Habari za Punde

Siku 558 za Mhe. Rais Samia Madarakani Misingi ya Falsafa za Uchumi Kuongoza Uchumi Zafanikiwa -- Mwenezi Shaka

 

Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka, AKIKAGUA Baadhi ya Mabanda ya Maonesho alipotembelea Maonesho ya Tatu ya Uwekezaji na Biashara Mkoa wa Pwani leo Oktoba 9, 2022, Kibaha mkoani Pwani (Picha na Fahadi Siraji CCM Makao Makuu)


KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka amesema ndani ya siku 558 tangu Rais Samia Suluhu Hassan aapishwe kuwa Rais wa Tanzania, amefanikiwa kutekeleza Misingi ya falsafa za uchumi kuongoza uchumi waTanzania

Shaka ameyasema hayo leo Oktoba 9, 2022, Kibaha mkoani Pwani alipotembelea Maonesho ya Tatu ya Uwekezaji na Biashara Mkoa wa Pwani amesema misingi hiyo ni pamoja na kuvutia wawekezaji, ushirikishaji sekta binafsi na kutumia diplomasia badala ya mabavu katika kufungua uchumi.

"Leo ni takribani siku 558 tangu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan aapishwe kuwa Rais wa nchi yetu, ambapo baada ya kiapo alitoa mwelekeo wa serikali atakayoiunda na kuiongoza kuwa, nia yake ni kuifungua nchi kiuchumi.

"Sote ni mashuhuda tumeanza kushuhudia akiruhusu misingi ya falsafa za uchumi kuongoza uchumi badala ya nguvu za kiutawala. Tumeshuhudia Rais Samia akitumia taaluma yake ya uchumi na uzoefu wake wa kiuongozi na masuala ya kidiplomasia akibadili kabisa mazingira na kasi ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo," amesema.

Shaka amesema ndani ya kipindi hicho kupitia diplomasia ya uchumi Rais Samia amefanikiwa kutafuta na kuvutia wawekezaji, kuimarisha mazingira ya biashara na kuongeza shughuli za uzalishaji zitakazoongeza ajira na mapato ya serikali.

Aidha, amesema ameimarisha mazingira ya bishara na uwekezaji kwa kuondoa urasimu, ukusanyaji kodi wa mabavu, kufanya maboresho ya sheria na mifumo mbalimbali kwa lengo la kuondoa kero kwa wafanyabiashara na wawekezaji ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ibara 22, 46 na 49.

Akiwa katika maonyesho hayo, Shaka ambaye aliambatana na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Ahmed Abbas pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Sara Msafiri ametembelea mabanda mbalimbali yanayoshiriki maonesho hayo yakiwamo ya taasisi za umma, binafsi na wajasiriamali.

Akitoa shukran, Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Ahmed Abbas alisema ziara na maonyesho hayo yamempa funzo kubwa katika kwamba akirudi mkoani kwake atakwenda kulifanyia kazi.

Akiwa katika maonyesho hayo, Shaka alitembelea mabanda mbalimbali yakiwemo ya taasisi za umma, binafsi na wajasiriamali ambao wameyatumia kuonyesha bidhaa na huduma mbalimbali wanazozitoa.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.