Waziri wa Maendeleo ya Jamii Zanzibar, Mhe. Riziki Pembe Juma amesema mashindano ya ‘CRDB Bank Ngalawa Race' yaliyoandaliwa na Benki ya CRDB katika Tamasha la Kizimkazi ni mfano wa michezo ya utamaduni inayotangaza utalii visiwani humo.
Mhe. Riziki ameyasema
hayo wakati akifungua mashindano katika hafla iliyofanyika kwenye fukwe za
Kizimkazi Mkunguni ambapo mamia ya watu walijitokeza kushudia mtanange mkali wa
washiriki mahiri 20 wa mchezo wa ‘Resi za Ngalawa’ kutoka Kizimkazi Mkunguni na
Kizimkazi Dimbani.
“Ni imani yangu ni kuwa
mchezo huu utasaidia kuongeza thamani kwa fukwe zetu kwa kutoa burudani kwa
watalii wanaotembelea katika visiwa vyetu, na kutoa ajira kwa vijana wetu,”
amesema huku akitoa changamoto kwa Wizara za Michezo na Utalii kushirikiana na
Benki hiyo kuendeleza mchezo huo.
Aidha, aliishukuru
Benki ya CRDB kwa kuwa mstari wa mbele kusaidia jitihada za Serikali katika
kutatua changamoto zinazoikabili jamii na kuwaletea wananchi maendeleo.
“Niwapongeze kwa namna ambavyo mnajitoa kusaidia jamii. Ufadhili wenu katika
miradi ya maendeleo hapa Kizimkazi unaonyesha kiu mliyonayo katika kuboresha
maisha ya Watanzania.”
Kwa upande wake
Mkurugenzi wa Mawasiliano Benki ya CRDB, Tully Esther Mwambapa alisema Benki
hiyo imeamua kuwekeza katika mchezo huo wa ‘Resi za Ngalawa’ kwa kuwa ni moja
ya michezo ya asili hapa nchini ambayo ikitangazwa vizuri inaweza kutangaza
utamaduni wa Wazanzibari na kuvutia watalii kuja kutembelea nchini.
“Rais wetu Mama
Samia amefanya jitihada kubwa katika kutangaza vivutio vya utalii nchini
kupitia filamu ya ‘Royal Tour’, tukiwa Benki kiongozi na ya kizalendo nchini
tumeona ni vyema kuunga mkono jitihada hizi kupitia mashindano haya ambayo
asili yake ni katika visiwa hivi vya Zanzibari,” amebainisha.
Akielezea lengo
jengine la kuandaa mashindano hayo kwa mwaka wa pili mfululizo kupitia Tamasha
la Kizimkazi, Tully alisema Benki ya CRDB pia imedhamiria kuutumia mchezo huo
wa Resi za Ngalawa kuwawezesha vijana kiuchumi kwa kuufanya mchezo kuwa wa
kibiashara kama ilivyo michezo mingine.
“Katika kutekeleza
azma hii, mwaka huu tumekabidhi vifaa vipya kwa washiriki wote 20 vyenye jumla
ya thamani ya shilingi milioni 50 ikiwamo ngalawa za kisasa na maboya ya
uokoaji. Hii imeongeza hamasa kubwa sana kwa washiriki ambapo mashindano ya
mwaka huu yamekuwa na ushindani mkubwa.”
Washiriki hao 20
walishindana katika resi za maili 2 kwa mizunguko miwili ambapo Khatib Haji
Hamis mkaazi wa Kizimkazi Mkunguni aliibuka mshindi wa kwanza na kuondoka na
zawadi ya shilingi milioni 2.5 na boti ya uvuvi kwa ajili ya kikundi kutoka
kijiji anachotoka.
Mshindi wa pili
alikuwa Juma Ramadhani Haji kutoka kijiji cha
Kizimkazi Mkunguni ambaye aliondoka na kitita cha shilingi milioni 1, na watatu
alikuwa Muhammad Ambar Mpate kutoka kijiji cha
Kizimkazi Mkunguni ambaye aliibuka na zawadi ya shilingi laki 7, na mshindi wan
ne alikuwa Daudi Wajihi Zahor mkazi wa Kizimkazi Dimbani ambaye
alijishindia shilingi laki 5.
Mbali na mchezo wa
wa “Resi za Ngalawa”, Benki ya CRDB pia imetumia zaidi ya shilingi milioni 65
kudhamini michezo mingine katika Tamasha la Kizimkazi ikiwamo; mpira wa miguu,
mpira wa pete, nage, mbio za baiskeli, bao, kukuna nazi, kuvuta kamba, na
uchoraji.
Aidha, Benki hiyo
pia imejenga maabara ya kisasa ya sayansi iliyokamilika pamoja na vifaa vyake
katika Skuli ya Kizimkazi yenye thamani ya shilingi milioni 50. Maabara hiyo
inalenga kuhamasisha wanafunzi kusoma masomo ya sanyansi.
Tamasha la Kizimkazi linatarajiwa kufikia tamati siku ya jumamosi ya tarehe 3 Agosti 2022 ambapo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan. Miradi mbalimbali ya maendeleo inatarajiwa kukabidhiwa siku hiyo.
Kuhusu Benki ya CRDB
Benki ya CRDB ni moja benki zinazoongoza katika
ukanda wa Afrika Mashariki, inatoa huduma kwa wateja wadogo, wakati na wakubwa
ikiwamo huduma kwa wateja binafsi, huduma za hazina, huduma za bima, mikopo ya
biashara, kilimo na wajasiriamali.
Benki ya CRDB ndio benki ya kwanza nchini
Tanzania kutambuliwa na kampuni ya kimataifa ya utafiti ya Moody’s Investors
Service kuwa moja kati ya benki 10 imara na salama Afrika katika uwekezaji. Benki
ya CRDB ni Benki pekee katika ukanda wa Afrika Mashariki iliyopata usaili wa Mfuko
wa Mazingira wa Umoja wa Mataifa (GCF).
Benki ya CRDB imekuwa kiungo muhimu cha biashara Tanzania
na Burundi kwa kuhudumia wateja zaidi ya milioni 4 kupitia matawi 268, CRDB
Wakala zaidi ya 22,000, ATMs zaidi ya 550, POS zaidi ya 1,800, na Kituo cha
Huduma kwa Wateja kinachotoa huduma saa 24/7.
No comments:
Post a Comment