Habari za Punde

Ufunguzi wa Tawi la Benki ya NMB Ngamiani Tanga RC Mgumba Wanaoweka Fedha Kwenye Magodoro Wamepungua

MKUU wa Mkoa wa Tanga Mhe.Omari Mgumba akiweka Jiwe la Msingi la Ufunguzi wa Tawi la Benki ya NMB Ngamiani barabara ya 20 Tanga na (kulia ) Afisa Mkuu wa Wateja Wakubwa wa Benki ya NMB Bw.Alfred Shayo, hafla ya ufunguzi huo umefanyika katika Tawi hili Barabara ya 20 Ngamiani Tanga.
MKUU wa Mkoa wa Tanga Mhe.Omari Mgumba akikata utepe kuashiria Ufunguzi wa Tawi la Benki ya NMB Ngamiani barabara ya 20 Tanga na (kulia ) Afisa Mkuu wa Wateja Wakubwa wa Benki ya NMB Bw.Alfred Shayo, hafla ya ufunguzi huo umefanyika katika Tawi hili Barabara ya 20 Ngamiani Tanga.

Na Oscar Assenga,TANGA

SERIKALI mkoani Tanga imesema kwamba kusogezwa karibu kwa huduma za kibenki kumesaidia kupunguza wananchi waliokuwa wakihifadhi fedha zao kwenye magodoro jambo ambalo ilikuwa ni athari kubwa ikitokea wizi inakuwa rahisi kuweza kuibiwa au kupotea lakini pia zimekuwa salama na hivyo kuepukana na matumizi yasiyokuwa ya lazima.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga Omari Mgumba wakati akifungua tawi jipya la Benki ya NMB Ngamiani lililopo barabara ya 20 Jijini hapa katika halfa iliyokwenda sambamba na utoaji wa mabati 250 kwa shule ya msingi Masiwani.

Alisema uwepo wa tawi hilo utawawezesha wananchi kupata sehemu ambayo yataweza kuhifadhi fedha zao walizozitolea jasho na kuondoa changamoto ya uhifadhi kwenye vyungu vya maji au kulalia kwenye magodoro ambapo ikitokea moto au wizi kuiba kwake inakuwa ni rahisi lakini pia fedha zina vishawishi ukiziweka ndani matumizi yake yanakiwa ni makubwa sana.

Mkuu huyo wa mkoa alisema lakini ikiziweka benki unaweza kuokoa matumizi yasiyokuwa yalazima na unaweza kutumia hapo baadae kwenye matumizi muhimu katika mahitaji na maisha yenu.

Alisema Serikali imeweka mazingira mazuri kuhakikisha jamii ya kitanzania inapata huduma Bora sa kibenki na nafuu huku akiishukuru benki hiyo ambayo imekuwa ikiunga mkono juhudi za Serikali na hivi karibuni mlitenga zaidi ya Bilioni 200 ya mikopo kwenye sekta ya kilimo kwa riba ya asilimia 9.

"Niwapongeze Benki ya NMB kwa kuendelea kubuni huduma mpya kwa kufungua matawi mapya na zaidi ya hapo kuwajali na kuwathamini wateja bila kujali kipato pia serikali inatambua juhudi zenu za kuwawezesha wananchi kupitia mikopo ya wafanyakazi,wakulima na wafanyabiashara wakubwa na wadogo" Alisema Mkuu huyo wa Mkoa

Alisema dunia kwa sasa inakwenda kasi hususani kwa upande wa teknolojia ambazo zimerahisisha huduma za kibenki kutokutegemea matawi rasmi ingawa haiondoi ukweli kwamba kufungua matawi mapya ni kusogeza huduma karibu zaidi na wananchi ambao hauwezi kupata nje ya tawi la benki.

Mkuu huyo wa mkoa alisema pamoja na mafanikio yaliyoyapata katika kubuni huduma bora na nafuu na za haraka ikiwemo huduma mpya ya Teleza Kidigitali ambayo kwa mara ya kwanza benki inatoa mikopo midogo midogo bila kufika kwenye tawi la benki bila kuwa na dhamana unakopa mwenyewe kupitia simu ya mkononi.

Alisema mikopo hiyo itaondoa adha kwa mama mntilie,babalishe na watu wengine wenye biashara ndogondogo ambao mitaji yao haizidi laki tano hiyo inafaida kubwa ya matumizi ya teknolojia kwani wananchi wengi hususani wafanyabiashara wadogo wadogo huduma hiyo itawanufaisha sana.

