Habari za Punde

Serikali Yaelekeza Kiwanda Kutatua Changamoto ya Kimazingira

 

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis akitoa maelekezo wakati wa ziara ya kikazi ya katika kiwanda cha nguo cha A to Z ya kukagua na kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Serikali kuhusu kuondoa changamoto ya harufu na majitaka yanayotirirka kupita mtaro unaopita kwenye makazi ya watu.

Sehemu ya mtambo wa zamani wa kutibu majitaka katika kiwanda cha nguo cha A to Z mkoani Arusha ambao Serikali ilitoa maelekezo ufanyiwe maboresho.

Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis ameelekeza kiwanda cha nguo cha A to Z kilichpo mkoani Arusha kikamilishe ujenzi wa mtambo wa kutibu majitaka ndani ya miezi miwili.                                    

Ametoa maelekezo hayo jana alipofanya ziara ya kukagua na kufuatilia utekelezaji wa maagizo ya Serikali kuhusu kuondoa changamoto ya harufu na majitaka yanayotirirka kupita mtaro unaopita kwenye makazi ya watu.

Pia, ameelekeza Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) Kanda ya Kaskazini, wataalamu wa mazingira kutoka Ofisi za Mkuu wa Mkoa, Wilaya na Halmashauri ya jiji la Arusha kufanya kazi kwa pamoja kuhakikisha maeleekzo hayo yanatekelezwa.

“Hamuwezi kujua hizi harufu mbaya za haya majitaka yanayotoka hapa na kutiririka kwenye makazi ya watu zina athari gani, sasa ninatoa miezi miwili mkamilishe mtambo wa huu,” alisema Mhe. Khamis.

Aidha, naibu waziri huyo alisema kiwanda hicho kimekuwa kikilamikiwa na wanachi kwa muda mrefu kwa uchafuzi wa mazingira kwa kutiririsha majitaka katika makazi ya wananchi.

Hivyo, kutokana na hali hiyo Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali kwa kutoa maeleekzo kwa uongozi wa kiwanda kujenga mtambo wa kusafishia majitaka kabla ya kwenda kwenye mazingira.

Akikagua ujenzi wa mtambo huo Naibu Waziri ameridhika na utekelezaji wa mradi huo na kuwataka uongozi wa kiwanda hicho kukamilisha mara moja mtambo huo.

Alisema Serikali inawapenda wawekezaji lakini wakati huohuo inalinda afya za wananchi wake pamoja hifadhi ya mazingira lakini kiwanda hicho kimekuwa kikilamikiwa na wananchi kuhusu kuchafua mazingira.

Awali Meneja wa NEMC Kanda ya Kaskazini Bw. Lewis Nzali alisema baraza hilo limekuwa likitoa maelekezo mbalimbali ikiwemo kukipiga kiwanda hicho faini kwa uharibifu wa mazingira.

Meneja huyo alisema kuwa kutokana na hatua hizo kiwanda cha A to Z kimeweza kuanza kujenga mtambo wa kuchakata majitaka kabla ya kwenda kwenye mazingira.

Nzali aliongeza kwa kusema kuwa hata hivyo hatua hiyo imeleta mafanikio katika sekta ya uwekezaji nchini kwa kuweza kuzingatia Sheria ya Mazingira ya Mwaka 2004.

Kwa upande wake Meneja wa Kiwanda cha A to Z Bw.Sylivester Kazi aliahidi kukamilika kwa ujenzi wa mtambo huo ili kulinda afya za wananchi wanaozunguka eneo hilo.

Mtambo huo umegharimu kiasi cha sh. Bilioni 1 ambapo kukamilika kwake kutaondoa tatizo la majitaka kutiririka katika makazi ya wanachi na kusambaa kwa harufu mbaya.

Alisema baada ya kukamilika kwa mtambo huo majitaka yote yataunganishwa na mradi wa kuondosha majitaka wa Mamlaka ya Maji Safi na Majitaka Arusha (AUWSA) hayatapita tena katika mtaro huo unaotumika sasa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.