Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis akizungumza na Wananchi wa Kijiji cha Lymidati Mkoani Shinyanga wakati wa ziara ya Kamati ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta wanaoshughulikia migogoro ya Matimuzi ya Ardhi ya Vijiji 975.
Wananchi wa Kijiji cha Lyamidati Mkoani Shinyanga wakimsikiliza Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis akizugumza wakati wa ziara ya Mawaziri nane wa Wizara za Kisekta wanaoshughulikia migogoro ya matumizi ya ardhi ya vijiji 975 walipofika eneo hilo.
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Khamis Hamza Khamis amekemea tabia kwa baadhi ya wananchi kukata miti hali inayosababisha uharibifu wa mazingira.
Ametoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza na wananchi wa Kijiji
cha Lyamidati mkoani Shinyanga wakati Kamati ya Mawaziri nane wa Wizara za
Kisekta wanaoshughulikia migogoro ya matumizi ya ardhi ya vijiji 975 walipofika
eneo hilo.
“Tumepita
huko tumezunguka tumeona baadhi ya maeneo hayana hata majani lakini tumeviona
vishina vya miti kwa maana ya kwamba miti ilikuwepo lakini ilikatwa, sio kwamba
wamekuja watu kutoka mbali na kukata hii miti ni siye tuliohamia hapa ndio
tumekata miti hii,” alisema.
Mhe. Khamis aliwataka wananchi waliokata miti
katika maeneo hayo na maeneo mengine kuacha mara moja tabia hiyo na kuchukua
hatua za kuipanda tena ili kuepukana na ukosefu wa mvua na hivyo kusababisha
ukame.
Aliongeza kuwa Serikali kwa kushirikiana na
Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) na Mamlaka za Serikali za Mitaa
zitahakikisha miche inapatikana ili ipandwe katika maeneo mbalimbali nchini ili
kuboresha mazingira.
Pia aliwataka wananchi kuunga mkono juhudi za
Serikali za kuhakikisha maeneo mbalimbali yanapandwa miti na kuitunza ili iweze
kukua na hivyo mazingira kuhifadhiwa.
“Ndugu zangu wananchi uhai wetu ni hii miti tunayoina
hapa sasa nawaombeni sana ndugu zangu sisi kama Serikali tuko tayari kuwapeni
miti ili nanyi pia muipande katika yale maeneo ambayo imekatwa,” alisisitiza.
Kamati ya Mawaziri nane wa Wizara za
kisekta iko katika ziara ya kutembelea mikoa mbalimbali kwa lengo la kutoa
mrejesho wa Maamuzi ya Baraza la Mawaziri kuhususiana na utatuzi wa migogoro ya
matumizi ya ardhi katika vijiji 975.
Tayari katika awamu hii ya pili kamati
hiyo imeshatembelea na kuzungumza na wananchi wa vijiji vilivyopo katika mikoa
ya Rukwa, Katavi, Kigoma, Simiyu na Shinyanga.
No comments:
Post a Comment