Aidha alisema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu imaweka mikakati mizuri ya kupunguza umaskini kwa wananchi wake hivyo nitoe changamoto kwa ajili ya kuwasaidia na kukuza ajira kwa wananchi kuendelea kutoa mikopo kwa wakazi wa vitongoji vyote vya mkoa wa Tanga mijini na vijijini.

Awali akizungumza wakati wa halfa hiyo,Afisa Mkuu na Wateja wakubwa na Serikali wa Benki ya NMB Alfred Shayo alisema kwamba benki hiyo imekuwa ikiendeshwa kwa waledi na ufanisi na ndio maana wameweza kufikia hatua kubwa ya kimaendeleo hapa nchini

Alisema tokea Benki hiyo ilipoanzishwa mwaka 1997 imepiga hatua kubwa kwani awali ilikuwa na matawi 97 lakini sasa matawi yamefikia 227 na uzinduzi wa tawi hilo unaongezeka na kufikia 228 ni hatua kubwa imefanya ili kuweza kuwafikia wateja wake kwa karibu zaidi ambapo usogezaji karibu huduma kwa wananchi hatujaaachwa nyuma kidigitali.

"Benki ilipoanzishwa ilikuwa haina wakala wala ATM lakini kwa sasa ina na atm 762 na mawakala zaidi ya 15000 hii inaonyesha namna mnavyoishi ndoto zenu Benki ua NMB karibu yako na kujipanua kwenye mtandao na tunafanya kazi karibu na Serikali pamoja na wateja wetu kuhakikisha tunaboresha huduma na kutoa masuluhisho kwa wateja wetu"Alisema.

Alisema kwa mwaka jana wametoa trilioni 4.3 za mikopo kwa wateja wadogo wadogo kwa kilimo, biashara ndogondogo na wateja binafsi hiyo imetokana na ushirikiano mzuri walionayo kati yao na Serikali na wateja wao

"Kwa Tanga Benki wetu ya NMB ina matawi 10 kanda ya kaskazini tuna matawi 40 hii inaonyesha namna gani tupo karibu na serikali huku wananchi wanapata masuluhisho ya kuwasaidia kuendeleza shughuli za kuweza kujikwamua kiuchumi"Alisema

Alisema kwa upande wa Kilimo kama walivyosikia serikali ilitoa trilioni 1 kwa ajili ya kukopesha sekta ya kilimo kwa riba ambayo ni ya chini ya asilimia 10 huku akieleza kwamba hawakwenda kuchukua hela benki kuu Tanzania (BOT) hivyo walitenga fedha zao Bilioni 100 kwa ajili ya kukopesha kwa asilimia 10 ilipoisha na wakatenga nyengine bilioni 100 ambayo wanapokesha wakulima wadogo wadogo kwa riba ya asilimia 9.

Naye kwa upande wake Meneja wa Benki ya NMB Kanda ya Kaskazini Prosper kwa niaba ya Benki alisema kwamba wamefarijika sana kuona mwitikio kutoka kwa wananchi waliojumuika katika shughuli hiyo muhimu ya uzinduzi wa tawi hilo ambapo ni utekelezaji wa azma yao ya kusogeza huduma karibu na wana chi.

Naye kwa upande wake Meneja wa Uchumi na Takwimu Benki kuu ya Tanzania (BOT) tawi la Arusha Ernest Ndunguru alisema baadhi ya Benki zimekuwa na tabia ya kutokuweka fedha kwenye ATM mashine hususani nyakati za sikukuu na wikiendi jambo ambalo zimekuwa kero kwa wananchi wengi.

"Mimi ni moja ya wateja wa Benki hapa nchini lakini changamoto kubwa ambazo umekuwa tukikutana nazo ni kukosekana kwa fedha kwenye ATM Mashine hususani nyakati za sikukuu na wikiendi hili tatizo tunaomba lishughulikiwe "Alisema
Afisa Mkuu na Wateja wakubwa wa Benki ya NMB Alfred Shayo akizungumza wakati wa halfa hiyo
MENEJA wa Benki ya NMB Kanda ya Kaskazini Dismas Prosper akizungumza wakati wa halfa hiyo
Meneja wa Uchumi na Takwimu wa Benki Kuu ya Tanzania BOT Tawi la Arusha Ernest Ndunguru akizungumza wakati wa halfa hiyo
MENEJA wa Benki ya NMB tawi la Ngamiani Elizaberth Chawinga akizungumza wakati wa halfa hiyo
MKUU wa Mkoa wa Tanga Omari Mgumba akizungumza wakati akifungua tawi la Benki hiyo eneo la Ngamiani Jijini Tanga





No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.