaulu mwaka hadi
mwaka mfano mwaka 2020 daraja la kwanza ni 124 na mwaka 2022 ni 693, mwaka huo
huo 2020 daraja sifurini 99 na mwaka 2022 ni .
Katibu mkuu huyo aliwashukuru
wanafunzi, walimu,wazazi,walezi na wadau wa elimu mbalimbali ambao wako pamoja
nao katika kusaidia utoaji na upatikanaji wa elimu bora, ambao miongoni mwao ni
MIF,UNICEF,GPE,SIDA,KOICA,MILELE
FOUNDATION, TANZANIA CENTRE FOR EDUCATION,FAWE,UNESCO, GOOD NEIGHBOURS, WORLD
BANK, EARLY CHILHOOD MAADRASA na wengine
wengi.
Kwa upande wake Mfanyabiashara maarufu Zanzibar, Said Nassor (Bopar)
aliahidi kuwapatia zawadi za Kompyuta aina ya Laptop wanafunzi hao wote kwa
kushirikiana na Rais wa Zanzibar Dk. Hussein Mwinyi pamoja na Makamo wa Pili wa
Rais Hemed Suleiman Abdullah.
Pamoja na hayo, wanafunzi hao waliipongeza hatuwa hiyo iliochukuliwa
na Serikali ya kuwakutanisha na Rais kwa ajili ya kuwapongeza na kula nao
pamoja.
Imetayarishwa
na Idara ya Mawasiliano,
Ikulu
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment