Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ikitembelea Kituo cha Kufua Umeme cha Kinyerezi II. kinachozalisha umeme kwa kutumia Gesi Asilia na Mvuke.Kamati hiyo ilitembelea sehemu mbali mbali za kituo hicho ikiwemo sehemu ya kupokea taarifa za uzalishaji wa umeme na uendeshaji wa mitambo kituoni hapo na sehemu ya kuhifadhi na kuchakata maji yanayotumika kuendesha mitambo ya kutengeneza umeme kwa mvuke.
Na Dorina G. Makaya- Dar-es-Salaam.
Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Nishati na Madini imeupongeza Uongozi wa TANESCO na Watumishi wa Kituo cha
Kufua Umeme cha Kinyerezi II kinachozalisha umeme kwa kutumia Gesi Asilia na
Mvuke, kwa kudumisha usafi, kuendesha mitambo na kuikarabati kwa weledi pamoja
na kuwa na mikataba ya muda mrefu ya upatikanaji wa vipuri kutoka kwa waunda
Mitambo.
Pongezi hizo zimetolewa na
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Mhe. Dunstan
Kitandula, baada ya Kamati hiyo kutembelea Kituo hicho cha Kufua Umeme cha
Kinyerezi II, kinachozalisha umeme kwa kutumia Gesi Asilia na Mvuke chenye
uwezo wa kuzalisha 240 MW na kupata maelezo kutoka kwa Uongozi wa TANESCO na wa
Kituo hicho Oktoba 13, 2022.
Mwenyekiti huyo wa Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini ameutaka Uongozi wa TANESCO kuongeza
chanzo cha maji kwa ajili kutumika katika kuzalisha umeme kwa kuchimba kisima
cha maji ambacho kinaweza pia kutumiwa na DAWASA katika muda ambao kisima hicho
hakitumiki na Kituo cha Kinyerezi II.
Aidha, Mhe. Kitandula, ameikumbushia
TANESCO kuwa, kwa vile inajua muda wa matumizi ya mitambo iliyofungwa, ihakikishe
inajiandaa kuweka mitambo mipya pindi mitambo iliyopo itakapokwisha muda wake.
Naye Mwakilishi wa Katibu
Mkuu Wizara ya Nishati, Kamishna Msaidizi wa Masuala ya Gesi, Mha. Fakihi
Mohamed, ameishukuru kamati hiyo kwa kutembelea Kituo hicho na kuwapatia maoni
mazuri na ya kimkakati na kuahidi kuwa maoni hayo yatazingatiwa katika maandalizi
na maboresho ya mikakati ya Wizara katika kuongeza kasi ya utendaji na ufanisi
katika Sekta ya Nishati.
Vilevile, Mwakilishi wa
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania, Mha. Athanasius Nangali, ameishukuru
kamati hiyo kwa kutembelea kituo hicho na kuahidi kutekeleza maoni na
mapendekezo ya Kamati hiyo ipasavyo.
Akizungumza wakati wa ziara
ya Kamati hiyo ya Bunge kituoni hapo, Mkuu wa Matengenezo wa Kituo hicho cha
Kufua Umeme cha Kinyerezi II Mha. Benjamin Mghuna, aliielezea kamati ya Kudumu
ya Bunge ya Nishati na Madini namna Mitambo ya kuzalisha umeme kwa kutumia Gesi
Asilia na Mvuke inavyofanya kazi.
Kamati hiyo ilitembelea
kituo hicho na kujionea sehemu mbalimbali muhimu Pamoja na Mitambo inayotumika
kuzalisha umeme Kituoni hapo.
No comments:
Post a Comment