Habari za Punde

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Kassim Majaliwa Aaga Kundi Jengine Linalohama Ngorogoro

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akiziaga kaya 25 zenye watu 105 zinazohama kwa hiari yao kutoka katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro kuelekea kijiji cha Msomera, Handeni. Katika Ofisi za Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro Karatu, Arusha
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na wananchi wanaohama kwa hiari yao wenyewe kutoka katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro kuelekea kijiji cha Msomera, Handeni. Katika Ofisi za Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro Karatu, Arusha 
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akimkabidhi Hundi ya Malipo kwa Mkazi wa Ngorongoro na Naibu Waziri na Mbunge wa Ngorongoro Mstaafu Kaika Saning'o Ole Telele wakati akiziaga kaya 25 zenye watu 105 zinazohama kwa hiari yao kutoka katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro kuelekea kijiji cha Msomera, Handeni. Katika Ofisi za Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro Karatu, Arusha Agosti 19, 2022
 (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)


WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema mpaka kufikia Agosti 18, 2022 jumla ya kaya 1002 zenye watu 5,382 zimejiandikisha kwa hiari yao wenyewe kuhama katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro na kuelekea katika Kijiji cha Msomera, Wilayani Handeni eneo ambalo limetengwa na Serikali kwa ajili ya wakazi hao.

Ameongeza kuwa kati ya kaya hizo zilizojiandikisha tayari kaya 624 zenye watu 3,323 zimehakikiwa na kufanyiwa uthamini na kati ya kaya hizo, kaya 106 zenye watu 536 zimeshahamia kijiji cha Msomera.

Amesema Rais Samia Suluhu Hassan amepongeza uamuzi wa wananchi hao na kwamba Serikali itaendelea kuwekeza katika kuboresha miundombinu ya eneo la Msomera. “Napenda kumhakikishia Mheshimiwa Rais kwamba tulianza kuratibu, tunaendelea kuratibu na kuhakikisha wote walioamua kuhama wanapata faraja.”  

Amesema hayo leo (Ijumaa, Agosti 19, 2022) wakati akiziaga kaya 25 zenye watu 105 zinazohama kwa hiari yao wenyewe kutoka katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro kuelekea katika kijiji cha Msomera, zoezi lililofanyika kwenye Ofisi za Mamlaka ya hifadhi  hiyo.

Amesema zoezi la kuratibu uhamaji wa hiari kuelekea Msomera limefanywa kwa utaratibu mzuri ikiwa ni pamoja na kuzingatia mazingira rafiki yaliyoko katika eneo la Msomera kwa binadamu na mifugo.

“Serikali imetoa fedha kujenga miundombinu ya barabara, Umeme, maji, shule huduma za afya na huduma nyingine za kijamii ikiwemo uwezo wa umiliki wa ardhi, kilimo na malisho”.

“Lile eneo lishatengenezwa barabara na mitaa, na tumesambaza maji, na haya maji ni kwa ajili ya matumizi ya binadamu na wanyama, tumejenga, mabakuli na majosho, Tumejenga shule ya msingi kubwa, zahanati na tunataka kujenga kituo cha afya kikubwa, Endeleeni kuiamini Serikali yenu chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan”

Kwa upande wake, Moja ya wakazi wanaohama kwa hiari yao wenyewe Bi.Hulda Godwin, Ameishukuru Serikali kwa kusimamia vizuri zoezi hilo, na wanamshukuru Mheshimiwa Rais kw kuwawezesha wao kuhama kwa hiari na kuendelea kuboresha miundombinu  huku akitoa wito kwa baadhi ya watu walioko ndani ya hifadhi kuacha kuwazua au kuwapotosha wanaotaka kuhama kwa hiari yao wenyewe.

 

Naye, Aliyekuwa Mbunge na Naibu Waziri Mstaatu Bw. Ole Telele, amesema anawapongeza wote walioamua kuhaa kwakuwa ni uamuzi wa busara katika kulinda uhifadhi. ”Nawapongeza wote walioamua kuhama, mmefanya maamuzi yanayopashwa kuheshimiwa na kila mtu, hiki ni kipindi cha hiari hakuna aliyelazimishwa kuondoka.”

 

(mwisho)

 

IMETOLEWA NA:

OFISI YA WAZIRI MKUU,

S. L. P. 980,

41193 – DODOMA

IJUMAA, AGOSTI 19, 2022. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.